Habari za Punde

Maoni ya Hutuba ya Kamati ya Kusimamia Ofisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa.

HOTUBA YA MAONI YA KAMATI YA KUSIMAMIA AFISI ZA VIONGOZI WAKUU WA KITAIFA YA BARAZA LA WAWAKILISHI KUHUSU BAJETI YA OFISI YA MAKAMO WA PILI WA RAIS KWA MWAKA 2015/2016.

Mhe. Spika,
Kwanza naomba kwa sote tumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujaalia uzima na Afya njema na kuweza kukutana hapa kuweza kutekeleza majukumu tuliyopewa na wananchi wetu waliotuchagua.

Mhe. Spika,
Pili nikushukuru kwa kunipa nafasi ya mwanzo kwa niaba ya Kamati yangu kuweza kuchangia hotuba hii iliyowasilishwa na Mhe Waziri, wa Nchi Afisi ya Makamo wa Pili wa Rais, kwa utulivu na umahiri mkubwa.

Mhe Spika, Pia nimshukuru Mhe Waziri pamoja na watendaji wake kwa kuweza kushirikiana vizuri na Kamati kwa kipindi chote cha miaka mitano, mashirikiano hayo tunaamini yameleta ufanisi mkubwa kwa Wizara. Pia katika Serikali na ndio maana leo hii Waziri ameweza kusimama hapa mbele ya Baraza lako tukufu akijinasibu kwa mafanikio makubwa ya Serikali katika kipindi chao cha Awamu ya saba yenye mfumo wa Umoja wa Kitaifa ambapo hata sisi wananchi tumeridhika na hatua ya maendeleo inayopigwa na Serikali yetu huku Nchi yetu ikishuhudia utulivu, 

Amani na mashirikiano makubwa kwa viongozi wetu wakuu na hata sisi tunaofuata jambo ambalo limeleta hali ya amani kwa wananchi wetu wa kawaida, tunaomba wananchi wote vwa Zanzibar waendelee na utulivu huo hasa katika kipindi hiki kigumu kisiasa kwatika Nchi yetu kuelekea kwenye uchaguzi Mkuu wa 2015, kwa sote basi tumuombe Mwenyeenzi Mungu atujaalie na Amani yetu hadi kumaliza uchaguzi wetu mkuu kwa salama na Amani. AMIN.

Mhe Spika, tatu kwa niaba ya Kamati yangu niungani na wewe kwa Kumshukuru na kumpongeza Mhe Rais wetu D.k Ali Mohd Shein kwa uongozi wake bora na wenye busara kubwa kwa kuiongoza nchi yetu hii kwa salama na Amani katika vkipindi chake chote cha miaka mitano cha Serikali yake ya awamu ya Saba iliyopata mafanikio makubwa katika maendeleo ,ustawi wa jamii, na Amani na utulivu kwa muda wote wa miaka mitano, na pale ilipotokea dalili za vurugu hakuyumba ila alisimamia Katiba na Sheria za Nchi yetu katika kukabiliana na Changamoto hizo na leo hii tunajivunia Amani tuliyonayo na iko haja ya kuilinda kwa hali zote.

Mhe Spika, kwa kua hii ni Bajeti ya mwisho ya Serikali hii ya Awamu ya Saba basi naomba utuvumilie kwa kuchukua muda wako mwingi wa kuwapongeza viongozi wetu wa Nchi yetu, kwa hiyo nachukua fursa hii adhim kwa kutoa pongezi zetu maalum kwa Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar ,Mhe Balozi Seif Ali Iddi kwa uwezo wake mkubwa aliounyesha kwa kumsaidia Mhe Rais kuongoza Nchi yetu kwa umahiri wake, ustahamilivu na uvumilivu mkubwa wakati wote huo wa uongozi wake kwani amekua ni kiungo kikubwa baina ya Serikali na Baraza lako la Wawakilishi na pia amekua Balozi mkubwa wa Serikali kwa matakwa ya Serikali kwa wajumbe wa Baraza lako hili na hata pale tulipokua wagumu basi alitumia uzoefu wake wa Kidiplomasia kutulainisha na kweli tuliweza kulainika na mambo yao kama Serikali yalipita bila ya kupingwa, hii inatuonyesha kua kweli Zanzibar ni chimbuko la viongozi ,mahiri na wenye busara na wanaweza kuivusha Nchi yetu kwa salama na Amani katika mawimbi na misukosuko ya aina yeyote bila ya msaada kutoka nje, nadhani somo hili la Zanzibar iko haja na Nchi nyingine za kiafrika waje Zanzibar ili kujifunza namna ya kuweza kusuluhisha tofauti zao bila ya kumwaga damu na kuweza kuendesha Nchi zao kwa upendo na mashirikiano makubwa. 

Mhe Spika, pia naomba kutoa shukrani zetu za Kamati kwa Makamo wa kwanza wa Rais kwa ,kuweza kumsaidia Mhe Rais wa Zanzibar, katika kutekeleza majukumu yake kwa nchi yetu, pamoja na tofauti zao za kisiasa na wakati mwingine wananchi walipata wakati mgumu kuhisi labda kauli zinatofautiana lakini kimsingi bado kiujumla mambo mengi wamekua wakishirikiana na kwa kua tumeukubali mfumo wa vyama vingi wa kisiasa na pia tukaongezea mfumo mpya Duniani wa Serikali ya umoja wa Kitaifa inabidi tuwe wastahamilivu kwani ndio kipindi cha mwanzo cha mfumo huo kwa hiyo inabidi tuvumiliane, hapa kubwa kwa wananchi wetu tushukuru kuwa tumeweza kuvuka salama katika mfumo mpya wa kuongoza Nchi kama nilivyosema hapo awali basi wenzetu Nchi jirani na hata wa mbali basi wanaweza kuja kujifunza miujiza hii ilyotokea hapa Zanzibar, kwa hiyo naomba naomba wananchi wote tuige mfano ulioonyeshwa na viongozi wetu hawa wa kutoautiana bila ya kugombana. 

