Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Mwinyi Azungumza na Ujumbe wa Chuo cha NDC Ikulu Zanzibar

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akizungumza na Ujumbe kutoka Chuo cha Ulinzi cha Taifa (NDC) ukiongozwa na Mkuu wa Chuo hicho Balozi Meja Generali Wilbert Augustine Ibuge, mazungumzo hayo yaliyofanyika katika ukumb Ikulu Jijini Zanzibar leo 30-4-2024
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akimsikiliza Mkuu wa Chuo cha Ulinzi cha Taifa (NDC) Balozi Meja Generali Wilbert Augustine Ibuge, akizungumza wakati walipofika Ikulu Jijini Zanzibar na ujumbe wake kwa ajili ya mazungumzo yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Zanzibar leo 30-4-2024
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Hussein Ali Mwinyi akikabidhiwa zawadi maalum kutoka kwa Mkuu wa Chuo cha Ulinzi cha Taifa (NDC) Balozi Meja Gerenali Wilbert Augustine Ibuge, baada ya kumaliza mazungumzo na ujumbe huo, yaliyofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar leo 30-4-2024
 

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema Zanzibar inajengwa na sera kuu ya Uchumi wa Buluu katika kuimarisha uchumi wa watu wake.

Amesema uchumi wa buluu una mawanda mapana na kujipambanua kwenye maeneo muhimu yakiwemo Utalii, Uvuvi na ufugaji wa vifaranga vya samaki, Bandari, Mafuta na gesi pamoja na Sekta ya usafirishaji wa majini.

Dk. Mwinyi aliyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipozungumza na Mkuu wa Chuo cha Ulinzi cha Taifa (NDC) Balozi, Meja Jenerali Wilbert Augustin Ibuge na ujumbe alioongozana nao wa wanafunzi 52 wa chuo hicho kutoka mataifa 15 ya Afrika ikiwemo Tanzania pamoja na watumishi wengine wa Serikali waliofika hapo kumtembelea.

Akizichambua kwa upana wake sekta za Uchumi wa Buluu, Rais Dk. Mwinyi aliueleza ugeni kuo kwamba Utalii wa Zanzibar nitegemeo kwa uchumi wa nchi, unaochangia asilimia 30 ya pato la taifa na unajumuisha utalii wa fukwe, Urithi, michezo na utalii mpya wa afya na mikutano.

Kuhusu sekta ya Uvuvi na ufugaji wa Samaki, Rais Dk. Mwinyi alimueleza Meja General Ibuge na ujumbe wake, kwamba Uchumi wa buluu pia una fursa nyingi kwa wavuvi na ajira za mtu mmoja mmoja wanaojihusisha na shughuli za maboti na majahazi, kilimo cha Mwani kilichobeba asilimia kubwa ya kina mama ambapo alieleza Zanzibar inaongoza kwa kuzalisha mwani mzuri Afrika.

Fursa nyengine za Uchumi wa buluu, Rais Dk. Mwinyi aliueleza ugeni huo kuwa Zanzibar inanufaika na Sekta ya Bandari zikiwemo Bandari jumuishi ya Mangapwani iliyokwenye matengenezo makubwa, bandari ya Malindi, Mkokotoni na bandari ya Fumba zinazoendeleza uchumi wa nchi ili kukidhi mahitaji ya uchumi wa watu kama vituo muhimu vya usafirishaji, usambazaji wa bidhaa kutoa huduma na kufanyia biashara ikiwemo kupokelea mizigo, kusafirishia mazao, na mahitaji mbalimbali kama mafuta, nafaka, na kukuza uchumi wa nchi.

Alisema, sekta hiyo pia inaimarisha biashara na uchumi kupitia bandari za Zanzibar, Pemba, Tanga, Dar es Salaam na Mtwara kusafirisha maeneo mengine ikiwemo Msumbiji, visiwa vya komoro na kwengineko.

Suala la mafuta na gesi pamoja na sekta ya usafirishaji wa majini, Rais Dk. Mwinyi alizungumzia ni muhimu pia kwa Uchumi wa Zanzibar.

Naye, Balozi, Meja Jenerali Ibuge, alimueleza Rais Dk. Mwinyi lengo la ziara yao hiyo waliyoipa kauli mbiu ya “Kuimarisha biashara na usalama kwa uchumi endelevu wa Uchumi wa Buluu Zanzibar” ni moja kati ya ziara zao za ndani ya nchi za kujivunia utamaduni wa Tanzania kwa wageni wanaosoma chuoni hapo.

Mataifa mengine yenye wanafunzi wanaosoma kwenye chuo cha Ulinzi cha Taifa (NDC) ni pamoja na Botswana, Burundi, Ethiopia, India, Kenya, Malawi, Misri, Namibia, Nigeria, Rwanda, Sera Leone, South Afrika, Uganda, Zambia na Zimbabwe. 

IDARA YA MAWASILIANO, IKULU ZANZIBAR

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.