Menu

Wednesday, August 20, 2025

Juhudi Zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi Zanzibar Kuimarisha Haki za Jamii ya Watu Wenye Ulemavu

Na.Mwandishi OMKR Zanzibar 

Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Othman Masoud Othman amesema licha ya juhudi zinazochukuliwa na serikali ya Mapinduzi Zanzibar kuimarisha haki za jamii ya watu wenye ulemavu, bado yapo mahitaji mengi na kupitia maradi CADiR  nchi itaongeza uwezo wa kulifikia vyema kundi hilo ili kuimarisha upatikanaji huduma, haki na fursa za kimaendeleo kwa watu hao.

Hayo ameyasema  huko hoteli ya Madinat Al Bahar Mbweni Mjini Zanzibar alipozungunza katika ufunguzi rasmi wa mradi wa miaka mitano wa kukuza na kuimarisha utoaji wa haki za watu wenye Ulemavu (CADiR), unaozishirikisha taasisi za serikali, asasi za kiraia na Binafasi nchini.

Hvyo, mhe. Othman ametoa wito kwa jamii nchini  kwamba ni vyema kila mmoja kulichukulia  suala la haki  na fursa za watu wenye ulemavu  ni jambo la wajibu, sio tu kwa serikali, lakini kwa watu wote  na linakuwa sehemu ya utamaduni wa wananchi na linalohitaji mashirikiano kutoka kila mtu  na kujenga jamii bora yenye ustawi.

Mhe. Othman amefahamisha kwamba kwa kutambua umuhimu wa mradi huo ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar itaendelea kutoa mashirikiano ya kutosha katika kuhakikisha unafanikiwa  kama ilivyopangwa  na kufikia leo la jamii jumuishi.

Kuhusu suala la watu wenye ulemavu kutumika kuwa omba omba Mhe. Othman amesema kwamba sharia kuhusu suala hilo inasema wazi kwamba ni kosa la jinai kuwatumia watu wa aina hiyo na kwamba kwa kuwa suala hilo lipo sana Mkoa wa mjini Magharib serikali za wilaya na mkoa wanayo mamlaka ndani ya wiki moja kuliondosha jambo hilo.

Amesema kwamba ni muhimu kwa viongozi katika jambo hilo ambalo linawadhalilisha watu wenye ulemavu kutolitia siasa na badala yake sharia ichukue nafasi yake katika kuikabili na kulimaliza ndani ya kipindi kifupi bila kuangaliwa watu machoni.

Kwa upande wake Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar Mhe. Harous Said Suleimani akimkaribisha Mhe. Makamu amemshukuru kwa jitihada zake za kufanya kazi kwa kuwashirikisha jambo0 ambalo limesaidia kupatikana ufanisi kwenye masuala mbali mbali kiutendaj.

Naye Mwenyekiti wa Shirikisho la Watu wenye Ulemavu Zanzibar (SHIJUWAZA) Mwandawa Khamis Mohammed, amesema  kwamba jumuiya hiyo itajitahidi katika kuhakikisha kwamba inatoa ushirikiano wa kutosha ili  kufanikisha utekelezaji wa mradi huo wa kuimarisha haki kwa watu wa jamii hiyo na malengo yaweze kufikiwa.

Ametoa wito kwa Watu wenye ulemavu kuwa tayari katika kuzichangamkia fursa mbali mbali zinazotolewa kupitia mradi huo na kuhakikisha kwamba hakuna mtu yeyote katika jumuiya hiyo anayeachwa nyuma kwenye manufaa ya mradi huo.

Naye Mwenyekiti wa Shirikisho la watu wenye ulemavu kutoka Tanzania Bara Tungi Mwanjala, amesema kwamba  uzinduzi wa mradi huo ni tukio walilolisubiri kwa muda mrefu na kwamba mjumuiko huo unatoa matumaini katika kuhakikisha kwamba mradi huo unatekelezwa katika kufikia maisha mazuri kwa watu wenye ulemavu.

Naye Mkurugenzi Mkaazi wa Mradi huo hapa Zanzibar ndugu Abdalla Omar, amesema kwamba Progaram hiyo imefadhiliwa na serikali ya Norway kupitia shirika lao la Maendeleo la NORAD na kuzishirikisha Taasisi tano kutoka nchini humo zinazoshughulikia maendeleo ya watu wenye ulemavu.

Naye Katibu Mtendaji wa Baraza la Watu wenye Ulemavu Zanzibar Mhandisi Ussi Khamis Debe akiwatambulisha wageni kwenye uzinduzi huo, amesema kwamba mradi huo utasaidia kujenga misingi imara zaidi ili kuondosha vikwazo kwa jamii hiyo  na kuweza kufikia dira ya kujenga jamii jumuishi katika shughuli zote za maendeleo nchini.

Mradi huo muhimu kwa  Maendeleo ya Watu wenye  Ulimavu unalenga  katika utoaji wa elimu mjumuisho , uwezeshaji kiuchumi, afya na marekebisho,na pia uhamasishaji na utetezi wa haki za watu wenye ulemavu ambao unatekelezwa kwa Tanzania Bara na Zanzibar unathamani ya zaidi ya shilingi 20 bilioni  za Tanzania.

Mwisho

Imetolewa na Ofisi ya Makamu wa Kwanza wa Rais wa Zanzibar kupitia Kitengo chake cha habari leo Jumatano tarehe 20 Agosti 2025.

No comments:

Post a Comment