Habari za Punde

CCM Zanzibar Inahitaji Viongozi Wachapa Kazi,Wazalendo na Waadilifu- Dkt.Dimwa

Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt.Mohamed Said Dimwa,akisalimiana na Mwananchi ngugu Mussa Juma Hamad wa Shehia ya Nyerere katika hafla ya kumkabidhi nyumba iliyojengwa na Mbunge wa jimbo la Magomeni Unguja Mhe.Mwanakhamis Kassim Said.

NA IS-HAKA OMAR,ZANZIBAR.

CHAMA Chama Cha Mapinduzi(CCM)Zanzibar kimesema kinahitaji viongozi wachapakazi,wazalendo na waadilifu katika kuwatumikia Wananchi ambao ndio wenye nguvu ya mamlaka ya kukiweka madarakani kupitia michakato ya Uchaguzi wa kidemokrasia.

Kauli hiyo imetolewa na Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Dkt.Mohamed Said Dimwa wakati akikabidhi nyumba iliyojengwa na Mbunge wa Jimbo la Magomeni Mhe.Mwanakhamis Kassim Said  kwa Mwananchi wa shehia ya Nyerere ndugu Mussa Juma Hemed huko Magomeni Zanzibar.

Dkt.Dimwa,alisema viongozi wanaotekekeza kwa vitendo ahadi walizoahidi kupitia Uchaguzi mkuu uliopita wanaenda sambamba na malengo ya Chama Cha Mapinduzi katika kuwatumikia Wananchi na kwamba wanatakiwa kuongeza Kasi ya utekelezaji wa ilani ya Uchaguzi Ili CCM ishinde kwa ngazi mbali mbali katika Uchaguzi mkuu ujao.

Alieleza kuwa Wananchi wanahitaki kuona maendeleo katika majimbo yao ikiwemo huduma Bora za maji safi na salama,hospitali,skuli,barabara zenye ubora,umeme na makaazi bora ya kuishi.

Katika maelezo yake Dkt.Dimwa,alisema kuwa CCM inaendelea kutathmini na kufuatilia utendaji wa kila kiongozi wakiwemo madiwani,Wabunge na wawakilishi kwa lengo la kujiridhisha kama wanakidhi vigezo vya kuendeleza kuongoza kuwatumikia wananchi.

Kupitia hafla hiyo alimpongeza Mbunge huyo wa Jimbo la Magomeni kwa juhudi zake za kuhakikisha Mwananchi huyo anapata nyumba nzuri ya kuishi na kwamba sio kuwa ametekeleza ilani ya CCM pia ametoa sadaka kubwa itanayoongeza baraka kwa Mwenyezi Mungu.

Alisema kuwa Chama Cha Mapinduzi hakitowavumilia baadhi ya viongozi wasiotekeleza ilani ya Uchaguzi ya CCM badala yake kitatoa nafasi za kuendeleza kuongoza kutokana na uchapakazi wa kiongozi na sio umaarufu wake.

"Tunapowatumikia Wananchi kwa uadilifu kwa kutatua changamoto zao inasadia kutengeneza mazingira bora ya ushindi wa CCM wa ngazi mbali mbali katika Uchaguzi Mkuu ujao.

Nitumie nafasi hii tu kuwaeleza kuwa CCM kwa awamu hii ya Mwenyekiti wetu Rais Dkt.Samia npamoja na Rais Dk.Mwinyi,haitomuonea mtu bali tutaenda na kutoa kipaumbele kwa wale tuliolima nao mazao  juani ndio tutakaovuna na kula nao kivulini.",alisisitiza Dkt.Dimwa.

Alisemea tabia za baadhi ya makada na wanachama kupita majimbo kuanza kampeni za kuharibu sifa za viongozi waliopo madarakani kwa sasa na kueleza kuwa viongozi hao waachwe na kupewa nafasi za kuwatumikia Wananchi na kwamba wanaotaka kuwania Uongozi wasubiri muda wa Uchaguzi ufike mwaka 2025.

Naye Mbunge wa Jimbo la Magomeni Zanzibar Mhe.Mwanakhamis Kassim Said, alipongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt.Samia Suluhu Hassan pamoja na Rais wa Zanzibar Dk.Hussein Mwinyi kwa utendaji wao mzuri wa kuwaletea wananchi maendeleo.

Alisema maendeleo yaliyopatikana katika Jimbo Hilo yametokana na ushirikiano mzuri ulipo baina ya wanachama,viongozi wa ngazi za mashina hadi Mkoa ikiwemo Kamati ya Jimbo na Wananchi wote kwa ujumla.

Akizungumzia ujenzi wa nyumba ya Mwananchi huyo ndugu Mussa Juma,alisema imegharimu kiasi cha shilingi milioni 17,357,000.

Mhe.Mwanakhamis,amesema lengo la kujenga nyumba hiyo ni kuhakikisha Mwananchi huyo anaishi katika maakazi Bora kama ilivyo kwa Wananchi wengine wa Jimbo hilo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.