Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapiunduzi Mhe.Dk Hussein Ali Mwinyi Amekutana na Kuzungumza na Mlezi wa CCM Mikoa ya Kusini na Kaskazini Unguja Spika Mhe.Job Ndugai.

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na mgeni wake Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa,Mlezi wa Chama Cha Mapinduzi Mikoa ya Kusini na Kaskazini Unguja ambae pia ni Spika wa Bunge la Tanzania Mhe.Job Yustino Ndugai, alipofika Ikulu kwa mazungumzu, akiwa Zanzibar kwa ziara ya Kichama katika Mikoa wa Kusini na Kaskazini Unguja.(Picha na Ikulu)

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Hussein Ali Mwinyi amempongeza Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa na Mlezi wa CCM Mikoa ya Kusini na Kaskazini Unguja ambaye pia, ni Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Yustino Ndugai kwa ziara yake hapa Zanzibar.

Rais Dk. Mwinyi alitoa pongezi hizo leo wakati alipokutana na kufanya  mazungumzo na Mjumbe huyo wa Kamati Kuu ya CCM Taifa, Mlezi wa CCM Mkoa wa Kusini na Kaskazini Unguja na Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Job Yustino Ndugai, Ikulu Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dk. Mwinyi alimueleza Spika Ndugai kuwa ziara yake hiyo itamuwezesha kuona shughuli mbali mbali za maendeleo zinazoendelea kutekelezwa na Serikali ya Awamu ya Nane ikiwemo ujenzi wa bandari ya kisasa huko Mangwapawani pamoja na miradi mengineyo.

Akieleza kuhusu suala zima la uwekezaji, Rais Dk. Mwinyi alisema kuwa licha ya kuwepo kwa UVIKO 19, lakini mwamko wa wawekezaji walio na nia ya kuja kuekeza Zanzibar ni mkubwa sana.

Aidha, Rais Dk. Miwnyi alimueleza Spika Ndugai kuwa wawekezaji walio wengi wameweza kuvutika zaidi na kuonesha nia ya kuja kuekeza Zanzibar hasa katika visiwa vidogo vidogo, baada ya Serikali kutangaza visiwa vyake vidogo vidogo kwa ajili ya utalii.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Mwinyi alieleza kwamba juhudi za makusudi zitaendelea kuchukuliwa na Serikali katika kuhakikisha miradi inayotekelezwa inaleta manufaa kwa wananchi sambamba na kuimarisha uchumi wa Zanzibar.

Rais Dk. Mwinyi pia, alitumia fursa hiyo kueleza mikakati na mipango ya Serikali katika kuimarisha sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya elimu, lengo la kupunguza umasikini kwa kuwawekea mazingira mazuri wajasiriamali, mipango bora ya ardhi pamoja na mipango na mikakati mengineyo.

Nae Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa, Mlezi wa CCM Mkoa wa Kusini na Kaskazini Unguja ambaye pia, ni  Spika wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Job Yustino Ndugai alitoa pongezi kwa Rais Dk. Mwinyi kwa uongozi wake uliotukuka na kumueleza matarajio makubwa ya wananchi wa Zanzibar kutokana na uongozi wake bora.

Katika maelezo yake, Spika Ndugai  ambaye ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa na Mlezi wa Mikoa ya Kaskazini na Kusini Unguja kichama alimueleza Rais Dk. Mwinyi azma ya ziara yake inayoendelea katika Mikoa hiyo hapa Zanzibar.

Spika Ngugai ambaye amefika Zanzibar na kuanza ziara yake hiyo katika Mkoa wa Kaskazini Unguja mnamo Jumatatu ya Septemba 20, 2021 na anatarajia kumalizia katika Mkoa wa Kusini Unguja mnamo Septemba 24, 2021 ni kuja kuimarisha uhai wa Chama Cha Mapinduzi (CCM) hasa ikizingatiwa kwamba chama hicho kinatarajia kufanya uchaguzi wake hapo mwakani.

Aidha, Spika Ndugae alimueleza Rais Dk. Mwinyi jinsi alivyofarajika na mashirikiano mazuri yaliopo kati ya Serikali ya Mkoa wa Kaskazini, Wilaya, Kamati za Ulinzi na Usalama pamoja na Chama hatua ambayo itasaidia kwa kiasi kikubwa kufikia malengo yaliyowekwa na Serikali ya kuwaletea maendeleo wananchi.

Spika Ndugai alitumia fursa hiyo kumueleza Rais Dk. Mwinyi maeneo kadhaa aliyotembelea katika ziara yake hiyo yakiwemo maeneo ya uwekezaji wa Hoteli za kitalii, kiwanja cha ndege cha Kigunda kiliopo Nungwi, ujenzi wa Bandari ya Mkokotoni, eneo la mradi wa bandari kubwa na ya kisasa Mangapwani na maeneo mengineyo sanjari na kujionea shughuli za maendeleo zinavyotekelezwa.

Katika maelezo yake Mlezi huyo wa Mikoa ya Kaskazini na Kusini Unguja alitoa pongezi kwa mikakati na mipango iliyowekwa na Serikali ya Awamu ya Nane katika uwekezaji sambamba na kumpongeza Rais Dk. Mwinyi kwa kuja na wazo la mpango wa ujenzi wa bandari ya Mangapwani.

Spika Ndugai pia, alitumia fursa hiyo kuwapongeza Wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wanaotoka Zanzibar na kumueleza Rais Dk. Miwnyi kwamba Wabunge hao wamekuwa na nidhamu ya hali ya juu na wamekuwa wakifanya kazi vizuri za Kamati.

Sambamba na hayo, Spika Ndugai alieleza kwamba mbali ya ziara yake hiyo kichama pia, amekuwa akitumia nafasi hiyo kuwashajiisha wananchi juu ya suala zima la Sensa ya watu na makaazi ambayo inatarajiwa kufanyika hapo mwakani na kusema kwamba katika maeneo yote anayopita mapokeo juu ya jambo hilo yamekuwa mazuri.

Kitengo cha Habari

Ikulu Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi, akimsikiliza Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa, Mlezi wa Chama Cha Mapinduzi Mikoa wa Kusini na Kaskazini Unguja ambae pia ni Spika wa Bunge la Tanzania Mhe. Job Yustino Ndugai alipofika Ikulu Zanzibar kwa mazungumzo yaliofanyika katika ukumbi wa Ikulu, akiwa katika ziara yake ya Kichama Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akifuatana na mgeni wake Mjumbe wa Kamati Kuu ya CCM Taifa, Mlezi wa Chama Cha Mapinduzi Mikoa ya Kusuni na Kaskazini Unguja, ambae pia ni Spika wa Bunge la Tanzania.Mhe. Job Yustino Ndugai, wakitoka katika ukumbi wa baada ya kumaliza mazungumzo yao, akiwa Zanzibar kwa ziara ya Kichama katika Mkoa wa Kusini na Kaskazini Unguja.(Picha na Ikulu)

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.