Mhe Spika, nitakua mwizi wa fadhila bila ya kukushukuru wewe mwenyewe binafsi kwa kuendelea kutuongoza kwa kipindi chote cha miaka mitano ya uhai wa Baraza hili la nane kwa umahiri mkubwa na busara zisizo na kifani katika kipindi cha hali ya utulivu Barazani na pale ambapo kunapotokea dalili za misukosuko umekua ukiirejesha hali ya utulivu Barazani bila ya kuonekanwa unapendelea upande wowote kati ya pande mbili zilizopo hapa Barazani hii inatuonyesha ni jinsi gani ulikomaa kwenye utendaji na uadilifu katika kusimamia haki, kwa kusaidiana na wasaidizi wako akiwemo, Naibu Spika, na Wenyeviti wa Baraza. Kwa hiyo mimi na Kamati yangu tumeridhika kabisa na uongozi wako.

Mhe. Spika,
Kama Waheshimiwa Wajumbe wako wanavyoelewa kuwa, Serikali imeanzisha rasmi utaratibu wa kuwasilisha Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Bajeti ya Serikali kwa mfumo wa kuzingatia program (PBB), mfumo ambao kwa Waheshimiwa Wajumbe wameshakuwa waelewa kutokana na juhudi za Serikali kwa kushirikiana na Baraza letu, lakini wanaowawakilisha bado ulelewa wao upo kama zamani, wa bajeti ya mfumo wa vifungu vya matumizi (Line Budget)

Mhe. Spika,
Pamoja na juhudi zilizochukuliwa na Serikali, sote tunakubaliana na ukweli kwamba, kumfahamisha mtu aliyetumwa ni lazima kuende sambamba na kumuelewesha yule aliyemtuma, kwani kumuelemisha aliyetumwa bila aliyetuma, ni sawa na kuufanya utumishi usiohitajika kwa wakati huo.

Mhe. Spika,
Nakusudia kusema kuwa, pamoja na juhudi za elimu ya bajeti ya mfumo wa PBB kutolewa kwa Waheshimiwa Wajumbe, elimu hiyo pia inapaswa kutolewa kwa watendaji katika ngazi za chini za Serikali, taasisi, mashirika, pamoja na wananchi ambao ndio waliowachagua na kuwateua Wajumbe wa Baraza hili, kwani mipango yote hiyo inamalizia kwao kwani ndio watakaopata huduma zilizokusudiwa.


Mhe Spika, kama alivyoelezea Mhe Waziri kuhusu hali ya kisiasa hapa Zanzibar kwa hivi sasa ni nzuri kwani kama tulivyoelezea hapo awali kuwa viongozi na wananchi wanaendelea kushirikiana katika shughuli mbali mbali za kiuchumi na kijamii, kwa hiyo tunamshukuru sana Rais wetu kwa kuweza kuisimamia kwa kikamilifu hali hiyo na kwa sote tumuombe Mwenyeenzi Mungu hali hiyo iendelee hivyo hivyo milele ili kuijenga nchi yetu kiuchumi kwani huko nyuma tumeshajifunza mambo mengi ya vurugu hayakutusaidia chochote ila kututia hasara kwa kujenga chuki baina yetu.

Mhe Spika, kamati yangu tunaendelea kumuunga mkono Mhe Waziri kwa kuwaomba wananchi wote wa Zanzibar kwa kua huko mbele Nchi yetu inategemea kuingia katika maamuzi magumu ya kinchi ya kupiga kura ya maoni ya Katiba inayopendekezwa kwa kupiga kura ya kuiamulia hatma ya baadae nchi yetu basi ni vyema wananchi wakaendelea kuzitafuta nakala za Katiba hiyo ili kuzisoma na kuzielewa vizuri ili siku ikifika kuweza kuipigia kura Katiba inayopendekezwa, kwa hiyo kamati yangu tunawaomba wananchi wote kuweza kuitumia haki yao hiyo ya msingi ya kidemokrasia ya kuamua wanachokitaka bila ya kubughudhiwa na mtu yeyote, kwani sisi wazanzibari kwa muda mrefu ndio tuliokua tukilalamika kua Katiba ilyopo hivi sasa inamapungufu mengi na wakati umefika kutokana na mabadiliko makubwa ya kisiasa na kiuchumi katika Nchi yetu basi iko haja ya kuweza kuirekebisha ili na sisi Zanzibar tuweze kutononoka kiuchumi.

Mhe Spika, sambamba na hilo pia si muda mrefu Nchi yetu inategemea kuingia katika mtihani mwingine wa wananchi kupiga kura ya kuweza kuwachagua tene viongozi wao ili kuweza kuwaongoza na kuwawakilisha katika kipindi kingine cha miaka mitano na kuiweka Serikali itakayowaongoza kwa kipindi kingine cha miaka mitano, hapa kamati yangu inawaomba tena viongozi na wananchi kuweza kuilinda Amani tuliyonayo na wala tusikaribishe viashiria vyovyote vya vurugu kwani huu utakua ndio mtihani wa mwanzo baada ya ya kuanzisha Serikali ya Umoja wa Kitaifa hapa Zanzibar, kwani tukifeli mtihani huu basi Zanzibar haitokuweko njia nyingine ya sulhu ya Amani kwani itakua vurugu ndio maumbile yetu, lakini sisi kama ndio viongozi tuliopewa dhamana na wananchi wetu kutuongoza basi ni vyema kuweza kua mstari wa mbele katika kuisimamia na kuilinda kwa maslahi ya wananchi wetu wanyonge.

