Habari za Punde

Makamu wa Kwanza wa Rais, Maalim Seif afanya ziara ya kushtukiza Hospitali ya Wete Pemba



Na Mwandishi Wetu

Makamu wa kwanza wa Rais wa Zanzibar Maalim Seif Sharif Hamad ametoa muda wa wiki tatu kwa Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba Bi.Salama Mbarouk Khatib  kuhakikisha mashine ya Kuchambua damu imefungwa na kuanza kazi.

Maalim Seif ametoa kauli hio baada ya kufanya ziara ya kushtukiza katika hospitali ya Wete Mkoa wa Kaskazini Pemba.

Makamu huyo amefika katika kitengo cha damu salama na kutaka kujua namna shughuli zinavoendeshwa.

Sambamba na hilo Maalim Seif ametaka kujua ni kwanini mpaka sasa mashine mpya ya kuchambua damu  BLOOD CENTRIFUGE MACHINE bado haijafungwa na kufanya kazi kama inavyotakiwa.

Mashine hiyo yenye  uwezo wa kuchambua mpaka chupa mia moja za damu kwa siku imeletwa katika Hospitali hiyo takriban miezi miwili sasa.

Kiongozi Mkuu wa Kitengo cha Damu salama Pemba Dr. Khalfan Ali Masoud amesema mashine hiyo haijafungwa kutokana na ukosefu wa eneo sahihi.

Pamoja na utetezi huo wa Mkuu wa kitengo cha damu salama Pemba, Makamu wa kwanza wa Rais  amemuagiza Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Pemba kuhakikisha ndani ya wiki tatu tu mashine hiyo iwe imefungwa na kufanya kazi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.