Habari za Punde

SMZ Inathamini Juhudi za Taasisi Binafsi Katika Kuisaidia Kuwafikishia Wananchi Huduma za Jamii

 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Ujumbe wa Uongozi wa Kitaifa wa Jumuiya ya Ahmadiyya Muslim  Jamaat Tanzania ukiongozwa na Amir Mbashiri Mkuu Sheikh. Tahir Mahmood (kulia kwa Rais) na Naibu Amir Sheikh.Abdulrahaman Mohammed Ame, walipofika Ikulu Jijini Zanzibar kwa mazungumzo  na kujitambulisha leo 4-2-2023, mazungumzo hayo yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Zanzibar

SERIKALI ya Mapinduzi ya Zanzibar imesema inathamini juhudi za taasisi binafsi katika kuisaidia serikali kuwafikishia wananchi huduma za jamii zikiwemo afya, elimu, maji na umeme.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi aliyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipozungumza na uongozi wa Jumiya ya Ahmadiyya Muslim Jamaat Tanzania waliofika kuzungumza naye.

Dk. Mwinyi alisema Serikali inaungamkono juhudi njema zinazofanywa na taasisi za dini kusaidia kuleta maendeleo ya nchi pamoja na kuendelea kuitangaza amani.

Aliishukuru taasisi hiyo kwa misaada wanayoitoa kwa jamii na kueleza serikali daima iko pamoja na taasisi zinazoungamkono juhudi za Serikali.

“Kipekee niishukuru taasisi yenu kwa misaada mnayoitoa kwa jamii, sisi kama serikali tuna wajibu wa kutoa huduma za jamii kwa wananchi lakini wakati mwengine hatuwezi kufanya hayo yote hutokana na uwezo wa Serikali zetu, idadi ya watu na ukubwa wa nchi, hivyo mara zote tunawashukuru wale wanaotuungamkono”. Alieleza Dk. Mwinyi.

Alisema thamani kubwa ya nchi ni kudumisha amani, na yeyote anayeihubiri amani na kujitihadi kuidumisha lazima Serikali imuunge mkono kwa kutambua umuhimu wa amani katika ustawi wa nchi.

Alieleza Serikali inawataka wananchi wote waendelee kuimarisha umoja, upendo na kuvumiliana. Hata hivyo alieleza serikali haibagui taasisi yeyote iwe ya dini, siasa au jamii muhimu itii sheria za nchi na taratibu zake.

Akizumgumza Amiiri na Mbashiri Mkuu wa Jumuiya hiyo, Sheikh Tahir Mahmood alisema Tanzania inasifika kwa amani, umoja na mshikamo wa watu wake nakueleza mara zote, serikali zote mbili za Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania nay a Mapinduzi ya Zanzibar zinajali uhuru wa kuabudu licha ya kuwepo kwa imani tofauti za dini, lakini wanaendelea kuishi kwa umoja jambo alilolieleza kwamba ni mafanikio makubwa kwa taifa.

Naye, Naibu Amir wa taasisi hiyo, Sheikh Abdul Rahman Muhammad Ame alieleza taasisi hiyo ilitoa mchango mkubwa kwa taifa tokea kuanzishwa kwake mwaka 1934, kwa baadhi ya waumini wake kina Marehemu Sheikh Kaluta Amri Abedi, Mzee Hassan Tawfiq na wengine walishirikiana na Hayati Baba wa Taifa, Mwl. Julius Kambarage Nyerere kwenye harakati za ukombozi na kuleta uhuru wa nchi.

Alisema taasisi ya Ahmadiyya Muslim Jamaat ilikua ya kwanza kuchapisha kadi za chama cha TANU kwa wakati huo kupitia mtambo wa jumuiya hiyo uliokuwepo Tabora ukichapisha gazeti la Kiswahili la jumuiya lililoitwa “Mapenzi ya Mungu”.

Aliongeza jumuiya hiyo ndio iliyobuni jina la “Tanzania” kupitia muumini wake bw. Muhammad Iqbal Dar aliekua akiishi Morogoro kwa wakati huo. Pia alieleza jumuiya hiyo ilikua ya kwanza kuitafsiri Quran kwa lugha ya kiswahili pamoja na kutoa mchango mkubwa wa kukuza Kiswahili, Afrika Mashariki baada ya kuchapisha gazeti la Kiislam kwa lugha ya hiyo ambalo alisema lilitoa hamasa kubwa wakati wa harakati za ukombozi kupitia Makala na mashairi.

Taasisi ya Ahmadiyya Muslim Jamaat Tanzania ni Jumuiya ya kimataifa yenye malengo ya kidini, ipo kwenye nchi 212 duniani kote na sasa ina zaidi ya waumini 50,000 Tanzania na imesaidia huduma za jamii kujenga vituo vya afya, maji, umeme wa jua na elimu vijijini. imeongozwa na Makhalifa wanne na watano ni Sheikh Hadhrat Mirza Masroor anaendea kuongoza hadi sasa.

IDARA YA MAWASILIANO, IKULU ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.