Mhe Spika, Kamati yangu inaipongeza Serikali  kupitia hotuba ya Mhe Waziri kua tume ya Uchaguzi imeshajiandaa na kusimamia kura ya Maoni na uchaguzi Mkuu katika hali ya Amani na utulivu na kupitia kauli mbali mbali za viongozi akiwemo Mhe Rais, na leo Makamo wa pili wa Rais kuwa uchaguzi utakua wa huru na wa Haki kwa hiyo tunaiomba Tume ya Uchaguzi kuwa waadilifu katika kulisimamia hilo ili wananchi wote wa Zanzibar wenye haki ya kupiga kura basi waweze kuitumia haki yao hiyo ya msingi ya kuwachagua viongozi wao wanaowataka.kwa uhuru mkubwa bila ya bughudha yeyote, kwa hiyo kamati yangu inawataka wananchi wote waliotimiza masharti ya kupiga kura wakajiandikishe ili kuweza kuja kuitumia haki yao hiyo ya kikatiba ya kupiga kura.

Mhe Spika, kamati yangu pia inaungana na hotuba ya Mhe Waziri kwa kuipongeza Serikali yetu kwa kuendelea kuwaonyesha moyo wananchi wetu kwa kuwapunguzia mzigo wa maisha wananchi wetu kwa kufuta ada zote za kiingilio cha Skuli pamoja na kufuta ada ya mitihani yote kuanzia Skuli za msingi hadi form six ,hili ni jambo kubwa sana hasa kwa wananchi wetu wanyonge ambao hata mlo mmoja kwao ni shida, kwa mtu wa kawaida hili jambo jama kwani utakuta katika familia moja kwa wakati mmoja familia inao wanafunzi kiasi watano au sita kwa wakati mmoja na wote wanahitaji ada ya kiingilio cha Skuli na wengine ada ya mitihani jambo ambalo linampelekea mzazi kuchanganyikiwa kwani uwezo hana na wakati mwingine kushindwa kupata pesa na watoto kukosa haki yao ya msingi ya kupata Elimu.kwa hiyo tunawaomba vijana wetu kuunga mkono jitihada za Serikali yetu ili kuweza kuwapatia Elimu bora kwa hiyo wajitahidi katika kujisomea ili waweze kufaulu masomo yao, ili kuja kuijenga nchi yetu hapo baadae.

Mhe Spika, sambamba na hilo tunaipongeza Serikali kwa kuweka mazingira mazuri ya kuwawezesha vijana wetu waliofaulu masomo yao kuweza kupata mikopo kupitia Mfuko wa Elimu ya juu kwa masomo yao ya ndani na nje ya Nchi ,kwa hapa kamati yangu tunaiomba Serikali kwa mwaka huu pamoja na pesa zitakazotolewa kwa mfuko wa Elimu ya juu basi ikiwa wanafunzi wengi watajitokeza watakaohitaji pesa za mkopo basi kuangalia uwezekano kuongezewa fedha hizo kupitia pesa za kodi ya miundombinu tuliyoipitisha jana tu ili kuweza kuusapoti mfuko huu ili kuhakikisha kila kijana wetu anaehitaji mkopo wa Elimu ya juu basi aweze kupata fursa hiyo, lakini pia kamati yangu inaiomba Afisi ya Makamo wa pili wa Rais ambayo ndiyo inayoratibu na kusimamia shughuli zote za Serikali kufuatilia wanafunzi wote waliopata mikopo ya Elimu ya juu siku za nyuma ili kuweza kuanza kurejesha pesa hizo ili ziweze kuzunguka na wenzao waweze kuzitumia kwa ajili ya kujiendeleza kielimu.

Mhe Spika, kama alivyoeleza Mhe Waziri katika kitabu chake ukurasa wa 8 kif. (19.0) katika sekta ya Afya Serikali imeendelea kuboresha huduma za Afya na hapa tunaipongeza Serikali kwa kutekeleza ahadi yake kupitia Waziri wa Fedha pale kwenye Bajet ya mwaka uliopita tulipozuia Bajeti ya Wizara ya Afya kwa kushindwa kukitengeneza chumba cha ICU ambapo hali yake ilikua mbaya au hata kusema tulikua hatuna kabisa huduma ya ICU na kupelekea Waziri wa Affya kwa wakati ule Mhe Juma Duni Haji kutaka kujiuzulu lakini aliposimama Waziri wa Fedha na kumuokoa kwa kusema kua Serikali itahakikisha ICU kwa Hospitali kuu ya Mnazi mmoja itajengwa, leo tunafuraha kusema zile kelele zetu za wajumbe Wa Baraza clako hili tukufu kuitaka Serikali kujenga ICU tunathubutu kusema tumeridhika kabisa na tunaimani kwa hivi sasa huduma hiyo inatumika vizuri na wananchi wetu.

Mhe Spika, sambamba na hilo pia tunaipongeza Serikali kwa kusikia kilio chetu cha muda mrefu cha ukosefu wa madaktari bingwa na wauguzi kuwa kilio hicho sasa kimeanza kupungua kwa kuongeza idadi kubwa wa madaktari na wauguzi katika Hospitali yetu kuu ya Mnazi mmoja  na zile kilizoko katika vijiji vyetu, kwa kweli hivi sasa tunashuhudia tumeletewa madaktari na wahudumu kwatika Hospitali zetu ikiwemo na ile ya Jimbo langu la Kwamtipura kwakweli tunawashukuru sana.

Mhe Spika, sambamba na hilo tunaipongeza Serikali kwa kuandaa Shiria ya Condominium pamoja na kuanzisha Sheria ya kuunda Shirika la nyumba ili kuweza kuwawezesha wananchi wanaoishi katika nyumba za maendeleo pamoja na nyingine za Serikali kuweza kumiliki sehemu ya nyumba hizo kwa kushirikiana na Serikali lakini pia kuanzisha ujenzi wa makaazi ya wananchi kwa bei nafuu ili kuweza kuleta maisha bora na yenye faraja wananchi wetu. Kwa hiyo tunaiomba Serikali kuinazisha Mamlaka hiyo ya nyumba na wakabidhiwe watu wenye ubunifu na uwezo wa kuweza kuandaa mbinu za kupata fedha na kuweza nyumba hizo kwa haraka ili lile lengo la Serikali liweze kufikiwa kwa haraka.

