Habari za Punde

Tanga Uwasa Yapongezwa kwa Utekelezaji wa Miradi ya Maji

Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (Tanga Uwasa) Mhandisi Geofrey Hilly akionyesha katika ramani muonekano wa ujezi unaoendelea wa mradi wa kuboresha hali ya upatikanaji wa maji katika mji wa Tanga uliopo kwenye eneo la Mowe.
Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (Tanga Uwasa) Mhandisi Geofrey Hilly (katikati) akizungumza jambo na mstahiki meya wa jiji la Tanga Abdurahman Shillow (kushoto) pamoja Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi CCM wilaya ya Tanga Meja Mstaafu Hamis Mkoba wakiwa katika ziara ya kutembelea mradi wa maji unaotekelezwa na mamlaka hiyo.
Mkuu wa wilaya ya Tanga Hashim Mgandilwa akizungumza mara baada ya kutembelea mradi wa kuboresha hali ya upatikanaji wa maji katika eneo la Mowe unaotekelezwa na mamlaka ya maji safi na usafi wa mazingira (Tanga Uwasa)

Na Oscar Assenga,TANGA

MAMLAKA Maji safi na Usafi wa Mazingira (Tanga uwasa) imepongezwa kwa namna inavyoendelea kutekeleza na kuboresha mradi wa kuongeza huduma ya maji kwa wananchi katika Mtambo uliopo Mowe unaoghalimu kiasi cha shilingi Bilioni 9.18 ambapo kwa sasa upo katka hatua nzuri ya utekelezaji ukitarajiwa kukamilika mwanzoni mwa mwaka 2023. 

Pongezi hizo zilitolewa na Kamati ya Siasa ya CCM pamoja na kamati ya ulinzi na usalama ya wilaya ya Tanga ikiongozwa na Mwenyekiti wake Mkuu wa wilaya ya Tanga Hashimu Mgandilwa wakati ilipofanya ziara kutembelea bwawa la Mabayani pamoja na eneo la Mowe kwenye mtambo wa kusafishia maji ambapo mradi huo utakapokamilika  unatarajiwa kuboresha huduma ya maji ikiwemo pembezoni mwa jiji la Tanga pamoja na wilaya za Pangani na Muheza. 

Akizungumza mara baada ya kutembelea na kujionea mradi huo pamoja na Bwawa la Mabayani Mkuu wa wilaya ya Tanga Hashimu Mgandilwa alimpongeza Rais Dkt. Samia Suluhu Hassani ambaye aliridhia na kutoa fedha Shilingi Bilioni 9.9  kwa ajili ya mradi huo ambao umelenga kupunguza au kuondoa kabisa adha ya maji iliyopo ndani ya jiji la Tanga. 

"Tanga ni moja ya miji ambayo inakuwa kwa kasi sana, sasa ukuwaji wa mji wa Tanga unatakiwa kwenda sambamba na ukuwaji wa miundombinu mingine na hiyo ikampendeza Rais wetu Samia Suluhu Hassan kutoa fedha kwaajili ya Mradi tunaamini baada ya kukamilika kwa mradi huu sasa Tanga inakwenda kutatua kabisa tatizo la maji " alisema Mgandilwa.

Awali akizungumza wakati wa ziara hiyo Mwenyekiti wa Chama cha Mapinduzi wilaya ya Tanga (CCM)  Meja Mstaafu Hamis Mkoba ameishauri mamalaka ya maji na usafi wa mazingira (Tanga Uwasa) kuhakikisha inazidi kutatua na kuondoa kabisa changamoto ya kukatika katika kwa maji hii ikiendana sambamba na ukuwaji wa mji wa Tanga ambapo wananchi wanazidi kuongezeka.

 "Tumeridhika kama chama cha mapinduzi kwamba kazi hii inaenda vizuri, ili kusudi matatizo ya kukatika katika kwa maji yasitokee tulikuwa tunawashauri muwe na mipango ya muda mrefu sana ushauri wetu kama chama kwa mamlaka pamoja na kuwapa watu taarifa panatokea changamoto ya kukatika kwa maji lakini tunawapongeza sana Tanga Uwasa kwa jitihada nilizoziona ambazo zinaendelea vizuri kama tutaendelea hivi ninaamini Tanga tutakuwa hatuna shida ya maji" Alisema Meja Mkoba 

Naye kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Maji Safi na Usafi wa Mazingira (Tanga uwasa) Mhandisi Geofrey Hilly alisema kuwa miradi wanayoitekeleza katika kituo kikubwa cha kutibu maji cha Mowe ina lengo la kuboresha hali ya upatikanaji wa maji inaendele vizuri ambapo ifikapo mwezi January 2023 wanatarajia kuanza kuyafanyia majaribio ya kupeleka huduma ya maji kwa wananchi. 

Mamlaka hiyo kwa sasa ipo kwenye mchakato wa kuboresha mtambo wa kusafisha maji katika kituo kikubwa cha Mowe pamoja na kujenga tanki za kuhifadhia maji ambazo zitasaidia kupeleka maji kwa wananchi hata panapotokea changamoto ya kukatika kwa umeme au uzalishaji wa maji kupungua kutoka kwenye vyanzo vinavyoyegemewa . 

"Hali ya utekelezaji mradi mpaka sasa tunaenda vizuri na tunatarajia kwamba mpaka mwishoni mwa mwezi huu December na mwanzoni mwa January miradi yote itakuwa imekamilika na January mwishoni tunatatajia kufanya majaribiao ya kutumia mradi mpya ambao tumeujenga, lengo kuu hasa ni kuboresha hali ya upatikanaji wa maji kwa jiji letu la Tanga lakini pia maji haya yataweza kuhudumia mji wa Muheza pamoja na vijiji vya njiani" alisema Hilly.

Alisema kuwa changamoto ya kukatika kwa umeme inaathiri utendaji wa mamlaka hiyo katika kuwafikishia wananchi huduma ya maji ikisababisha kusimama kwa kazi za uendeshaji wa mitambo ya kuzalisha maji ambapo hata hivyo mamlaka ipo kwenye hatua za kuongea na shirika la umeme Tanzania TANESCO katika kuona njia bora ya itakayotumika kuondokana na adha hiyo.

"Kuna changamoto ya umeme kipindi hiki ambapo inasababisha mitambo yetu ishindwe kuendeshwa hivyo kusababisha upatikanaji wa maji kuwa hafifu sana, sasa hivi tuna tatizo la kukatika kwa umeme kwa takribani masaa matatu hadi matano kwa siku na inaathiri sana uendeshaji wa mitambo"

 " Kwa sasa tuna changamoto ya kutokuwa na tanki kubwa la kuhifadhia maji kwahiyo umeme ukikatika pia na hali ya upatikanaji maji baada ya masaa mawili au matatu hali inakuwa ni tete kwa wananchi lakini tuko katika mipango ya kuongea na Tanesco waangalie namna gani ya kutusaidia lakini pia sisi tupo katika mipango ya kutafuta vifaa madhubuti vya kudhibiti mapungufu ya umeme" alisema Mkurugenzi huyo. 

Bwawa la Mabayani ambalo ni moja wapo ya chanzo kikubwa kinachotegemewa na mamlaka ya maji na usafi wa mazingira (Tanga uwasa ) katika kuwahudumia wananchi wa jiji la Tanga lilianza kujengwa mnamo mwaka 1976 hadi 1978 likiwa na ujazo wa mita bilion 7.7 kwa sasa ,ambapo lina uwezo wa kuzalisha maji lita Milion 30 kwa siku. 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.