Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akisalimiana na Balozi wa Comoro Nchini Tanzania Dk.Ahamada El Badaoui Mohamed alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo kwa mazungumzo na Rais
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akizungumza na Balozi wa Comoro Nchini Tanzania Dk.Ahamada El Badaoui Mohamed alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein akifuatana na Balozi wa Comoro Nchini Tanzania Dk.Ahamada El Badaoui Mohamed baada ya mazungumzo yao leo alipofika Ikulu Mjini Zanzibar
STATE HOUSE ZANZIBAR
OFFICE OF THE PRESS SECRETARY
PRESS RELEASE
Zanzibar
7.1.2015
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisistiza kuwa Zanzibar itaendeleza uhusiano
na ushirikiano wa kihistoria uliopo kati yake na Comoro hasa katika uimarishaji
wa sekta za maendeleo na utamaduni.
Dk. Shein aliyasema
hayo wakati alipofanya mazungumzo na Balozi wa Comoro nchini Tanzania Dk.
Ahmada El Badaoui Mohamed, Ikulu mjini Zanzibar.
Katika mazungumzo
hayo Dk. Shein alisema kuwa Zanzibar inajivunia uhusiano na ushirikiano huo wa
muda mrefu sambamba na maingiliano na uhusiano wa watu wake kati ya nchi mbili
hizo ambao wameweza kuimarisha udugu wao wa kihistoria.
Kutokana na hatua
hiyo, Dk. Shein alisema kuwa mashirikiano katika uimarishaji wa sekta za
maendeleo sambamba na utekelezaji wa Mkataba wa Makubaliano uliotiwa saini hapo
mwaka jana wakati wa ziara yake aliyoifanya
nchini humo utasaidia kuimarisha juhudi hizo.
Dk. Shein alisema
kuwa utekelezaji wa makubaliano hayo utasaidia kwa kiasi kikubwa kuimarisha
ushirikiano kati ya Zanzibar na Comoro ambao umeweza kukuza udugu miongoni mwa
watu wake.
Mbali ya uhusiano
huo wa kimaendeleo kati ya Zanzibar na Comoro, Dk. Shein alisema kuwa nchi
mbili hizo zimekuwa na uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu katika kukuza mila
na tamaduni zake sambamba na mafunzo
hasa katika elimu ya dini ya Kiislamu.
Alisisitiza kuwa
mashirikiano katika sekta ya elimu, habari,biashara, usafiri na usafirishaji pamoja na sekta nyenginezo utazidi kuimarisha
uhusiano wa Comoro na Zanzibar ambao ni wa muda mrefu.
Sambamba na hayo,
Dk. Shein alimueleza Balozi huyo wa Comoro juhudi zinazochukuliwa na Serikali
ya Mapinduzi Zanzibar katika kupambana na kupiga vita uingizaji na matumizi ya
dawa za kulevya hapa nchini kwa kutambua changamoto zilizopo kwa nchi za
visiwa.
Nae Balozi wa
Comoro nchini Tanzania Dk. Ahmada El Badaoui Mohamed alisema kuwa Comoro
inathamini sana uhusiano na ushirikiano wa muda mrefu kati yake na Zanzibar
ambao nchi yake umeahidi kuudumisha kwa manufaa ya pande zote mbili.
Balozi huyo
alisema kuwa Comoro na Zanzibar ina historia kubwa katika kutoa elimu hasa ya
dini ya Kiislamu na kueleza kuwa mashekhe wengi wakubwa wa Comoro elimu yao
hiyo wameipata hapa Zanzibar akiwemo baba yake mzazi.
Alisema kuwa
Comoro inajivuinia kwa hilo na kusisitiza kuwa ipo haja kwa viongozi wa dini wa
nchi mbili hizi kuzidisha mashirikiano na kukuza uhusiano ikiwa ni pamoja na
kutembeleana na kubadilishana uzoefu katika elimu ya dini ya Kiislamu.
Aidha, Dk. Ahmada
alisema kuwa utekelezaji wa mkataba wa makubaliano uliosainiwa katika ziara ya
Dk. Shein aliyoifanya nchini humo mwaka jana utasaidia kwa kiasi kikubwa
kufikia malengo yaliokusudiwa katika uimarishaji wa sekta za maendeleo na
ukuzaji wa uchumi kwa pande zote mbili.
Pamoja na hayo,
Balozi huyo alieleza faraja atakayoipata yeye binafsi pamoja na nchi yake katika
utekelezaji wa moja ya makubaliano hayo ambayo ni kuimarisha lugha ya kiswahili
nchini humo kutokana na mashirikiano na taasisi husika ya hapa Zanzibar.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail:
rajabmkasaba@yahoo.co.uk




0 Comments