Habari za Punde

BALOZI MBAROUK AWATAKA VIONGOZI VIJANA KUSIMAMIA AGENDA YA KUONDOA UMASKINI

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, ambaye pia ni Katibu wa NEC - Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (SUKI) – CCM Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.) akifungua mafunzo ya uongozi kwa viongozi vijana yanayotolewa katika Chuo cha Uongozi cha Mwalimu Julius Nyerere mjini Kibaha, Pwani. 

Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, ambaye pia ni Katibu wa NEC - Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (SUKI) – CCM Mhe. Balozi Mbarouk Nassor Mbarouk (Mb.) amewaasa viongozi vijana kusimamia na kutekeleza agenda na mikakati ya kuondoa umaskini kwa vitendo. 

 

Balozi Mbarouk ametoa wito huo wakati alipokuwa akifungua mafunzo ya uongozi kwa viongozi vijana kutoka vyama vya Chama cha Mapinduzi (CCM), ANC- Afrika Kusini, SWAPO-Namibia, ZANU-PF – Zimbabwe, AMPLA – Angola, FRELIMO – Msumbiji, yanayotolewa katika Chuo cha Uongozi cha Mwalimu Julius Nyerere kilichopo Kibaha, Pwani.  

 

Balozi Mbarouk amewahimiza viongozi hao kutumia ujuzi na elimu watakayoipata katika mafunzo hayo ili kuleta mageuzi ya maendeleo kwa kutatua changamoto mbalimbali zinazoikabili jamii. 

 

“Vyama hivi rafiki vimefanya kazi nzuri ya kuleta ukombozi wa kisiasa, hivyo ni wakati muafaka sasa kwa viongozi vijana kutoka vyama hivi vikongwe barani Afrika kujikita katika kuondoa umaskini. Suala hili la kuondoa umasikini linapaswa kufanyika kwa vitendo, uadilifu na umoja kama ilivyofanyika katika kipindi cha kutafuta ukombozi,” alisema Balozi Mbarouk.

 

Kwa upande wake Mkuu wa Chuo hicho, Prof. Marselina Mvula Chijoriga alisema mafunzo hayo pamoja na masuala mengine, ni jukwaa muhimu katika kuwaunganisha viongozi hao vijana, kubadilishana mikakati na uzoefu wa namna bora ya kuongoza jamii. 

 

Pamoja na mambo menhine, Balozi Mbarouk ambaye pia ni Katibu wa NEC - Siasa na Uhusiano wa Kimataifa (SUKI) – CCM amekipongeza chama rafiki cha Kikomunisti cha China (Chinese Communist Party) kwa kuendelea kushirikiana kwa ukaribu na vyama hivyo na kufadhili baadhi ya mafunzo yanayotolewa katika Chuo hicho.  

 

Mafunzo hayo ya siku 14 (27 Machi hadi 7 Aprili 2023) yanajumuisha jumla ya washiriki 100, ambapo 26 kati yao wanatoka Tanzania.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.