Mhe Spika, kama alivyoeleza Mhe Waziri kuwa Serikali imeguswa sana na suala la udhalilishaji na ukatili wanaofanyiwa wananchi wetu hasa wakiwemo wanawake na Watoto, kwa kweli suala hili ni kubwa na linakera sana na linauma sana na linakera, kwakweli hivi sasa Zanzibar imekua ni aibu kubwa hasa unapowaona watu wazima wenye akili zao wanawabaka watoto wafdogo wengine hata hawajafiikia umri wa miaka kumi hii ni aibu kubwa kwa hiyo tunaungana na jitihada za Mhe Rais kwa kuunda kamati ya Mawaziri ili kushughulikia suala hilo, lakini tunaiomba kamati hiyo bado hatujaona makali yake kwani kila siku ikisikiliza habari za mawio utasikia kesi mpya za watoto kubakwa na wala hatusikii hukumu za watu waliobaka, tunaitaka Serikali kuhakikisha suala hili linakoma hapa Zanzibar.

Mhe Spika, suala la Rushwa limekua ni suala la kusikitisha sana na tunapongeza jitihada za Serikali kwa kuanzisha Sheria ya kupambana na Rushwa pamoja na  Sheria ya Maadili ya Viongozi, ingawa kuunda Sheria ni suala moja lakini tatizo linakuja katika kutekeleza Sheria hizo kwani tumeona kuna vitando vingi vya rushwa bado vinaendelea na nyingine ni za wazi wazi, lakini pia kuna ukiukwaji mkubwa taratibu za kisheria katika shughuli nyingi Serikalini nadhani wakati umefika tupunguze kuoneana muhali hasa katika mambo mazito ya shughuli za Serikali, ili kujenga jamii inayoheshimu Sheria na kufuata taratibu tunazojiwekea vinginevyo kila siku tutakua tunapiga kele kua Sheria hazifuatwi lakini wakosaji ndio sisi, kwa hiyo tunaomba kwanza tuanze sisi viongozi kufuata Sheria ili na walio chini yetu kuweza kutuiga vinginevyo na wao wataiga mifano yetu.

Mhe. Spika,
Kwa ujumla Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais, inahitaji kuidhinishiwa Tsh. 23,333,300,000 kwa matumizi ya kawaida na matumizi ya shughuli za maendeleo, fedha ambazo zinahitajika kwa Ofisi yenyewe ya Makamo wa Pili wa Rais, Baraza la Wawakilishi na Tume ya Uchaguzi. Aidha, kati ya Taasisi hizi tatu kuu, ni Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais pekee ndiyo yenye makadirio ya makusanyo kupitia Idara ya Upigaji Chapa na Mpiga Chapa Mkuu wa Serikali na Idara ya Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa, huku Taasisi zenye makadirio ya fedha za Maendeleo kwa mujibu wa taarifa zilizowasilishwa kwa Kamati, ni Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais pekee.

OFISI YA MAKAMO WA PILI WA RAIS

Mhe. Spika,
Kama alivyoeleza Waziri afisi hii inatarajia kukusanya Tsh. 612,360,000 kwa mwaka 2015/2016, fedha ambazo zitapatikana kutokana na huduma wanazozitoa Idara ya Upigaji Chapa na Mpiga chapa Mkuu wa Serikali, fedha ambazo ni Tsh. 600,000,000 kutokana na mauzo ya uchapishaji na Tsh. 12,360,000 zinatarajiwa kupatikana kutoka katika Idara ya Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa, ambapo Tsh. 3,000,000 zitatokana na malipo ya Ukodishaji wa Vifaa na Tsh. 9,360,000 zitatokana na malipo ya kazi za biashara.

Mhe. Spika,
Kamati yangu inafahamu kuwa, Serikali inajaribu kujitahidi kuwa na njia za uhakika za kufanya makadirio ya makusanyo ya fedha mbali mbali kwa kipindi cha mwaka wa bajeti, hasa kupitia katika Wizara na Taasisi zake mbali mbali. Bado hufanya makisio ya uzoefu wa mwaka ama miaka iliyopita katika kuamua na kuzielekeza taasisi zake kutafuta mapato kwa kupitia vyanzo mbali mbali vya makusanyo hayo. Kwa mfano, Mauzo ya Uchapishaji ambayo mwaka huu yamekisiwa kuwa Tsh. 600,000,000 ndio hizo hizo zilizokadiriwa mwaka uliopita. Aidha, fedha zilizokadiriwa kwa mwaka 2013/2014 kwa Idara ya Upigaji Chapa na Mpiga chapa Mkuu wa Serikali, zilikuwa Tsh. 500,000,000 kupitia Mauzo ya Uchapishaji, lakini fedha halisi zilizokusanywa zilikuwa Tsh. 42,776,200 kukiwa na tofauti ama upungufu mkubwa wa Tsh. 457,223,800, na mapato halisi yaliyopatikana ni sawa na asilimia 8.5 tu ya makadirio. Ambapo hali hii kama tunavyoelewa hali iliyokua nayo Idara hii ya Mpigachapa Mkuu wa Serikali hatushangai kua kweli walishindwa kutimiza malengo yao, kutokana na uchakavu wa mitambo pamoja eneo walilokua wakifanyia kazi lilikua katika hali mbaya sana, lakini kwa sasa kamati yangu inajinasibu kuwa zile kelele za Serikali kihamishia Idara ile katika katika eneo lililo salama ili waweze kufanya kazi zao kwa utulivu mkubwa kama tulivyoanza kuona hivi sasa.

Mhe. Spika,
Kamati yangu inakubali ni kweli Serikali kuwa, iliipa Idara dhima kubwa zaidi ya makusanyo kwa mwaka 2014/2015, ikizingatiwa kuwa mwaka 2013/2014, Idara hii na Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais kwa ujumla haikuweza kufikia malengo hata kwa asilimia 10 ya makadirio ya makusanyo. Na ndipo mwaka 2014/2015 kama ilivyo pia kwa mwaka 2015/2016, Idara hii kwa kupitia chanzo hicho hicho cha Mauzo ya Uchapishaji, kimekadiriwa kukusanya Tsh. 600,000,000. Kiwango ambacho ni kikubwa ukilinganisha na makadirio ya mwaka 2013/2014 na 2014/2015.

