Habari za Punde

Viongozi wa Jumuiya ya Walimu wa Madrasa wakutana na Makamu wa Pili wa Rais Mhe Hemed

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  Mh. Hemed Suleiman Abdulla akizungumza na Viongozi wa Jumuiya ya Walimu wa Madrasa wanaopinga Vitendo vya udhalilishaji Zanzibar Afisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.
Mwenyekiti wa Jumuiya ya Walimu wa Madrasa wanaopinga Vitendo vya udhalilishaji Zanzibar Bwana Shaaban Rashid Ndondoe akielezea Mikakati ya Jumuiya yake katika mapambano dhidi ya vitendo vya udhalilishaji.

Picha na – OMPR – ZNZ.

Na Othman Khamis, OMPR

Serikali pamoja na Taasisi zinazosimamia masuala ya Sheria Nchini zinapaswa kuangalia kwa kina baadhi ya sheria zinazotumika  ili pale zinapochukuliwa hatua dhidi ya Mtu anayefanya makosa  maamuzi yanayotolewa yawe ya haki bila ya kusumbua upande mwengine.

Viongozi wa Jumuiya ya Walimu wa Madrasa wanaopinga Vitendo vya udhalilishaji Zanzibar walieleza hayo pale walipofanya mazungumza na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Afisini kwake Vuga Mjini Zanzibar.

Mjumbe wa Jumuiya hiyo Bibi Nyazige Saidi alisema yapo matukio ya vitendo vya uasherati katika Jamii yanayowahusisha zaidi Vijana wa Umri wa kati na pale inapotokea kuchukuliwa hatua za kisheria dhidi yao anayehusisha na tuhuma anakuwa mmoja mwengine akiendelea kubakia mitaani.

Bibi Nyazige alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba matukio hayo yanapofanyika na kuripotiwa Vituo vya Polisi kinachoendelea Mitaani ni kuibuka kwa chuki, uhasama na hata baadhi ya Watu kufanyiana Ushirikina kwa zile familia zinazohusika na matukio hayo.

Naye Katibu Mkuu wa Jumuiya hiyo ya Walimu wa Madrasa wanaopinga vitendo vya udhalilishaji Zanzibar  Bwana Omar Said Rajab alisema Jumuiya yao yenye Wanachama 50 Unguja na Pemba imekuwa ikiendeleza harakati za kupinga vitendo vya udhalilishaji katika maeneo mbali mbali Nchini.

Nd. Rajab alisema Wanachama wa Jumuiya hiyo wamekuwa wna nguvu katika harakati zao kwa kupata ushirikiano mkubwa kwa baadhi ya Wazazi licha ya mazingira magumu wanayopambana nayo kwa baadhi ya matukio wanayoyafuatilia.

Alisema Kesi za udhalilishaji zinazotokea Mitaani zimekuwa zikiripotiwa katika Vituo vya Polisi kwenye maeneo ya matukio lakini baadhi ya kesi hizo huchukuwa Zaidi ya Miaka Mitatu kutokana na baadhi ya Watendaji kukosa uaminifu na kuendeleza ubabaishaji.

Katibu Mkuu huyo wa Jumuiya hiyo ya Walimu wa Madrasa wanaopinga vitendo vya udhalilishaji Zanzibar alimueleza Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar kwamba ipo changamoto kwa baadhi ya sehemu kufuatilia matukio yanayosababisha udhalilishaji inayosababishwa na ukosefu wa usafiri pamoja a Ofisi Watendaji hao jambo ambalo huleta viklwazo wakati mwengine.

Akitoa shukrani zake kwa kazi kubwa inayoendelea kutekelezwa na Viongozi wa Jumuiya hiyo Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Mh. Hemed Suleiman Abdulla alisema Serikali itakuwa kali katika kupambana na vitendo vya udhalilishaji pale ushiriki wa Jamii utakuwa wa kina  katika kutoa ushahidi.

Mh. Hemed alisema janga hilo la udhalilishaji hivi sasa limekithiri na kuleta sura mbaya inayolitia sifa mbaya Taifa jambo ambalo Serikali Kuu italazimika kumchukulia hatua zinazostahiki Mtu ye yote atakayebainika na kutuhumiwa kufanya vitendo hivyo bila ya kujali sifa au umaarufu wa Mtu huyo.

Alisisitiza kwamba Wazazi wataendelea kubeba dhima  na dhamana ya kusimamia malezi ya Watoto wao na pale patapohitajika ushirikiano wa Taasisi na Serikali nguvu za pamoja zitajumuishwa ili kuwalinda Watoto na majaribu yanayowazunguuka.

 Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar  alibainisha kwamba Wazazi lazima wawe na jukumu la ziada ya kuchukuwa hadhari ya kuangalia mfumo wa masomo ya ziada {Tuition} kwa Watoto wao ambao baadhi yao hutumia fursa kama hiyo kwa kujiingiza katika vitendo viovu.

 

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.