Habari za Punde

Dk. Shein ateta na mabalozi wa UAE, Msumbiji



Rajab Mkasaba, Ikulu
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amekutana na Balozi wa Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) nchini Tanzania,Mallallah Mubarak Alameri na kueleza kuwa Zanzibar inathamini sana uhusiano na ushirikiano wa kihistoria kati yake na Umoja huo.

Katika mazungumzo hayo yaliyofanyika Ikulu mjini Zanzibar, Dk. Shein alisema Zanzibar na UAE zimekuwa na mahusiano na mashirikiano ya muda mrefu ambayo yameweza kuimarika siku hadi siku katika nyanja mbali mbali za maendeleo.
Dk. Shein, alimueleza Balozi huyo ambaye alifika Ikulu kwa ajili ya kuaga, kuwa kutokana na uhusiano na mashirikiano hayo kukua ipo haja ya kukuza mashirikiano katika sekta za maendeleo na hatimae kupata mafanikio kwa pande zote mbili. 


Dk. Shein alisema juhudi za makusudi zimekuwa zikichukuliwa na serikali katika kuimarisha sekta za maendeleo ikiwemo sekta ya uwekezaji ambapo nchi za umoja huo zimeweza  kuonesha mwelekeo mkubwa wa kuwekeza katika sekta ya utalii.


Kwa upande wa sekta ya afya, Dk. Shein alieleza hatua kadhaa zinazochukuliwa na nchi za Umoja huo katika kuiunga mkono Zanzibar kuimarisha sekta ya afya, juhudi ambazo zimeweza kusaidia kwa kiasi kikubwa sekta hiyo.

Akieleza kuhusu sekta ya biashara, Dk. Shein alieleza pamekuwa na uhusiano mwema kati ya Zanzibar na UAE katika kuendeleza sekta hiyo ambayo ni muhimu katika kuimarisha uchumi ambpo pia, aliushukuru mfuko wa Abudhabi kwa kusaidia upatikanaji wa maji safi na salama katika baadhi ya maeneo nchini.

Alitoa pongezi za pekee kwa viongozi wa Umoja huo kwa juhudi zao za kuendelea kuiunga mkono Zanzibar na kuzidisha uhusiano na ushirikiano uliopo zikiwemo baadhi ya nchi za umoja huo ambazo alifanya ziara hapo Novemba mwaka 2011.

Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwepo kwa Kamati ya Pamoja ya Ushirikiano kati ya Zanzibar na Ras-Al-Khaiman kwa ajili ya kuendeleza mashirikiano katika nyanja hizo pamoja na miradi na shughuli mbali mbali zilizokubalika kutokana na utiaji saini waraka wa makubaliano kati ya pande mbili hizo. 

Nae Balozi Mallallah, alitoa shukurani kwa viongozi na wananchi wa Zanzibar kwa mashirikiano makubwa waliyompa wakati akiwa nchini.

Alisema wananchi wa UAE na wale wa Zanzibar ni ndugu na wana uhusiano wa muda mrefu na mashirikiano katika nyanja mbali mbali za kimaendeleo ambazo aliahidi kuendelea kuimarishwa na umoja huo kwa manufaa ya wote.

Pamoja na hayo, Balozi Mallallah alimuahidi Dk. Shein kuwa umoja huo utaendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha sekta zake za maendeleo huku akisisitiza kuwa sekta ya uwekezaji hasa katika sekta ya utalii litapewa kipaumbele na Umoja huo. 

Alisema UAE inathamini uhusiano na ushirikiano uliopo na kueleza kuwa miradi mbali mbali ambayo iliahidiwa kuanza ukiwemo kuanza safari kwa ndege za Shrika la Emirate, suala hilo  linafanyiwa kazi.

Wakati huo huo, Dk. Shein alifanya mazungumzo na Balozi wa Msumbuji nchini Tanzania,Dk. Vicente Mebunia Veloso na kumueleza haja kwa nchi mbili hizo kuimarisha mashirikiano katika sekta ya kilimo, biashara, usafiri na usafirishaji.

Katika maelezo yake, Dk. Shein alimueleza Balozi Veloso kuwa ipo haja kwa Zanzibar na Msumbiji zikaimarisha uhusiano na ushirikiano katika kuendeleza sekta ya kilimo kwani ni kata muhimu katika maendeleo ya nchini.

Kwa upande wa biashara, Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa umefika wakati kwa wafanyabiasahara wa Msumbiji kushirikiana na wafanyabiashara wa Zanzibar katika kuimarisha sekta ya biashara kwa pande zote mbili.

Alisisitiza haja ya kuwepo kwa mashirikiano katika usafiri wa angani na kueleza haja kwa Shirika la ndege la nchi hiyo kufanya safari zake moja kwa moja Zanzibar hatua ambayo itaimarisha sekta utalii.
 Kuhusu  usafiri wa majini, Dk. Shein alieleza umuhimu wa kuwepo mashirikiano katika sekta hiyo hali ambayo itasaidia kusafirisha bidhaa mbali mbali pamoja na wananchi katika nchi mbili hizo hatua ambayo inahitaji zaidi kuwepo kwa meli kubwa za usafiri.
Nae Balozi huyo mpya wa Msumbiji  alimueleza Dk. Shein kuwa nchi yake inathamini uhusiano na mashirikiano ya muda mrefu yaliopo kati ya nchi mbili hizo ikiwa ni pamoja na kutambua juhudi za ukombozi zilizochukuliwa na Tanzania.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.