Mhe. Spika,
Kamati yangu kwa mwaka huu wa fedha kupitia vyanzo vya mapato vya Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais, imeshuhudia tena kuondoshwa kwa vyanzo vya mapato ambavyo vilikuwa vinatumika kwa miaka iliyopita. Kwa mfano, mwaka 2014/2015, Idara ya Uendeshaji na Utumishi ilikadiriwa kukusanya Tsh. 5,000,000 kupitia Ukodishaji wa Ukumbi wa Mikutano (Hire of Conference Seminar), chanzo ambacho kilianza kukisiwa na kuingizwa katika vyanzo vya mapato vya Idara hii mwaka 2013/2014 . kamati yangu imeridhika kwa mwaka huu kukiondoa chanzo hicho kwani hali ya ukumbi ule uliotegemea kukusanya mapato hauko katika hali nzuri, kwa hiyo tunaitaka Serikali kuweza kufanya maamuzi katika umilikaji wa Ukumbi huo wakati ambapo hata Baraza la wawakilishi waliomba uwe chini yao.

Mhe. Spika,.
Halikadhalika kwa Idara ya Sherehe na Maazimisho ya Kitaifa, mwaka 2013/2014 ilikadiriwa kukusanya Tsh. 3,000,000 lakini fedha hizo hazikukadiriwa hata shilingi moja kwa mwaka 2014/2015 na mwaka 2015/2016 chanzo hicho cha fedha hakionekani kabisa katika bajeti ya Idara hii, sawa ilivyo katika Ofisi hii ya Makamo wa Pili wa Rais.

Mhe. Spika,
Kwa upande wa matumizi ya kazi za kawaida, Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais inakadiriwa kutumia Tsh. 5,066,700,000 kwa ajili ya Mishahara ambazo fedha zitakazotumika kwa matumizi haya ni Tsh. 1,967,950,000, Maposho yatatumia Tsh. 703,179,000 na fedha za kuendesha Ofisi ni Tsh. 2,395,571,000. Aidha, kwa matumizi ya maendeleo, fedha zinazohitajika kwa mwaka huu wa fedha ni Tsh. 100,000,000, kwa kuzingatiwa kuwa Tsh. 24,550,000 zitatumika kwa matumizi ya uendeshaji wa mradi na Tsh. 75,450,000 zitatumika kwa matumizi ya utekelezaji wa mradi.

Mhe. Spika,
Fedha hizo zinatarajiwa kutumika kupitia program kuu nne ambazo ni Uratibu awa Shughuli za Makamu wa Pili wa Rais, yenye program ndogo hiyo hiyo. Program Kuu ya Pili ni Uratibu wa Shughuli za Serikali yenye program ndogo tatu ambazo ni Kukabiliana na Maafa, Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa pamoja na kuwaenzi viongozi wa Kitaifa na Shughuli za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar. Aidha, Program Kuu ya Tatu ni Usimamizi wa Shughuli za Upigaji Chapa ambayo program yake ndogo ni hiyo hiyo na Program Kuu ya Nne ni Mipango na Utawala yenye program ndogo tatu ambazo ni Uongozi na Utawala, Mpingango, Sera na Utafiti na Ofisi Kuu Pemba.

Mhe. Spika,
Ofisi inahitaji kupatiwa Tsh. 625,569,000 kwa Program Ndogo ya Uratibu wa shughuli za Makamu wa Pili wa Rais, ambayo pia ni Program Kuu fedha ambazo zitatumika zaidi kwa kuwapatia maslahi bora wafanyakazi, kulipia gharama za uendeshaji wa Ofisi, kuimarisha huduma za usafiri za Idara kwa kazi za kila siku, kununua vifaa vya kuandikia, vya usafishaji, samani pamoja na vifaa vyengine kwa matumizi ya Ofisi na kwa ajili ya mafunzo ya muda mfupi na ya muda mrefu.

Mhe. Spika,
Program Kuu ya Uratibu wa Shughuli za Serikali inahitaji Tsh. 2,239,727,000 ili iweze kutekelezeka na kwa upande wa Idara ya Maafa ambayo kwa kuzingatia mfumo wa Bajeti ya PBB, tunaweza kusema kuwa, shughuli zote za Idara hii zimo katika program ndogo ya Kukabiliana na Maafa chini ya Program Kuu ya Uratibu wa Shughuli za Serikali, kwa mwaka 2014/2015 ilikadiriwa kutumia Tsh. 298,447,800 kwa kazi za kawaida, na kwa mwaka huu wa fedha, Programu ndogo hii inahitaji Tsh. 405,775,000, ikiwa ni ongezeko la Tsh. 107,327,200.

Mhe. Spika,
Tunaipongeza Wizara na Serikali kwa ujumla kwa ongezeko hilo, lakini tufahamu kuwa, fedha hizo pamoja na  kuongezwa kwake na ikizingatiwa maafa yanayoikabili nchi yetu, ni fedha kidogo ambazo zinapaswa ziongezwe mara dufu. Kwa mfano tu ukizingatia maafa ya mvua zinazoendelea kunyesha, namna ya kukabiliana na maafa haya, kuwasaidia walioathiriwa na mvua, kunahitaji matumizi makubwa ya fedha, pamoja na ukweli wa kutarajiwa kutumika kwa fedha za mradi zinazohusiana na maafa kama tutakavyoeleza baadae. Hapa tunaiomba Serikali sasa kuanzisha rasmin ule mfuko wa maafa ili uweze kusaidia kutoa huduma kwa haraka pale maafa yanapotokea kwani maafa siku zote hayapigi hodi pale yanapotaka kutokea.

