Na Fatma Salum- GCLA
Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali (GCLA) imetoa
elimu kwa Wanasheria na Mawakili ambao pia ni wanachama wa Chama cha Wanasheria
Tanzania (TLS) mkoani Arusha kuhusu majukumu na sheria mbalimbali zinazosimamiwa na Mamlaka
hiyo ili kuendelea kuongeza ufanisi katika utekelezaji wa sheria hizo.
Akizungumza katika mafunzo hayo Meneja wa Sayansi
Jinai Baiolojia na Vinasaba, Hadija Mwema alisema kuwa lengo la
GCLA ni kuwawezesha wanasheria kupata uelewa zaidi kuhusu utekelezaji wa sheria
za Mamlaka, utaratibu na kanuni za uchukuaji wa sampuli za sayansi jinai na
vinasaba hivyo kurahisisha majukumu yao wanapokuwa mahakamani.
“Tunaamini elimu hii
tunayoitoa kwa wanasheria itawasaidia katika kutekeleza majukumu yao kwa kuwa
wao ni miongoni mwa wanaotambulika kama mamlaka inayoweza kuomba kipimo cha
vinasaba (requesting authority) kwa mujibu wa sheria,” alieleza Hadija.
Akiwasilisha mada kuhusu majukumu ya GCLA, Meneja wa Maabara ya
Maikrobaiolojia, John Wanjala alisema kuwa wanasheria ni wadau wakubwa wa
mamlaka hiyo kwa sababu wataalamu wake
hutoa ushahidi wa kitaalamu kwenye mashauri mbalimbali mahakamani ili kusaidia
kupatikana kwa haki katika jamii.
Naye Mwanasheria wa GCLA, Abeid Kafunda aliwaeleza
mawakili hao kuwa majukumu yote ya Mamlaka hiyo hutekelezwa chini ya
sheria tatu ambazo ni Sheria ya Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali Namba
8 ya mwaka 2016, Sheria ya Usimamizi na Udhibiti wa Kemikali za Viwandani na Majumbani
Namba 3 ya mwaka 2003 na Sheria ya
Usimamizi na Udhibiti wa Vinasaba vya Binadamu Namba 8 ya mwaka 2009.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa TLS mkoani Arusha,
Wakili George Njooka aliishukuru GCLA kwa elimu waliyopatiwa na kuiomba Mamlaka
ikatoe elimu hiyo vyuoni kwa wanafunzi wanaosomea sheria hususan Shule ya
Sheria kwa Vitendo (Law School of Tanzania) kwa sababu utekelezaji wa sheria
hizo sio sehemu ya mafunzo wanapokuwa vyuoni.
Mamlaka ya Maabara ya Mkemia Mkuu wa Serikali imeweka utaratibu wa kutoa elimu kwa umma na mafunzo mbalimbali kwa wadau kuhusu majukumu yake ili kurahisisha utekelezaji wa kazi zake na kusaidia jamii kwa ujumla.
No comments:
Post a Comment