Habari za Punde

Wadai tatizo starehe, mfumo kidato cha pili. Wizara yasema bado haijakaa kujadili


Na Asya Hassan
WAKATI Waziri Mkuu wa Tanzania, Mizengo Pinda akiunda Tume kuchunguza sababu ya wanafunzi kufeli katika mitihadi ya kidato cha nne, kwa upande wa Zanzibar wadau wa elimu wametoa maoni tafauti kuhusu matokeo hayo.

Wakizungumza na mwandishi wa habari hizi, walidai hao walitaja sababu nyingi zilizochangia wanafunzi kufeli, ikiwemo wanafunzi kujihusisha na mahusiano ya kimapenzi, starehe, wazazi kushindwa kufuatilia maendeleo ya watoto wao na walimu kutokuwajibika ipasavyo kutokana na madai ya kiwango kidogo cha mishahara wanacholipwa, mbali ya Serikali kuwaongezea mishahara kwa kiwango kikubwa karibu miaka miwili sasa.


Walisema mahusiano ya kimapenzi yameliathiri kundi kubwa la wanafunzi hasa wanaosoma katika skuli za mijini.

Walisema hali hiyo imewafanya wanafunzi kuchanganya mapenzi na masomo kwa wakati mmoja.

Aidha walisema kushushwa kiwango cha ufaulu katika mitihani ya kidato cha pili kunasababisha wanafunzi wengi kufaulu kidato cha tatu, ingawa hawana uwezo wa kufaulu hali inayowafanya pia kukosa uwezo wa kufanya mitihani ya kidato cha nne.

Naibu Katibu Mkuu wa Chama cha Walimu Zanzibar (ZATU) Salim Ali Salim, alisema mitihani ya kidato cha nne inafanywa wakati wanafunzi wakiwa hawajawa tayari kufanya mitihani hiyo.


Lakini pia alisema wana uwezo mdogo sana wa kuukabili mtihani huo kwa sababu wizara ya elimu haina kiwango maalum cha ufaulu kwa wanafunzi wa kidato cha pili.

Kwa mfano alisema, wizara imekuwa ikiwachukua wanafunzi ambao wamefaulu kwa kiwango cha chini sana cha asilimia 29 kujiunga na kidato cha tatu, kiwango ambacho hakiwezi kumuwezesha mwanafunzi huyo kufaulu katika mitihani ya kidato cha nne.

Alisema ili kuweza kuziba mapango ya kufeli kwa wanafunzi hao ni vyema kwa serikali kuongeza bajeti ili wizara ya elimu iweze kufanya utafiti wa kutosha juu ya elimu na kuweza kujua kwa kina sababu halisi inayopelekea wanafunzi hao kufeli.

Aidha alisema pia inawezekana walimu walichangia wanafunzi hao kufeli, lakini alidai sababu kubwa ni mishahara midogo wanayolipwa walimu hao.

Nae Msaidizi wa Mwalimu mkuu wa skuli ya Mwembeladu, Salma Nassor ambae wanafunzi 565 wa skuli yake wamepata daraja sifuri, alisema matokeo hayo mabaya yamesababishwa na wanafunzi kushindwa kuwasikiliza walimu wao wawapo madarasani na badala yake kukimbilia kutafuta masomo ya ziada (tuition) ambazo walimu wake hawafahamu mbinu za kujibia masuali ya mitihani ya kitaifa.

Nae mwalimu wa skuli hiyo Ali Idd Hamad alisema, walimu wamekuwa wakifuata mtaala, lakini uwezo wa wanafunzi ni mdogo mno na kama mabadiliko hayatafanywa hawezi kufaulu.

Aidha alisema walimu wamekuwa na mzigo mkubwa wa vipindi na idadi kubwa ya wanafunzi ndani ya darasa moja.

Katibu Mkuu wa Wizara ya Elimu na Mafunzo ya Amali, Mwanaidi Saleh, alipotakiwa kueleza kuhusu matokeo hayo alisema, wizara bado haijakaa kujadili suala hilo.

Miaka miwili iliyopita Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iliongeza mishahara ya walimu kwa asilimia kubwa ili kuwafanya walimu kubakia nchini na kuondokana na mtindo wa kukimbia kufanya kazi nje kufuata malipo makubwa.


No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.