6/recent/ticker-posts

MCT yakiri baadhi ya vyombo vya habari vinachochea ghasia


Na Husna Mohammed
BARAZA la Habari Tanzania (MCT) ofisi ya Zanzibar, limesema licha ya kuwepo baadhi ya vyombo vya habari vinavyokwenda kinyume na maadili na kuchochea ghasia lakini tasnia ya habari Zanzibar imekua.

Meneja wa baraza hilo ofisi za Zanzibar, Suleiman Seif Omar, aliuambia ujumbe wa maofisa wa balozi wa baadhi ya nchi za Ulaya waliotembelea ofisi za baraza hilo Mlandege mjini hapa.

Maofisa hao walitaka kujua wajibu wa vyombo vya habari Zanzibar hasa katika kutekeleza wajibu wao wa kutoa taarifa kwa umma.

Meneja huyo, alisema vipo baadhi ya vyombo vya habari hasa vinavyofanyia kazi Tanzania Bara vimekuwa vikipotosha wananchi hasa kwa habari zinazohusiana na uchochezi na vurugu ambazo wamekuwa wakizipa nafasi kubwa kinyume na hali inavyokuwa pamoja na kuzitia chumvi.


“Tumekuwa mstari wa mbele kuelimisha vyombo vya habari kupitia baraza la habari Tanzania ili kutekeleza majukumu yao bila ya kukiuka maadili ila ni vyombo vichache vinavyofanya hivyo jambo ambalo wakati mwengine linachangiwa na wahariri,” alisema.

Aidha Meneja huyo alisema vyombo vya habari Zanzibar, vimekuwa vikisaidia kuelimisha jamii juu ya umuhimu wa kulinda amani na utulivu.

Sambamba na hilo,aliuambia ujumbe huo kuwa Baraza la Habari Tanzania limekuwa na msimamo wa pamoja juu ya kuingizwa vyombo vya habari katika katiba mpya kuwa ni muhimili wa nne kutokana na umuhimu wake katika nchi.

Nae Jussi Nummelin, ofisa Ubalozi wa Finland, alilitaka baraza la Habari kuendelea kutekeleza wajibu wake wa kuelimisha wananchi juu ya kulinda amani na utulivu.

Aidha alisema vyombo vya habari vinapaswa kusimamiwa na MCT kwa kuhakikisha havivunji maadili ya habari sambamba na kuhimiza amani ya nchi na wananchi kwa ujumla.

Ujumbe huo wa mabalozi unatoka nchi za Norway, Finland, Uholanzi na Jumuiya ya nchi za Ulaya.




Post a Comment

0 Comments