Habari za Punde

Kuweni Wazalendo, Tumikieni Taifa kwa Kuacha Alama. - WAZIRI NAPE

 

Waziri wa Habari Mawasiliano, Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye (Mb) akizungumza wakati wa mkutano wake na wafanyakazi wa Wizara hiyo uliofanyika leo Aprili 30, 2022 jijini Dodoma.

Na Mwandishi wetu, DODOMA

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye amewataka wafanyakazi wa Wizara anayoisimamia kubadilisha utamaduni wa kufanyakazi kwa mazoea badala yake wawe wazalendo, wapendane na kila mfanyakazi kuhalalisha nafasi aliyonayo kwa kufanya kazi kwa kuacha alama

Waziri Nape ameyazungumza hayo wakati wa kikao chake na wafanyakazi wa Wizara anayoisimamia kilichofanyika jijini Dodoma ikiwa utekelezaji wa agizo lake alillolitoa wakati wa Mkutano wa Baraza la wafanyakazi wa Wizara hiyo lililofanyika mwezi Machi mwaka huu.

“Kila mmoja wetu ahalalishe uwepo wake katika nafasi yake, acheni kufanya kazi kwa mazoea, twendeni tukafanye kazi kwa kuacha alama, na kila mmoja wetu akiweka nia inawezekana na Wizara yetu itafanya vizuri zaidi”, Amezungumza Waziri Nape

Ameongeza kuwa Wizara hiyo ina jukumu kubwa la kuwatumikia wananchi na Taifa kwa ujumla kwa kuhakikisha inalipeleka Taifa sambamba na mabadiliko ya dunia katika matumizi ya Teknolojia ya Habari na Mawasiliano pamoja na kuhabarisha na kuelimisha umma kidijitali

Kwa kuzingatia hilo, Waziri Nape amezitaka Idara zinazosimamia miradi ya Kitaifa inayotekelezwa chini ya Wizara hiyo kuhakikisha inawajengea uwezo watumishi wote kuhusu Mkongo wa Taifa wa Mawasiliano, Mfumo wa Anwani za Makazi na Mradi wa Tanzania ya Kidijitali ili waifahamu miradi hiyo na kuwa mabalozi wazuri kwa wadau wa nje ya Wizara

Katika hatua nyingine, Waziri Nape amewataka wafanyakazi wa Wizara hiyo kuona fahari kuitumikia Wizara hiyo na kila mmoja kumuona mwenzake ni zawadi kwake ili kwa pamoja wafurahie kazi wanazozifanya na mwisho wa siku wajivunie kuitumikia Wizara na kuacha alama

“Undugu ni kufaana, huku tunapokutana kwenye kazi ndio tunatengeneza familia, tusitafute fedha tukasahau utu na kuishi, tuheshimiane, tuhurumiane na tupendane, sisi kama viongozi wenu tutaendelea kusisitiza haki kwenye maeneo ya utawala”, amesisitiza Waziri huyo

Aidha, Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Jim Yonazi amesema kwake ni wajibu na nia ya dhati kutengeneza mazingira bora ya utendaji kazi kwa watumishi wa Wizara hiyo ili wafanye kazi kwa furaha bila msongo wa mawazo na kuweza kutafakari vema na kuleta ubunifu katika utekelezaji wa majukumu yao.

Imetolewa na Kitengo cha Mawasiliano Serikalini

Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari

Katibu Mkuu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Dkt. Jim Yonazi akizungumza wakati wa mkutano wa Waziri wa Wizara hiyo Mhe. Nape Nnauye (hayupo pichani) na wafanyakazi wa Wizara hiyo uliofanyika jijini Dodoma.

Waziri wa Habari Mawasiliano, Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye (Mb) akifurahia jambo na Katibu Mkuu wa Wizara hiyo, Dkt. Jim Yonazi wakati wa mkutano wake na wafanyakazi wa Wizara hiyo uliofanyika jijini Dodoma.

Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimali Watu wa Wizara ya Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Bi. Teddy Njau akizungumza wakati wa mkutano wa Waziri wa Wizara hiyo Mhe. Nape Nnauye (hayupo pichani) na wafanyakazi wa Wizara hiyo uliofanyika jijini Dodoma.

Mwenyekiti TUGHE wa Tawi la Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Laurencia Masigo akizungumza wakati wa mkutano wa Waziri wa Wizara hiyo Mhe. Nape Nnauye (hayupo pichani) na wafanyakazi wa Wizara hiyo uliofanyika jijini Dodoma.

Dkt. Revocatus Baltazar kutoka ofisi ya Mganga Mkuu wa jiji la Dodoma akitoa mada kuhusu magonjwa yasiyoambukiza wakati wa mkutano wa Waziri wa Wizara wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye (hayupo pichani) na wafanyakazi wa Wizara hiyo uliofanyika jijini Dodoma.

Waziri wa Habari, Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Nape Nnauye (aliyeketi katikati) akiwa katika picha ya pamoja na wajumbe wa Baraza la wafanyakazi la Wizara hiyo baada ya mkutano wake na wafanyakazi wa Wizara hiyo uliofanyika Aprili 30, 2022 jijini Dodoma.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.