Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo akizindua Kampeni ‘Urithi wa Kijani Gairo’ katika viwanja vya Shule ya Sekondari Gairo wilayani humo mkoani Morogoro Machi 30, 2022.
Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Rais (Muungano na Mazingira) Mhe. Dkt. Selemani Jafo ametoa wito kwa Wakala wa Huduma za Misitu Tanzania (TFS) kuanzisha vitalu vya miche ya miti katika shule za msingi na sekondari nchini.
Ametoa wito huo wakati akizungumza Machi 30, 2022 kwenye
uzinduzi wa Kampeni ya ‘Urithi wa Kijani Gairo’ inayotekelezwa na Wilaya ya
Gairo mkoani Morogoro na kutoa pongezi kwa uongozi wa wilaya na mkoa kwa
kuasisi kampeni hiyo.
Waziri Jafo alisema shule zikiwa na vitalu itasaidia
kupata miche ya miti kwa wingi ambayo itasambazwa, kuoteshwa na kutunzwa katika
halmashauri nchini hatua itakayoifanya Tanzania kuwa ya kijani kama maelekezo
ya Serikali yalivyotolewa.
“Ndugu zangu wa TFS niwapongeze sana kwa kuwezesha zoezi
la upandaji miti kwani nimepita maeneo mengi nimeona mmefanya kazi, niwapongeze
pia mabalozi wetu wa mazingira mnajituma sana kuikijanisha nchi yetu.
Sasa niwaombe TFS hakikisheni mnazipatia miche shule za
msingi na sekondari, lengo letu ni kuwa halmashauri zote 184 zikipanda miti
milioni moja na nusu kila moja basi tutakuwa tumepanda miti takriban milioni
276 kila mwaka,” alisema.
Waziri Jafo alisema kuwa suala la mazingira halina
mjadala ni ajenda yetu sote na ndio maana Serikali imetoa maelekezo kuhusu kila
mtu au taasisi kushiriki katika utunzaji wa mazingira.
Alisema kuwa Mkoa wa Morogoro una kila sababu ya
kuhakikisha mazingira yanatunzwa kwa kuwa kuna miradi mbalimbali ya kimkakati
ukiwemo wa Bwawa la kufua umeme la Mwalimu Nyerere na Kidatu ambalo linahitaji
maji wakati wote.
Kwa upande wake Mkuu wa Wilaya ya Gairo Jabiri Makame
alisema kampeni hiyo mbali ya kutekeleza maelekezo ya Serikali pia inalenga
kurejesha hali ya ukijani iliyokuwepo wilayani humo.
Alisema kuwa wilaya hiyo imekuwa ikikabiliwa na uharibifu
wa mazingira sambamba na kuongezeja kwa joto hivyo kukawa na umuhimu wa
kuwashirikisha wadau mbalimbali kuja na mkakati wa kurejesha asili yake kwa
kupanda miti.
Mkuu huyo wa wilaya alisema kutokana na hamasa ya wananchi kumekuwa na uhitaji mkubwa wa miche ya miti hvyo viongozi wilayani humo wanaendelea kuhamasisha wadau kuzalisha miche kwa wingi ili kukidhi mahitaji.
No comments:
Post a Comment