Habari za Punde

Katibu Mkuu Msingwa Asisitiza Ubunifu na Ulinzi wa Maadili ya Mtanzania

Na Eleuteri Mangi, WUSM.

Katibu Mkuu Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo Bw. Gerson Msigwa amekutana na watumishi wa Idara ya Maendeleo ya Utamaduni na Sanaa ambapo amewasisitiza watumishi hao wawe wabunifu na wachukue hatua kulinda maadili ya Mtanzania.

Katibu Mkuu Bw. Msigwa amesema hayo alipokutana na kufanya kikao na watumishi hao Oktoba 9, 2023 katika ofisi ya Wizara hiyo iliyopo Mji wa Serikali Mtumba jijini Dodoma.

“Bahati nzuri eneo hili la utamaduni Mhe. Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan analipenda na kulipa kipaumbele, amekua akitusisitiza tulinde maadili yetu na anapenda kutangaza Utamaduni wetu na ndiyo maana anaitwa Chifu Hangaya. Kwetu sisi Mhe. Rais kuwa Chifu Hangaya ni fursa ya kuhakikisha ajenda yetu ya kulinda na kutangaza Utamaduni wa Taifa letu tunaisimamia vizuri” Amesema Katibu Mkuu Bw. Msigwa.

Katibu Mkuu Bw. Msigwa ameongeza kuwa Wizara kupitia Idara ya Utamaduni na Idara ya Sanaa ina wajibu wa kuwaelimisha vijana ili wajue kuwa Tanzania ina Utamaduni wake na maadili yake akiwataka vijana wawe sehemu ya kulinda na kuendeleza maadili na Utamaduni wa Taifa.

Katika hatua nyingine amewasisitiza Watumishi hao wafanye kazi kwa bidii na kumpatia ushirikiano ili kwa pamoja wajenge mazingira wezeshi ambayo yataleta furaha na ufanisi kwa watumishi hao mahala pa kazi.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.