Habari za Punde

Maandalizi ya maonyesho ya miaka 50 ya mapinduzi yakamilika

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi akiangalia matayarisho ya mwisho ya maonyesho ya Miaka 50 ya Mapinduzi ya Zanzibar hapo uwanja wa Kampasi ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar {SUZA} uliopo  Beit El Ras nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ambae pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maadhimisho ya Kitaifa  Balozi Seif akiongozwa  na Mkurugenzi wa Idara ya Mipango, Sera na Utafiti Wizara ya Nchi Ofisi ya Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Ahmada Hamad kukagua matayarisho ya mwisho ya maonyesho ya miaka 50 hapo Beit El Ras.

 Balozi Seif akiwa pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo na Mali Asili Zanzibar Nd. Afan Othman Maalim wakifurahia kazi kubwa iliyofikia hatua za mafanikio ya Wizara ya Kilimi katika mabanda ya maonyesho hapo Beit el Ras.
Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif akiwa pamoja na Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo na Mali Asili Zanzibar Nd. Afan Othman Maalim wakibadilishana mawazo mara baada ya kungalia matayarisho ya banda la maonyesho la Wizara ya Kilimo.

Picha na Hassan Issa wa  - OMPR – ZNZ.

Na Othman Khamis Ame OMPR

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dr. Ali Mohd Sheni Jioni ya Januari Pili mwaka 2014  anatarajiwa kuyafungua rasmi  maonyesho  ya miaka 50  ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Maonyesho hayo ya siku Nne yanayoshirikisha zaidi ya Taasisi  122 za Serikali pamoja na Zile Binafsi yatafanyika katika uwanja wa Kampasi ya Chuo Kikuu cha Tanzibar { SUZA } uliopo Beit El Ras nje kidogo ya Mji wa Zanzibar.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar ambae pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Maadhimisho ya Kitaifa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi alikagua matayarisho ya mwisho ya maandalizi ya maonyesho hayo.


Balozi Seif alipata wasaa wa kuangalia mabanda ya Taasisi hizo ambazo 60 ni za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar 49 Taasisi za Serikali ya Jamuhuri ya Muungano  wa Tanzania pamoja na taasisi 13 za binafsi.

Mwenyekiti huyo wa Kamati ya Maadhimisho ya Kitaifa alionyesha kuridhika kwake na maandalizi ya mwisho ya maonyesho hayo kutokana na juhudi kubwa zinazoendelea kuchukuliwa na watendaji wa taasisi husika.

Hata hivyo baadhi ya Taasisi za Serikali na hata zile za binafsi zinaonekana kuendelea na matayarisho hayo katika mwendo wa kusua sua.

Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar alimalizia ziara yake kwa kuangalia banda la kitengo cha huduma za macho lilioko chini ya Wizara ya Afya ambapo watendaji wa kitengo hicho walimueleza Balozi Seif kwamba huduma za upimaji wa macho zitatolewa muda wote katika siku nne za Maonyesho hayo.



No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.