TAARIFA KWA VYOMBO VYA HABARI
Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania imeendelea kuimarisha ushirikiano wa kimkakati na Umoja wa Ulaya kufuatia mafanikio ya ziara ya mashauriano ya ngazi ya juu yaliyofanyika jijini Brussels, Ubelgiji. Ziara hiyo iliongozwa na Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, Mheshimiwa Balozi Mahmoud Thabit Kombo.
Katika ziara hiyo, Mheshimiwa Waziri Kombo alizungumza na viongozi wakuu wa Umoja wa Ulaya, wakiwemo Makamu wa Rais wa Tume ya Umoja wa Ulaya na Mwakilishi Mkuu wa Umoja wa Ulaya wa Sera ya Mambo ya Nje na Usalama Mheshimiwa Kaja Kallas; Kamati ya Kisiasa na Usalama ambayo ni jukwaa kuu la ngazi ya mabalozi la Umoja wa Ulaya kwa ajili ya uratibu wa sera za mambo ya nje, usalama na ulinzi; Makamu wa Rais wa Bunge la Ulaya Mheshimiwa Younous Omarjee; na Kamishna wa Umoja wa Ulaya anayeshughulikia Ushirikiano wa Kimataifa Mheshimiwa Jozef SÃkela.
Ushirikiano huu unaakisi mwelekeo wa diplomasia ya Tanzania yenye kujiamini, inayozingatia maendeleo, maslahi ya taifa, ushirikiano unaolenga matokeo, na ushirikiano wa kimataifa unaotekelezeka.
Akiambatana na Waziri wa Nchi Ofisi ya Rais Kazi Maalum, Mheshimiwa Profesa Palamagamba Kabudi, Waziri Kombo alifanya mashauriano ya kina na Mheshimiwa Kaja Kallas yaliyolenga kuimarisha ushirikiano wa vitendo kati ya Tanzania na Umoja wa Ulaya, hususan katika maeneo ya amani na usalama wa kikanda, biashara inayozingatia utawala wa sheria, uwezeshaji wa uwekezaji, pamoja na mifumo thabiti na inayotabirika ya ushirikiano inayosaidia utekelezaji na ufanisi wa miradi.
Ziara hiyo ilijumuisha mashauriano na Kamati ya Kisiasa na Usalama (PSC) katika makao makuu ya taasisi kuu za Umoja wa Ulaya. Kamati hiyo, inayoundwa na Mabalozi wa Nchi Wanachama 27 wa Umoja wa Ulaya na kuongozwa na Balozi wa Urais unaohudumu wa Baraza la Umoja wa Ulaya, ndiyo chombo kikuu cha ngazi ya mabalozi kinachounda na kuongoza sera za mambo ya nje, usalama na ulinzi wa Umoja huo.
Katika kikao hicho, Mheshimiwa Waziri Kombo alizungumza na kila mjumbe, na kusisitiza umuhimu mkubwa ambao Tanzania inaipa taasisi hiyo muhimu ya kimkakati. Waziri Kombo alipata fursa ya kuwasilisha mitazamo ya Tanzania ndani ya mifumo ya Umoja wa Ulaya ya uundaji wa maamuzi na kuthibitisha tena nafasi ya Tanzania kama mshirika wa kuaminika na mwenye mchango chanya katika masuala ya amani, usalama na utulivu wa kikanda katika Afrika Mashariki.
Katika ngazi ya kibunge, Mheshimiwa Waziri Kombo alifanya mazungumzo katika Bunge la Ulaya, ikiwemo mikutano na Makamu wa Rais wa Bunge hilo, Mheshimiwa Younous Omarjee.
Mikutano hiyo iliimarisha diplomasia ya kibunge kama nguzo muhimu ya uhusiano kati ya Tanzania na Umoja wa Ulaya, na kusaidia ushirikiano wa muda mrefu katika masuala ya biashara, utawala bora na mahusiano kati ya watu na watu.
Masuala ya ushirikiano wa maendeleo na uhamasishaji wa uwekezaji yalikuwa miongoni mwa ajenda kuu katika mazungumzo na Kamishna Jozef SÃkela, ambaye jukumu lake ni kujenga ushirikiano wa kimataifa ulio endelevu na wenye manufaa ya pande zote.
Tanzania ilisisitiza kipaumbele chake cha ushirikiano wenye miradi inayotekelezeka na yenye athari kubwa, unaosaidia ajira, maendeleo ya ujuzi, uongezaji thamani na miundombinu imara, sambamba na Ajenda ya Taifa ya Mabadiliko ya Kiuchumi na Kijamii.
Mwelekeo wa Sera ya Mambo ya Nje ya Tanzania Mashauriano ya Brussels yanaendana kikamilifu na maono ya sera ya mambo ya nje yaliyobainishwa na Mheshimiwa Dkt Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, katika hotuba yake ya Mwaka Mpya kwa mabalozi, iliyofungua ukurasa mpya wa diplomasia ya Tanzania. Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan alisisitiza msimamo unaojengwa juu ya uhalisia, heshima kwa mamlaka ya taifa, na mawasiliano endelevu na washirika wote.
