Waziri
wa Mambo ya ndani ya Nchi, Mhe. George Simbachawene akichukua kipande cha nyama
kavu iliyokaushwa na viungo maalum kwa ajili ya kuonja alipotembelea banda la
Wizara ya Mifugo na Uvuvi katika Maonesho ya Nane Nane, Dodoma Mwishoni mwa
Wiki. Kulia ni Afisa Mauzo wa Kampuni ya Ina’s, Hussein Juma.
Na
Mbaraka Kambona, Dodoma
Waziri
wa Mambo ya ndani ya Nchi, Mhe. George Simbachawene amewashauri wafugaji kubadilika na kufanya ufugaji wa
kisasa na wenye tija kwani ufugaji wa kienyeji pamoja na kuwa na tija ndogo, pia umekuwa ndio chanzo
kikuu cha migogoro ya ardhi na uharibifu wa Mazingira nchini.
Simbachawene
aliyasema hayo alipotembelea Maonesho ya Nane Nane yanayofanyika katika Viwanja
vya Nzuguni, Kanda ya Kati, Dodoma Mwishoni mwa wiki ( Agosti 7, 2020).
Akiwa
katika banda la Maonesho la Wizara ya Mifugo na Uvuvi, Simbachawene alisema
wafugaji wazingatie ushauri wa wataalamu na kufanya ufugaji wa kisasa ambao
unahimiza kuwa na ng’ombe wachache wenye tija kuliko kuwa na ng’ombe wengi
ambao tija yao ni ndogo.
“Ni
lazima wafugaji wafikirie kubadilika ili waende na hali halisi ya gharama za
uzalishaji, ifikie hatua wafugaji waanze kufuga kibiashara, ili mfugaji
anapotaka milioni moja au mbili aipate kwa kuuza ng’ombe mmoja na sio kuuza kundi
la ng’ombe ili aweze kupata hiyo
pesa,”alisema Simbachawene
“Unakuta
mfugaji huyo ana ng’ombe karibu 500, kwa
nyama hawafai, kwa maziwa hawafai, ng’ombe wamekonda na yeye mwenye kakonda,
kimsingi ni hasara juu ya hasara lakini pia migogoro ni mingi kati ya wakulima
na wafugaji, na wanasababisha uharibifu wa mazingira kwa kiasi kikubwa, hivyo
ni muhimu wafugaji wetu wakafundishwa na kuelekezwa kubadilika na kufuga
kisasa,”aliongeza Simbachawene
Aliendelea
kueleza kuwa Serikali na taasisi zake wamefanya kazi kubwa ya kufanya utafiti
mbalimbali wa kuboresha mifugo ikiwemo upatikanaji wa madume bora, mbegu bora
za malisho na kutenga maeneo maalum kwa ajili ya malisho.
“
Serikali imehakikisha kuwa karibu kila kanda huduma za kupandikiza mbegu bora
kwa ng’ombe majike zinapatikana hivyo ni suala la wananchi kuwa tayari kutumia
huduma hizo ili kufanya ufugaji wa kisasa,”alifafanua Waziri huyo
Aidha,
Simbachawene alitoa rai kwa viongozi kuanzia ngazi ya kata na Wilaya kuona
uwezekano wa kufanya maonesho hayo katika maeneo yao ili wananchi wanaoishi
vijijini huko waweze kuendelea kupata fursa ya kujifunza na kuangalia ubunifu
mbalimbali utakaowasaidia kuboresha ufugaji wao.
No comments:
Post a Comment