Habari za Punde

Waziri Balozi Mulamula Amuaga Balozi wa Ubelgiji.

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akiwa na Balozi wa Ubelgiji nchini Mhe. Peter Van Acker katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam.
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akizungumza na Balozi wa Ubelgiji nchini Mhe. Peter Van Acker katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam
Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula akimkabidhi  Balozi wa Ubelgiji nchini Mhe. Peter Van Acker  zawadi ya picha

Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Balozi Liberata Mulamula (Mb) ameagana na Balozi wa Ubelgiji nchini Mhe. Peter Van Acker ambaye amemaliza muda wake wa uwakilishi hapa nchini.

Akizungumza na Mhe. Balozi Peter walipokutana katika Ofisi Ndogo za Wizara Jijini Dar es Salaam, Waziri Mulamula amesema Tanzania na Ubelgiji zimekuwa na uhusiano wa karibu tangu nchi hiyo ilipofungua Ubalozi wake hapa nchini mwaka 1980.

“Uhusiano kati ya Tanzania na Ubelgiji umekuwa unakuwa na kuimarika………. kupitia awamu zote za serikali tumeshuhudia uwepo wa mipango ya maendeleo katika sekta za maji, elimu , nishati pamoja na biashara na uwekezaji,” amesema Balozi Mulamula.

Waziri Mulamula ampongeza Mhe. Balozi kwa kumaliza utumishi wake nchini na kuacha uhusiano kati ya Tanzania na Ubelgiji ukiwa imara.

Balozi Mulamula amesema pamoja na kwamba Balozi Peter anaondoka nchini amemhakikishia kuwa kundi la wafanyabiashara kutoka Ubelgiji litakuja nchini mwaka huu ikiwa ni mwendelezo wa kukuza ushirikiano wa kibiashara na uwekezaji.

Kwa upande wake, Balozi wa Ubelgiji nchini, Mhe. Peter Van Acker ameongelea kuridhishwa kwake na uhusiano uliopo baina ya Ubelgiji na Tanzania na kuahidi kuwa balozi mwema wa Tanzania.

“Nimeishi vizuri hapa Tanzania na nimefurahia kuwa hapa wakati wote wa uwakilishi wangu, kuna mengi ya kujivunia kufanya kazi Tanzania……asante sana, amesema Balozi Acker.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.