Habari za Punde

DKT. JAFO ATETA NA WADAU WA MAZINGIRA

 

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira), Dkt. Mhe. Selemani Jafo akifungua mkutano wa wadau mbalimbali  wa mazingira wa kutoka Dodoma uliofanyika leo Januari 26, 2022 jijini hapa.

Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Dkt. Selemani Jafo leo Januari 26, 2022 amekutana na wadau wa Mazingira wa Jiji la Dodoma kutoka sekta binafsi na taasisi za Serikali kwa lengo la kuweka mikakati ya pamoja katika kuendelea kutekeleza kwa vitendo kampeni ya kuifanya Dodoma kuwa ya kijani.

Amesema ili kuwa na Kampeni endelevu ni lazima kuwe na ushirikishwaji wa wadau katika ngazi zote na kusisitiza kuwa kila mmoja aweze kutimiza wajibu wake katika kuhakikisha Dodoma inakuwa ya kijani na kutoa rai kwa jamii kutumia mvua zinazoendelea kunyesha kupanda miti kwa wingi.

“Zoezi la kukijanisha Dodoma linaendelea kwa kupanda miti maeneo mbalimbali ya jiji la Dodoma ambapo zaidi ya miti 40,000 imeshapandwa katika maeneo ya viwanja vya Chuo kikuu cha Dodoma, Mji wa Serikali Mtumba, Eneo la Medeli na maeneo ya kuzunguka Shule za Msingi na Sekondari zilizopo Dodoma” Dkt. Jafo alisisitiza

Pia ametoa wito kwa jamii kufuata taratibu na kuzingatia Sheria na kuacha kujishughulisha na shughuli zisizoendelevu ikiwemo uchomaji wa moto hovyo katika maeneo mbalimbali, hususan maeneo ambayo miti inapandwa

Nae Naibu Katibu Mkuu Ofisi ya Makamu wa Rais (Mazingira) Bw. Edward Nyamanga ametoa wito kwa sekta binafsi na Wafanyabiashara wa aina mbalimbali Jijini Dodoma kushiriki kwa dhati katika kuunga mkono serikali kwenye azma yake ya kuifanya Dodoma kuwa ya kijani na kuwa Jiji la mfano nchini katika masuala ya Hifadhi na Usafi wa mazingira.

Lengo la kuanzishwa Mpango wa kupanda miti wa kukijanisha Jiji la Dodoma ni kuhakikisha kuwa maeneo ya wazi, pembezoni mwa barabara, makazi pamoja na maeneo ya kuzunguka mashamba yanapandwa miti ili kuhifadhi mazingira na kupendezesha jiji la Dodoma. Kila eneo inapendekezwa kupandwa aina ya miti inayofaa kulingana na sehemu husika

Kwa upande wake Meya wa Jiji la Dodoma Profesa Davis Mwamfupe amesema zoezi la upandaji miti liwe endelevu na kutoa rai kwa Serikali kuepuka zoezi la upandaji miti wakati wa maadhimisho na sherehe za kitaifa pekee.

Jumla ya wadau 70 wameshiriki katika kikao hicho kilichofanyika katika Hotel ya Morena, Dodoma na kuhusisha wadau wa mazingira wa Jiji la Dodoma kutoka sekta binafsi na taasisi za Serikali.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.