Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Alhajj Hemed Suleiman Abdulla ametoa wito kwa Taasisi na Kampuni mbali mbali kusaidia jamii ili kujikimu hasa katika kuelekea mwishoni mwa Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.
Mhe. Hemed ametoa Wito huo katika Zoezi la ugawaji wa Sadaka kwa wananchi wa Makundi mbali mbali ya Mkoa wa Kaskazini Unguja iliyoyolewa na Kampuni ya IRIS ASER ya Uturuki iliyopewa Tenda ya ujenzi wa barabara Zanzibar hafla iliyofanyika Mkokotoni Mkoa wa Kaskazini Unguja.
Amesema kitendo kilichofanywa na Kampuni hiyo ni cha kupigiwa Mfano ambapo inaonesha moyo waliokuwa nao viongozi wa Kampuni hiyo na kueleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini mchango huo na kuwataka kuendeleza zaidi kuwafikia jamii mbali mbali.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ameeleza kuwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi anafurahishwa kuona Kampuni na Taasisi mbali mbali zinatenga fedha kwa kutoa sadaka kwa wananchi wa Makundi mbali mbali hatua ambayo inaipa faraja Serikali kwa kuendelea kuziamini Taasisi hizo.
Pamoja na mambo mengine Mhe. Hemed ameeleza kuwa msaada huo unaleta upendo kwa wananchi pamoja na kuingiza mapenzi baina yao jambo ambalo limesisitizwa katika maamrisho ya Dini ya Uislamu hasa katika kipindi hichi cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhan.
Aidha Alhajji Hemed amewataka wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja kuthamini sadaka hiyo kwa kuendeleza umoja na mshikamano baina yao.
Nae Mkuu wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Mhe. Ayoub Mohamed Mahmoud ameeleza kuwa kitendo hicho ni chimbuko la wito unaotolewa na Viongozi Wakuu wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar wakiongozwa na Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi kuwataka wenye uwezo kuwasaidia wananchi wa Makundi maalum ili kuwarahisishia upatikanaji wa futari katika kipindi hichi cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.
Akitoa Shukurani kwa Niaba ya wananchi wa Mkoa wa Kaskazini Unguja Maalim Haji Haji ameishukuru Kampuni ya IRIS ASER kwa kutoa Sadaka hiyo na kuwataka wahisani wengine kujitokeza kutoa sadaka zao katika Mkoa wa Kaskazini akieleza kuwa Mkoa huo una wahitaji wengi wenye hali duni za kimaisha.
Katika hafla hiyo Mhe. Hemed amekabidhi vyeti na Nishani kwa wanafunzi waliopata nafasi ya kwanza kwa juzuu mbali mbali kwenye mashindano ya kuhifadhi Qur-an kwa Mkoa wa Kaskazini Unguja yaliyofanyika Katika Mwezi huu Mtukufu wa Ramadhan.
No comments:
Post a Comment