Mhe. Spika,
Program Ndogo ya Sherehe na Maadhimisho ya Kitaifa pamoja na kuwaenzi Viongozi wa Kitaifa ambayo shughuli hii mwanzo ilisimamiwa na Idara ya Sherehe na Maazimisho ya Kitaifa, kwa mwaka uliopita ilikadiriwa kutumia Tsh. 871,615,500 lakini kwa mwaka huu kwa kuzingatia program ndogo niliyoitaja kabla, fedha zinazohitajika kwa matumizi hayo ni Tsh. 987,260,000, ikiwa kuna ongezeko la Tsh. 115,644,500 sawa na ongezeko la asilimia 113.2 ya makadirio ya mwaka jana. Aidha, Kwa program ndogo ya Shughuli za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, fedha zinazohitajika kukamilisha fedha za Program Kuu ni Tsh. 846,692,000.

Mhe. Spika,
Program Kuu ya Usimamizi wa Shughuli za Upigaji Chapa ambayo program yake ndogo ni hiyo hiyo, imekadiriwa kutumia Tsh. 714,050,000 kwa mwaka 2015/2016, ambazo ni nyongeza ya Tsh. 231,983,400.
Fedha za program ndogo hii zinatarajiwa kutumika kwa kuwapatia stahiki na maslahi bora wafanyakazi ikiwa ni pamoja na maposho, mafunzo ya muda mfupi na muda mrefu (kwa wafanyakazi 7 wa Idara), kuimarisha huduma za uchapaji, ikiwa ni pamoja na ununuzi wa mafuta na vilainisho, kulipia gharama za umeme, kununua vifaa vya usafishaji, vespa, matengenezo ya mitambo na kununua zana na vifaa bora vya uchapishaji, kulipia gharama za matangazo na kuandaa mpango wa biashara, sheria na miongozo.

Mhe. Spika,
Program Kuu ya Mipango, Sera na Utawala inakadiriwa kutumia Tsh. 1,587,354,000 kwa mwaka 2015/2016 huku fedha hizo zikielekezwa kwa matumizi ya program ndogo ya Uongozi na Utawala (Tsh. 780,741,000), Mipango, Sera na Utafiti (Tsh. 271,792,000) na Ofisi Kuu Pemba (Tsh. 534,821,000).

Mhe. Spika,
Ofisi Kuu Pemba, mwaka 2013/2014 ilikadiriwa kutumia Tsh. 452,817,000 na fedha halisi zilizoingizwa hadi kufikia March 2014 zilikuwa Tsh. 254,014,050 sawa na asilimia 56 ya makadirio. Kwa mwaka 2014/2015, fedha zilizokadiriwa zilikuwa Tsh. 388,964,000 na fedha halisi zilizoingizwa hadi March 2015, zilikuwa ni Tsh. 85,815,350, kukiwa na upungufu wa Tsh. 303,148,650 ya makadirio. Hali hii bado inaonesha kuwepo kwa tatizo la uingizwaji wa fedha, bila ya kujali tuna mfumo gani wa bajeti. Idara ya Mipango, Sera na Utafiti ambayo sasa ni program ndogo ya Mipango, Sera na Utafiti kwa mwaka 2014/2015, kwa kipindi cha July hadi March, iliingiziwa Tsh. 55,621,903 na makadirio yalikuwa Tsh. 83,289,000 sawa na asilimia 88 ya makadirio.

Mhe. Spika,
Tsh. 100,000,000 zinazohitajika kwa matumizi ya miradi ya maendeleo, miradi ambayo imo katika Program Kuu ya Uratibu wa Shughuli za Serikali katika program ndogo ya kukabiliana na maafa, ambapo mradi wa Kujenga uwezo wa kukabiliana na maafa unahusika, huku Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imetenga kwa fedha za ndani Tsh. 15,000,000 kwa ajili ya kuandaa michoro na kusimamia Kituo cha huduma za dharura cha kukabiliana na maafa na Tsh. 35,000,000 kwa ajili ya kufanya matengenezo ya vituo vya kukabiliana na maafa.

Mhe. Spika,
Kamati imetaka kupatiwa fedha halisi za wafadhili zinazotarajiwa kuchangiwa na washirika mbali mbali wa maendeleo na kuelezwa kuwa ni Tsh. 204,950,000 kwa mwaka 2015/2016. Aidha, kwa mwaka 2014/2015, Serikali ilikadiriwa kuchangia Tsh. 40,000,000 na wafadhili kuchangia Tsh. 1,282,880,000 na hivyo, jumla ya Tsh. 1,322,880,000 zilikadiriwa kwa ajili ya kujenga uwezo na kukabiliana na maafa.

Mhe. Spika,
Kwa kuzingatia kuwa mwaka huu Serikali itachangia Tsh. 50,000,000 na wafadhili wa maendeleo kuchangia 204,950,000 kunaifanya bajeti inayokadiriwa kwa matumizi ya miradi ya program ndogo hii ya kukabiliana na Maafa kuwa Tsh. 254,950,000 wakati mwaka uliopita fedha zilizokadiriwa zilikuwa Tsh. 1,322,880,000 kwa upungufu wa 1,067,930,000, huku sote tukijua kuwa, kwa suala zima la kukabiliana na maafa, siku zote fedha huwa hazitoshi jambo linaloipekelea Serikali kuwa na uwezo mdogo sana wa kukabiliana na maafa hayo.

Mhe. Spika,
Kwa ajili ya utekelezaji bora wa progam ndogo ya shughuli za Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar iliyo chini ya program kuu ya Uratibu wa Shughuli za Serikali, inahitaji Tsh. 50,000,000 ambazo zitatumika kwa Mfuko wa Maendeleo ya Jamii (TASAF III) kwa kuzingatia uchambuzi ufuatao:
·        Tsh. 7,000,000 kwa ajili ya kusimamia miradi midogo 40 Unguja na Pemba.
·        Tsh. 2,900,000 kwa ajili ya kuratibu shughuli za miradi kati ya Zanzibar na Tanzania Bara.
·        Tsh. 5,300,000 kwa ajili ya kufanya vikao 8 vya Kamati ya Uongozi.
·        Tsh. 13,520,000 kwa ajili kusimamia shughuli za uendeshaji.
·        Tsh. 13,160,000 kwa ajili ya kufanya ziara za kikazi, mafunzo na kuandaa kikao cha ujumbe wa Benki ya Dunia.
·        Tsh. 3,500,000 kwa kutoa elimu kwa njia ya vipindi vya TV na Redio.
·        Tsh. 1,830,000 kwa kusimamia na kufuatilia miradi midogo midogo, na
·        Tsh. 2,790,000 kwa kuandaa vikao vinane vya Kamati ya Uongozi.

