RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi,
Mhe. Dk. Hussein Ali Mwinyi amesema Zanzibar inajengwa na sera kuu ya Uchumi wa
Buluu katika kuimarisha uchumi wa watu wake.
Amesema uchumi wa buluu una mawanda mapana na kujipambanua kwenye maeneo
muhimu yakiwemo Utalii, Uvuvi na ufugaji wa
vifaranga vya samaki, Bandari, Mafuta na gesi pamoja na Sekta ya usafirishaji
wa majini.
Dk. Mwinyi aliyasema hayo Ikulu, Zanzibar alipozungumza na Mkuu wa Chuo
cha Ulinzi cha Taifa (NDC) Balozi, Meja Jenerali Wilbert Augustin Ibuge na
ujumbe alioongozana nao wa wanafunzi 52 wa chuo hicho kutoka mataifa 15 ya
Afrika ikiwemo Tanzania pamoja na watumishi wengine wa Serikali waliofika hapo kumtembelea.
Akizichambua kwa upana wake sekta za Uchumi wa Buluu, Rais Dk. Mwinyi aliueleza
ugeni kuo kwamba Utalii wa Zanzibar nitegemeo kwa uchumi wa nchi, unaochangia
asilimia 30 ya pato la taifa na unajumuisha utalii wa fukwe, Urithi, michezo na
utalii mpya wa afya na mikutano.
Kuhusu sekta ya Uvuvi na ufugaji wa Samaki, Rais Dk. Mwinyi alimueleza
Meja General Ibuge na ujumbe wake, kwamba Uchumi wa buluu pia una fursa nyingi
kwa wavuvi na ajira za mtu mmoja mmoja wanaojihusisha na shughuli za maboti na
majahazi, kilimo cha Mwani kilichobeba asilimia kubwa ya kina mama ambapo
alieleza Zanzibar inaongoza kwa kuzalisha mwani mzuri Afrika.
Fursa nyengine za Uchumi wa buluu, Rais Dk. Mwinyi aliueleza ugeni huo kuwa
Zanzibar inanufaika na Sekta ya Bandari zikiwemo Bandari jumuishi ya Mangapwani
iliyokwenye matengenezo makubwa, bandari ya Malindi, Mkokotoni na bandari ya
Fumba zinazoendeleza uchumi wa nchi ili kukidhi mahitaji ya uchumi wa watu kama
vituo muhimu vya usafirishaji, usambazaji wa bidhaa kutoa huduma na kufanyia
biashara ikiwemo kupokelea mizigo, kusafirishia mazao, na mahitaji mbalimbali
kama mafuta, nafaka, na kukuza uchumi wa nchi.
Alisema, sekta hiyo pia inaimarisha biashara na uchumi kupitia bandari za
Zanzibar, Pemba, Tanga, Dar es Salaam na Mtwara kusafirisha maeneo mengine ikiwemo
Msumbiji, visiwa vya komoro na kwengineko.
Suala la mafuta na gesi pamoja na sekta ya usafirishaji wa majini, Rais
Dk. Mwinyi alizungumzia ni muhimu pia kwa Uchumi wa Zanzibar.
Naye, Balozi, Meja Jenerali Ibuge, alimueleza Rais Dk. Mwinyi lengo la ziara
yao hiyo waliyoipa kauli mbiu ya “Kuimarisha biashara na usalama kwa uchumi endelevu
wa Uchumi wa Buluu Zanzibar” ni moja kati ya ziara zao za ndani ya nchi za
kujivunia utamaduni wa Tanzania kwa wageni wanaosoma chuoni hapo.
Mataifa mengine yenye wanafunzi wanaosoma kwenye chuo cha Ulinzi cha Taifa
(NDC) ni pamoja na Botswana, Burundi, Ethiopia, India, Kenya, Malawi, Misri,
Namibia, Nigeria, Rwanda, Sera Leone, South Afrika, Uganda, Zambia na
Zimbabwe.
IDARA YA MAWASILIANO, IKULU ZANZIBAR
No comments:
Post a Comment