Habari za Punde

Wafanyabiashara watakiwa kutumia wigo wa biashara ya mtandaoni (E-Commerce)

Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Vipimo Mohamed Mwalimu (kushoto) na Meneja Masoko wa Zantel-Zanzibar, Rukia Mtingwa (pembeni) wakimsikiliza mfanyabiashara akielezea biashara yake katika warsha ya biashara-mtandao (e-commerce) iliyofanyika Kisonge Zanzibar. 

Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Vipimo Mohamed Mwalimu akimkabidhi hundi ya Sh300,000 mshindi wa kwanza wa Shindano la vijana wanaotumia mtandao wa intaneti kujiingizia kipato, Ahmad Masoud Seif katika warsha ya biashara-mtandao (e-commerce) iliyofanyika Kisonge Zanzibar.Katikati ni Afisa Meneja Masoko Zantel-Zanzibar Rukia Mtingwa
 

Wafanyabiashara wa Zanzibar wameaswa kutumia vyema wigo wa biashara ya mtandaoni (e-commerce) kuuza na kutangaza bidhaa zao katika masoko ya ndani na nje ya nchi ili kukuza biashara zao na mitaji.

Hii ni kutokana na kuwa na uwanja mpana wa masoko ya mtandaoni kwa wafanyabiashara kuuza bidhaa na huduma zao katika muda mfupi na kwa gharama ndogo za uendeshaji.

Meneja Masoko wa  Zantel-Zanzibar, Rukia Mtingwa alisema wakati wa warsha ya Biashara-Mtandao iliyoandaliwa na Zantel kujadili fursa na changamoto za biashara za mitandaoni kwamba; wafanyabiashara watapata wateja wengi wapya kutoka masoko mapya ya mtandaoni na kuongeza mauzo yao na mitaji.

Warsha hii ya siku mbili iliyofanyika Agosti 14 na 15, 2021 Zanzibar, iliwaleta pamoja wawakilishi wa serikali, wafanyabiashara na wadau mbalimbali wa biashara. Wafanyabiashara pia walipata fursa ya kuonyesha na kutangaza bidhaa zao mbalimbali.

“Kwa kutumia simu ya mkononi au kompyuta yako, unaweza kutangaza bidhaa au huduma yako kupitia kurasa zote za mitandao ya kijamii kama WhatsApp, Instagram, Facebook, Twitter na YouTube. Pia unaweza kufungua duka lako mtandaoni na ukauza bidhaa zako katika masoko ya ndani na nje ya Zanzibar,” alisema.

Aliongeza “Biashara-mtandao pia huokoa muda na kupunguza gharama za uendeshaji. Mfano, ukiwa na duka la mtandaoni, hauna haja ya kukodi eneo la kufanyia biashara; maana unaweza kuwa na bidhaa nyumbani kwako au kwenye chombo cha usafiri na ukafanya biashara yako vizuri sana.”

Kwa walio na biashara zao masokoni, wakulima na wavuvi; wanaweza kutangaza biashara zao mtandaoni na kuelekeza wateja wao mahala walipo.

“Warsha hii ni muendelezo wa kuiishi dhamira ya Zantel, ambayo inalenga kuendeleza matumizi ya intaneti na mfumo wa kidijitali katika masoko yetu.  Tunaendelea kuboresha mtandao wetu wa intaneti kutoka kasi ya 2G na 3G na kuweka mtandao wa 4G katika baadhi ya maeneo,” alisema.

Warsha hii pia ni muendelezo wa kampeni yake kabambe ya PASUA ANGA KI ZANTEL 4G inayolenga kuelimisha wananchi juu ya umuhimu wa intaneti katika kuchochea maendeleo ya kijamii na kiuchumi.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi wa Biashara na Masoko kutoka Wizara ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda – Zanzibar, Khamis Shauri, Mkurugenzi Mtendaji wa Wakala wa Vipimo Mohamed Mwalim alisema warsha hii ya biashara za kimtandao (e-commerce) ni mwanzo mzuri wa kusaidia kukuza sekta ya biashara nchini.

Aliwaasa wafanyabiashara kutumia vyema wigo mpana wa soko la kimtandao ambalo kwa mujibu wa takwimu za za Mamlaka ya Mawasiliano (TCRA), idadi ya Watanzania wanaotumia mtandao wa intaneti imeongezeka kutoka milioni 26,83 mwaka 2020 hadi milioni 29.07 mwezi Aprili 2021.

“Biashara za mitandao zinasaidia wafanyabiashara kupata idadi kubwa ya wateja, urahisi wa kutangaza biashara, kupata bidhaa kwa manunuzi, kuokoa wakati na gharama ndogo,” alisema.

Aliongeza “Kulingana na mlipuko wa janga la ugonjwa wa mapafu (Covid-19), dunia yote imehamishia biashara zake kwenye mitandao ambapo biashara hufanyika bila mteja na muuzaji kukutana. Hivyo, ni lazima na sisi wana Zanzibar tubadilike”

Kutokana na umuhimu wa e-commerce, alisema, serikali imeweka sheria na miongozo mbalimbali ili kuweza kuboresha na kusimamia ufanyaji wa biashara za aina hiyo.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.