BARAZA LA WAWAKILISHI

Mhe. Spika,
Baraza la Wawakilishi nalo limekadiriwa kutumia Tsh. 16,762,600,000 kwa matumizi ya kazi kawaida, fedha ambazo zitatumika kwa mishahara (Tsh. 1,383,160,000), maposho (Tsh. 12,802,363,000) na matumizi ya uendeshaji wa Ofisi (Tsh. 2,577,077,000) ikiwa ni tofatuti na mwaka 2014/2015 ambapo Baraza lilikadiriwa kutumia Tsh. 14,564,000,000 kwa matumizi haya ya kawaida, ambapo kwa mwaka huu kuna nyongeza ya Tsh. 2,198,600,000 .

Mhe. Spika,
Fedha hizo zinazoombwa mwaka huu wa fedha zinatarajiwa kutumika chini ya program kuu mbili. Ya kwanza ni Kutunga Sheria, Kupitisha bajeti na Kusimamia Taasisi za Serikali ambapo program yake ndogo ni hiyo hiyo na program kuu ya pili ni Uongozi na Utawala wa Baraza la Wawakilishi yenye program ndogo hiyo hiyo.

Mhe. Spika,
Program kuu ya kwanza ambayo bila ya shaka program hiyo hiyo ni ndogo, inahitaji kupatiwa Tsh. 6,539,295,000, fedha ambazo zinahitajika kwa kujadili, kurekebisha na kupitisha miswada ya sheria; Kusimamia utendaji wa Taasisi za Serikali na kupitisha bajeti ya Serikali. Katika kutumiwa kwa fedha hizo hadi kufikia tarehe 30 Juni ya mwaka 2016, Baraza linaahidi mambo yafuatayo:
·        Kufikia asilimia 100 ya uwiyano wa miswada iliyopelekwa na kupitishwa katika Baraza la Wawakilishi.
·        Kupitisha miswada 14.
·        Wajumbe watakaokuwa wamechangia miswada ya sheria kufikia asilimia 40.
·        Kamati za Kudumu za Baraza zitakuwa zimeweza kutekeleza majukumu yake mara nne kwa mwaka na pia zimeweza kuwasilisha ripoti zao katika Mkutano wa March, 2016.
·        Baraza litaweza kupitisha bajeti ya Serikali katika kipindi cha bajeti ya mwaka 2016/2017.

Mhe. Spika,
Fedha zinazohitajika kwa program kuu ya pili ya Uongozi na Utawala wa Baraza la Wawakilishi ambayo pia ndiyo program ndogo ni Tsh. 10,223,305,000, fedha ambazo zitatumika kwa kuwapatia Wajumbe na Wafanyakazi wa Baraza lako huduma na stahiki zao na kuimarisha uwezo wao; kuimarisha mazingira ya kazi ya Afisi ya Baraza pamoja na kuratibu shughuli za Afisi ya Baraza Pemba.

Mhe. Spika,
Wajumbe wako wana haki ya kulihoji Baraza lako na kumhoji Waziri wa Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais na kuchukua hatua wanazoona zinafaa kwa mujibu wa Sheria na taratibu za Baraza iwapo viashiria vifuatavyo vitashindwa kufikiwa hadi tarehe 30 Juni 2016:
·        Iwapo asilimia ya Wajumbe na Wafanyakazi wa Baraza hawatopatiwa stahiki zao kwa asilimia 100.
·        Iwapo Wajumbe wote na Wafanyakazi 24 wa Baraza hawatopatiwa mafunzo.
·        Iwapo asilimia ya utekelezaji wa Mpango Kazi hautofikia asilimia 90 na huduma pamoja na matengenezo yanayohusiana na mazingira ya kazi yatafikia asilimia 100.
·        Iwapo wafanyakazi watapata huduma kwa asilimia 100 na Wafanyakazi watano watapatiwa mafunzo. Hayo yote yanategemea upatikanaji na uingizwaji wa fedha kwa wakati kama Program inavyotaka.

Mhe. Spika,
Mradi wa Maendeleo wa Kuwezesha Mabunge (Legislative Support Programme (LSP)) ambao mwaka jana ulikadiriwa kutumia Tsh. 710,615,000 kutoka kwa UNDP bila ya kuwa na mchango wowote wa Serikali, haukuwasilishwa maendeleo yake mbele ya Kamati na wala hauonekani katika bajeti ya Baraza la Wawakilishi. Bila ya shaka inaweza kuwa kunatokana na ule mkakati wa Serikali wa kupanga zile fedha za ndani ama za Wahisani wa Maendeleo wenye muelekeo mkubwa wa kusaidia, lakini kwa taarifa tulizonazo, wenzetu UNDP bado wanaendelea na nia ya kutusaidia. Kwa kua kuna tetesi kuwa wanategemea kuendelea kutusaidi basi ni vyema kukaandaliwa taratibu za kuuingiza kwenye Bajet yetu katika siku zijazo.

TUME YA UCHAGUZI

Mhe. Spika,
Katika mwaka huu wa fedha wa 2015/2016, Zanzibar tunaingia katika uchaguzi Mkuu na Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar ndie yenye jukumu la kuratibu na kukamilisha uchaguzi huo. Hali hii inaifanya Tume kutumia fedha nyingi katika maandalizi ya Uchaguzi.

