Habari za Punde

MAREKANI YAAHIDI KUINUA SEKTA ZA MIFUGO NA UVUVI NCHINI

 

Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (katikati) akionesha kuvutiwa na zawadi aliyopewa na Balozi wa Marekani Nchini Tanzania, Dkt. Donald Wright (kulia) alipomtembelea ofisini kwake jijini Dodoma Aprili 14, 2021. Lengo la ziara hiyo ya Balozi Dkt. Wright ni kuimarisha ushirikiano wa nchi hizo mbili hususani katika sekta za Mifugo na Uvuvi.
Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki (mstari wa mbele kushoto) akiwa katika picha ya pamoja na Balozi wa Marekani Nchini Tanzania, Dkt. Donald Wright (kulia)  muda mfupi baada ya kumaliza mazungumzo yao yaliyofanyika jijiji Dodoma Aprili 14, 2021.


Na Mbaraka Kambona,

Serikali ya Marekani imesema itaendelea kushirikiana na Serikali ya Tanzania katika nyanja mbalimbali ikiwemo kuinua Sekta za Mifugo na Uvuvi ili ziweze kuchangia kwa kiasi kikubwa kwenye pato la Taifa.

Kauli hiyo ilitolewa na Waziri wa Mifugo na Uvuvi, Mashimba Ndaki wakati akizungumza na Waandishi wa Habari muda mfupi baada ya mazungumzo na Balozi wa Marekani Nchini Tanzania, Donald Wright yaliyofanyika jijini Dodoma Aprili 14, 2021.

Ndaki alisema kuwa katika mazungumzo yao, Balozi Wright alimuhakikishia kuwa Serikali ya Marekani ipo tayari kuleta wawekezaji kutoka Marekani ili kusisimua na kukuza sekta hizo mbili ili ziweze kutoa mchango mkubwa katika uchumi wa viwanda.

“Balozi Wright ameahidi kuleta wataalamu kutoka marekani ili kubadilishana uzoefu wa kiufundi katika sekta ya mifugo ili wafugaji wetu waweze kubadilika na kuanza kufuga kibiashara ili  kukuza kipato chao na kuongeza ajira nchini,”alisema Ndaki

Kuhusu uchumi wa Bluu ambao Serikali ya Tanzania imeanza kuwekeza, Ndaki alisema kuwa Serikali ya Marekani italeta wawekezaji kuja kuwekeza katika eneo hilo na kuisaidia Tanzania kuona tija ya uwekezaji  uchumi huo.

“Wenzetu wa Marekani wameendelea na wamewekeza sana katika uchumi wa bluu hivyo kupitia wao wanaweza kutusaidia kuimarisha eneo hilo ili sekta ya uvuvi iweze kuwa na tija zaidi kwa taifa letu,”aliongeza Ndaki

Aliendelea kusema kuwa Serikali ya Marekani ipo tayari kusaidia mapambano ya uvuvi haramu nchini ili kuhakikisha unakwisha na watu wanafanya uvuvi endelevu.

Aidha, Ndaki alimuomba Balozi huyo kuona uwezekano wa kuwapatia Watanzania nafasi ya kwenda kujifunza na kupata ujuzi kuhusu masuala ya mifugo na uvuvi katika nchi ya Marekani ili waweze kusaidia kuimarisha sekta hizo nchini.

Waziri Ndaki alisema kuwa ziara ya Balozi Wright ni kwa ajili kuimarisha ushirikiano katika sekta za mifugo na uvuvi, pia ililenga kutoa salamu za pole kutoka nchini Marekani kwa Rais wa Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe.  Samia Suluhu Hassan baada ya aliyekuwa Rais wa Tanzania, Hayati Dkt. John Pombe Magufuli kufariki.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.