Habari za Punde

Mikoa ya Ruvuma, Njombe, Songwe na Rukwa kuboresha daftari la wapiga kura Januari, 2025.

 

Mwandishi Wetu.


Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi imetangaza ratiba ya 

uboreshaji wa Daftari la Kudumu la Wapiga Kura kwenye 

mikoa ya Ruvuma, Njombe, Songwe na Rukwa ambapo zoezi 

hilo litafanyika kwa siku saba kuanzia tarehe 12 hadi 18 

Januari, 2025.


Hayo yameanishwa kwenye hotuba ya Mwenyekiti wa Tume 

Huru ya Taifa ya Uchaguzi, Jaji wa Mahakama ya Rufaa, Mhe. 

Jacobs Mwambegele iliyosomwa kwa niaba yake kwenye 

mikutano  ya Tume na  wadau wa uchaguzi iliyofanyika leo 

tarehe 31 Desemba, 2024 kwenye  mikoa ya Ruvuma, Njombe, 

Songwe na Rukwa.


Mhe. Mwambegele ambaye aliwakilishwa na wakurugenzi 

mbalimbali wa Tume kwenye mikutano hiyo,  amesema mikoa 

hiyo itafanya uboreshaji kwenye mzunguko wa tisa na 

kwamba tayari Tume imekamilisha uboreshaji kwenye mikoa 

19 ambayo ilijumuisha mizunguko nane kati ya mizunguko 13 

ambayo imepangwa kukabilisha zoezi hilo nchini.


“Leo tupo hapa Songwe na wenzetu wapo kwenye mikoa ya 

Njombe, Rukwa na Ruvuma ikiwa ni maandalizi ya uboreshaji 

wa Daftari kwenye mkoa huu wa Songwe, Njombe, Rukwa na 

mkoani Ruvuma kwenye Halmashauri za Wilaya ya Nyasa, 

Mbinga, Mbinga Mji, Wilaya ya Songea na Manispaa ya 

Songea, zoezi litakalofanyika kwa muda wa siku saba kuanzia 

tarehe 12 Januari, 2025 na kukamilika tarehe 18 Januari, 

2025 na ambapo vituo vitakuwa vinafunguliwa kuanzia saa 

2:00 asubuhi na kufungwa saa 12:00 jioni,” imesema sehemu 

ya hotuba hiyo.


Ameitaja mikoa ambayo tayari imekamisha zoezi hilo kuwa ni 

Kigoma, Tabora, Katavi, Geita, Kagera, Mwanza, Shinyanga, 

Mara, Simiyu, Manyara, Dodoma na Singida.


“Mikoa mingine ni mikoa ya Zanzibar ambayo ni Mjini 

Magharibi, Kusini Unguja, Kaskazini Unguja, Kusini Pemba, 

Kaskazini Pemba, Arusha na Kilimanjaro. Kwa sasa mikoa 

miwili ya Mbeya na Iringa inatarajia kukamilisha zoezi hilo 

tarehe 02 Januari, 2025,” imesema sehemu ya hotuba hiyo.


Mada ya Mkurugenzi wa Uchaguzi, Bw. Kailima Ramadhani 

iliyowasilishwa kwa niaba yake kwenye mikutano hiyo 

imeanisha kwamba kwenye mikoa hiyo jumla ya wapiga kura 

wapya 475,743 wanatarajiwa kuandikishwa kwenye Daftari la 

Kudumu la Wapiga Kura.


Mada hiyo imeanisha kuwa uboreshaji wa Daftari 

utakapokamilika, mikoa hiyo inatarajiwa kuwa na  jumla ya 

wapiga kura  3,091,485 ikilinganishwa na idadi ya wapiga 

kura 2,615,742 waliokuwemo kwenye Daftari mwaka 2020.


Idadi hii inaweza kuongezeka kwa kuwa inawezekana wapo 

watanzania ambao walikuwa na sifa za kuandikishwa kuwa 

wapiga kura wakati wa uboreshaji wa Daftari mwaka 2019/20, 

lakini kwa sababu moja au nyingine hawakuweza 

kujiandikisha,” imesema sehemu ya mada hiyo.


Mada hiyo imeanishwa kuwa kutakuwa na vituo 3,785 ikiwa 

ni ongezeko la vituo 233 kutoka vituo 3,552 vilivyokuwepo 

mwaka 2020.


Mwisho.

 

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.