Mhe. Spika,
Fungu laC.03 la Tume ya Uchaguzi linahitaji Tsh. 1,404,000,000 kwa ajili ya matumizi ya kazi zake za kawaida, ambapo Tsh. 501,758,000 zitatumika kwa malipo ya mishahara, Tsh. 630,982,000 zitatumika kwa maposho na matumizi ya uendeshaji wa Ofisi yatakuwa Tsh. 271,260,000. Kiwango hiki kilichokadiriwa mwaka huu na fedha iliyokadiriwa kwa matumizi ya kazi za kawaida mwaka jana ambayo ni Tsh. 1,314,100,000 kuna ongezeko la Tsh. 89,900,000 .

Mhe. Spika,
Tume ya Uchaguzi ina porgramu kuu mbili. Programu ya Uendeshaji na Usimamizi wa Shughuli za Uchaguzi ambayo program ndogo yake ni hiyo hiyo, na Program Kuu ya pili ni Usimamizi wa Kazi za Utawala na Uendeshaji wa Shughuli za Tume ya Uchaguzi ya Zanzibar yenye program ndogo mbili, ya Usimamizi wa kazi za Utawala na Uendeshaji wa Tume ya Uchaguzi, pamoja na Uratibu wa Shughuli za Uchaguzi Pemba.

Mhe. Spika,
Program Ndogo ya Usimamizi wa Kazi za Utawala na Uendeshaji wa Tume ya Uchaguzi inahitaji kupatiwa Tsh. 1,214,021,000 na Program ndogo ya Uratibu wa Shughuli za Uchaguzi Pemba upatiwe Tsh. 189,979,000 fedha ambazo kwa ujumla wake zitatumika kwa kuboresha maslahi ya wafanyakazi, kuimarisha mazingira bora ya kufanyia kazi,  kuwajengea uwezo uwezo wafanyakazi na kufanya ukaguzi na upimaji uwajibikaji.

Mhe. Spika,
Fedha za Maendeleo hazikuonekana katika bajeti iliyowasilishwa kwa Kamati, wakati Kamati yangu inafahamu kuwa mwaka jana, Tume ilikadiriwa kutumia fedha za maendeleo katika mradi wa kuimarisha demokrasia, uliowadhiliwa na UNDP kwa makadirio ya Tsh. 1,750,000,000. Ni vyema Kamati pamoja na Wajumbe wakafahamu mradi wa maendeleo unaotarajiwa kuwa Tume ya Uchaguzi kwa mwaka huu wa fedha.

Mhe. Spika,
Sasa naomba kukushukuru wewe na Wajumbe wote wa Baraza la Wawakilishi kwa usikivu wenu wa kunisikiliza tokea mwanzo wa hotuba yangu hadi hivi sasa. Napenda pia kwa niaba ya Kamati, kumshukuru Makamo wa Pili wa Rais, Mhe. Waziri Mohamed Aboud Mohamed, Katibu Mkuu na Watendaji wote wa Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais, kwa juhudi zao na ujasiri na moyo wa uzalendo katika kuiongoza Ofisi hii ya Makamo wa Pili katika kipindi chote cha miaka mitano sasa.

Mhe. Spika,
Nikushukuru wewe pamoja na Katibu wa Baraza la Wawakilishi pamoja na watendaji wote wa Afisi ya Baraza kwa huduma wanazozitoa kwetu Wajumbe na tunaendelea kuwanasihi wasichoke kutoa huduma bora kwa Wajumbe wote wa Baraza kwa kufuata ipasavyo Sheria na Kanuni za Utumishi na kwa mazingira pekee ya huduma inavyotolewa Barazani. Mhe. Spika, Tunamshukuru pia Mkurugenzi wa Tume ya Uchaguzi na watendaji wake wote kwa mashirikiano waliyoyatoa kwa Kamati katika kipindi chote cha uhai wa Kamati.

Mhe. Spika,
Shukurani za pekee ziwaendelee Wajumbe wa Kamati kwa mashirikiano ya pamoja na kuaminiana katika kazi zetu. Naendelea kuwaombea Wajumbe hawa kurejea tena katika Baraza linalokuja ili kwa uzoefu walioupata katika kazi zao mbali mbali ikiwa ni pamoja na kazi za Kamati, na elimu waliyofunzwa na Afisi ya Baraza na Taasisi nyengine mbali mbali zinazohusika pamoja na wataalamu binafsi, waweze kuzitumia katika kuwafunza na kuwajenga uwezo wajumbe wenzao hasa wala ambao mara ya kwanza wamefika katika Baraza hili na kuzisaidia Kamati za Baraza kutekeleza kazi zao kwa ufanisi mkubwa.

Mhe. Spika,
Naomba uniruhusu sasa niwatambue Wajumbe wote wa Kamati kama ifuatavyo:-  
1.    Mhe Hamza Hassan Juma                      Mwenyekiti
2.   Mhe. Saleh Nassor Juma                        Makamo Mwenyekiti
3.   Mhe. Ali Mzee Ali                           Mjumbe
4.   Mhe. Ashura Sharif Ali                          Mjumbe
5.   Mhe.Shadya Mohammed Suleiman             Mjumbe
6.   Mhe. Makame Mshimba Mbarouk           Mjumbe
7.   Mhe. Subeit Khamis Faki                      Mjumbe
8.   Ndg.Rahma Kombo Mgeni                  Katibu
9.   Ndg.Othman  Ali Haji                        Katibu

Mhe. Spika,
Nimalizie shukurani zangu kwa Makatibu Kamati yetu, ambao ndio macho na masikio ya Kamati. kutoona kwao, ni sehemu kubwa ya upofu wa Kamati na kutosikia kwao yenye maslahi na maendeleo ya Zanzibar kupitia utekelezaji wa majukumu yao, kuna mchango mkubwa wa Kamati zetu kutofanikiwa katika utekelezaji mzima wa majukumu yake.

Mhe. Spika,
Naomba kuwasilisha.

Hamza Hassan Juma
Mwenyekiti,
Kamati ya Kusimamia Afisi za Viongozi Wakuu wa Kitaifa
Baraza la Wawakilishi,

Zanzibar.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.