Mwelekeo huu unathibitisha dhamira ya Tanzania katika kuimarisha mfumo wa ushirikiano wa kimataifa na kufanya kazi kwa karibu na wadau wote kwa ajili ya ustawi wa pamoja, amani na maendeleo endelevu.
Kiini cha sera hii ni ujumbe thabiti wa heshima ya pande zote na ushirikiano unaojengwa juu ya usawa na manufaa ya pamoja. Tanzania inaendelea kutekeleza mifumo ya ushirikiano wa kunufaishana ambayo inakuza vipaumbele vya maendeleo ya taifa huku ikitoa thamani kwa washirika wa kimataifa.
Mashauriano haya pia yanaendana na vipaumbele vya ushirikiano vya Umoja wa Ulaya na Tanzania vinavyojikita katika maendeleo ya kijani, maendeleo ya rasilimali watu na ajira, pamoja na utawala bora, hivyo kuimarisha mkondo wa programu zilizoandaliwa, msaada wa utekelezaji na uhamasishaji wa uwekezaji.
Kama sehemu ya mawasiliano ya kimkakati na diplomasia ya umma, Mheshimiwa Waziri Kombo alifanya mahojiano na jarida la Diplomatic World katika Ubalozi wa Tanzania mjini Brussels, akieleza madhumuni na matokeo ya ziara hiyo ya ngazi ya juu “katika moyo wa Ulaya
Waziri Kombo alisisitiza kuwa ziara hiyo ya Tanzania jijini Brussels ni uwekezaji wa makusudi katika kujenga uhusiano ndani ya taasisi za Umoja wa Ulaya, unaolenga kuimarisha imani, kupanua fursa za ushirikiano, na kuijengea Tanzania taswira ya taifa thabiti, linaloaminika na lenye fursa nyingi za biashara, uwekezaji na ushirikiano wa maendeleo.
Ushirikiano na Umoja wa Ulaya unaendelea kuwa wa umuhimu mkubwa hususan katika kipindi baada ya Uchaguzi Mkuu wa Tanzania uliofanyika Oktoba 29, 2025. Umoja wa Ulaya ni mshirika muhimu wa maendeleo, biashara na kisiasa kwa Tanzania, na mdau muhimu katika mifumo ya ushirikiano wa kimataifa.
Kwa muktadha huo, Tanzania imeendelea na itaendelea kushirikiana kwa uwazi na kwa mtazamo chanya na Umoja wa Ulaya wakati ikitekeleza taratibu za ndani za kitaasisi, ikiwemo kazi ya Tume Huru ya Uchunguzi iliyoundwa kubaini chanzo cha matukio ya vurugu baada ya uchaguzi mkuu wa Oktoba 2025. Hatua hizi zinaonesha dhamira ya Serikali katika uwajibikaji, uwazi na uimarishaji wa taasisi kwa kuzingatia Katiba na sheria za nchi.
Mazungumzo endelevu na Umoja wa Ulaya yanahakikisha kuwa michakato hii ya kitaifa inaeleweka vyema huku yakilinda mwendelezo wa ushirikiano wa maendeleo, mtiririko wa uwekezaji na imani ya kiuchumi. Katika mazungumzo yake, Mheshimiwa Waziri Kombo alieleza kuwa Brussels ni muhimu kwa Tanzania kwa kuwa ni kitovu cha uratibu wa sera za Umoja wa Ulaya, maamuzi ya kifedha na ushirikiano wa kimataifa. Ushirikiano wa kudumu wa Tanzania katika ngazi ya taasisi mjini Brussels ni uwekezaji wa kimkakati katika diplomasia ya uchumi, upanuzi wa biashara na uhamasishaji wa uwekezaji, sambamba na kuhakikisha kuwa mitazamo ya Tanzania kuhusu amani na usalama wa kikanda inawasilishwa ipasavyo.
Ujumbe wa Tanzania uliofuatana na Mheshimiwa Waziri Kombo ulijumuisha Mheshimiwa Profesa Palamagamba Kabudi, Balozi Swahiba Mndeme (Mkurugenzi wa Idara ya Ulaya), Balozi Jestas Abuok Nyamanga (Mwakilishi wa Kudumu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania katika Umoja wa Ulaya), pamoja na maafisa wengine waandamizi.
Ujumbe huu wa ngazi ya juu unaoongozwa na Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki unathibitisha kwa mara nyingine kuwa Tanzania si mpokeaji tu wa ushirikiano wa kimataifa, bali ni mshirika hai na mwenye kujiamini—anayechagiza mahusiano yake ya kimataifa, kuhakikisha matokeo ya vitendo, na kuendeleza ushirikiano unaotoa manufaa ya moja kwa moja kwa wananchi wa Tanzania.
Imetolewa na:
Kitengo cha Mawasiliano ya Serikali
0 Comments