Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Mwinyi Azungumza na Kuwapongeza kwa Juhudi Zao na Kuhakikisha Amani na Utulivu Nchini

 

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Kamanda Mkuu Dk.Hussein Ali Mwinyi alipokuwa akizungumza na  Maafisa na Askari wa Vikosi vya SMZ katika  Kambi ya Jeshi la Kujenga Uchumi Kama, Wilaya ya Magharibi "A" leo katika shamra shamra za Miaka Mitatu ya Uongozi wake .[Picha na Ikulu] 30/10/2023.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Hussein Ali Mwinyi amevinasihi vikosi vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kuendeleza uadilifu na uwajibikaji wa majukumu yao ya kila siku.

Dk. Mwinyi ambae ni Kamanda Mkuu wa Idara Maalum ya vikosi vya SMZ, alitoa nasaha hizo viwanja vya JKU – Kama, alipozungmuza na wapiganaji kwa lengo la kuwapongeza kutokana na juhudi zao za kuhakikisha amani na utulivu nchini vinaendelea kuimarishwa.

Alivitaka vikosi hivyo kuweka mbele maslahi ya nchi kwanza, uwajibikaji pamoja na kusimamia uadilifu jeshini.

Rais Dk. Mwinyi alivisisitiza vikosi hivyo juu ya suala zima la kusimamia nidhamu kwenye maeneo yao ya kazi ili kufanya kazi zao kwa uadilifu.

“Jeshi ni nidhamu ikikosekana nidhamu katika jeshi basi hapo hakuna jeshi” alikazia Rais Dk. Mwinyi.

Dk. Mwinyi pia, alivipongeza vikosi hivyo kwa jitihada zao za kutoa huduma bora kwa jamii wakiwemo Kikosi Maalum cha Kuzuia Magendo (KMKM) kupitia hospitali yao iliopo Bububu pamoja na hospitali ya JKU, Saateni kwa huduma za afya wanazozitoa kwa wananchi na nyengine za jamii vikiwemo vyuo vya amali na taaluma.

Alivitaka vikosi hivyo kuwa mfano mzuri wa kutoa huduma bora kwa raia hasa kwenye vituo vyao vya afya na taaluma vinavyohudumia jamii.

Halikadhalika, Rais Dk. Mwinyi aliwaagiza wakuu wa vikosi hivyo kuendelea kusimamia uwajibikaji ili kuwe na tofauti baina ya hospitali za jeshi na za raia ili wananchi wapate huduma bora.

Pia, Dk. Mwinyi alivieleza vikosi hivyo kuwa vinajukumu la kutoa malezi bora kwa vijana na kuhakisha wanatoa vijana wazalendo wenye uchungu wa nchi yao watakaopigania maslahi ya taifa lao.

Akizungumzia suala la kuwajengea uwezo maofisa na wapiganaji wa vikosi hivyo, Rais Dk. Mwinyi aliwataka wakuu wa vikosi hivyo kuwaongezea uwezo wa kitaaluma maofisa hao kwa kuwapatia fursa za mafuzo.

Akizungumza kwenye hafla hiyo, Waziri wa Idara Maalum ya vikosi vya SMZ, Masoud Ali Muhammed alisema, Idara Maalum ya vikosi vya SMZ zote tano zikotayari kuendeleza jukumu mama la kuimarisha na kuendeleza amani, utulivu na mshikamano uliopo nchini vinaendelea kusimama wakati taifa likiendeleza maendeleo ya watu wake.

Alisema, Idara hizo pia zitaendelea kutekeleza maagizo, maono, mipango na fikra za Kamanda Mkuu kwa utii wa hali ya juu.

Akiwasilisha risala ya vikosi vitano vya Idara Maalum ya SMZ, Katibu Mkuu wa Idara hiyo, Issa Mahafoudh Haji alisifu juhudi kubwa ya Kamanda Mkuu wa Idara Maalum ya vikosi vya SMZ, Rais Dk. Mwinyi aliyoifanya kwa vikosi hivyo.

Alimshukuru Rais Dk. Mwinyi kwa kuvishirikisha vikosi hivyo kwenye ujenzi wa miradi mikubwa ya maendeleo nchini na kueleza kuwa imewaongezea uwezo na nguvu za kiuchumi kwa kutatua baadhi ya changamoto zao.

Pia, alieleza ushiriki wao kwenye miradi hiyo, umetanua uwezo wao wa ufahamu na ujuzi wa kutekeleza majukumu yao ya kila siku pamoja na kusifu hatua ya kuwapandishia mishahara makamanda na wapiganaji kufuatia nyongeza ya mishahara aliyoitoa kwa watumishi wa umma wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Vikosi vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar vinaundwa na Jeshi la kujenga Uchumi (JKU), (KMKM), Vikosi vya Uokozi na Zimamoto, Valantia (KVZ) na Chuo cha Mafunzo.

IDARA YA MAWASILIANO, IKULU ZANZIBAR.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.