Habari za Punde

Mhe. Amina Asisitiza kufanyiwa kazi Sheria ya Maendeleo ya Karafuu


Na Majid Omar Najim

Waziri wa Biashara, Viwanda na Masoko Zanzibar Mhe. Amina Salum Ali amevitaka vyombo vinavyosimamia Sheria kuhakikisha Sheria ya Maendeleo ya Karafuu inatumika ipasavyo ili uwepo wake uweze kuleta tija kwa wakulima na Taifa.

Alisema Baraza la Wawakilishi limekamilisha wajibu wake wa kutunga sheria hiyo hivyo sio sahihi kuwa sheria hiyo isitumika ipasavyo. Alisema vitendo vya makusudi vya hujuma dhidi ya Sekta ya Karafuu haviwezi kufumbiwa macho na lazima Sheria itumike ili kutoa haki inayostahiki.

Aliyasema hayo wakati akifunga semina ya mafunzo ya siku moja ya kuwafahamisha wasimamizi wa Sheria- Jeshi la Polisi, Wapelelezi na Mahakimu kuhusu Sheria No. 2 ya Maendeleo ya Karafuu ya mwaka 2014 iliyofanyika katika ukumbi wa Zanzibar Ocean View, Kilimani Zanzibar.

Alitolea mfano tukio la uchomaji moto wa mashamba ya mikarafuu uliotokea katika Shehia ya Mzambarauni Mtambwe, Mkoa wa Kaskazini Pemba, ambapo mikarafuu 151 iliteketea kwa moto na kusema vitendo kama hivyo vinatokana na usimamizi duni wa Sheria hiyo.

Alisema kuwa iwapo wadau wa sekta hiyo hasa wasimamizi wa Sheria likiwemo Jeshi la Polisi, Wapelelezi wa Makosa, Mahakimu na Wanasheria wataitendea haki Sheria hiyo basi Sekta ya Karafuu itakuwa ni faraja kubwa kwa wakulima wa zao hilo.

“Nimeisoma vizuri Sheria hii, nimeiona imeweka misingi imara ya haki, kama itafanyiwa kazi kwa vitendo basi hakuna shaka zao la karafuu litabadilisha hali ya uchumi wa Zanzibar”. Alifahamisha Mhe. Amina.


Akifungua Mafunzo hayo, Jaji wa Mahakama Kuu Zanzibar Rabia Husein Mohamed alisema Sheria ya Maendeleo ya Karafuu imetungwa kwa ajili ya kulinda maslahi ya wakulima na wananchi wanaojishughulisha na zao la karafuu pamoja na wadau wengine wote.
  
“Sheria hii ni msingi imara wa kuijenga na kuiimarisha Sekta hii ya karafuu katika mazingira yote, maendeleo ya Zanzibar na ustawi wa wakulima wa zao la karafuu, wananchi wanaojishughulisha na biashara ya karafuu na wadau wote wenye maslahi ya moja kwa moja au kupitia kwa njia nyengine za kujenga uchumi wa nchi wanamatumaini makubwa na Sheria hii”. Alifahamisha Mhe, Rabia.

Aliwasisitiza wasimamizi wa Sheria kutekeleza wajibu wao kwa kuhakikisha kuwa haki inatendeka kwa pande zote na hakuna anaedhulumiwa katika utekeleji wa Sheria hiyo, na pale penye utata suluhisho lifanyike mara moja ili isije kuleta athari ya kutotendeka haki kwa wahusika.

Akiwasilisha Sheria hiyo No. 2 ya Maendeleo ya Karafuu Katibu wa Shirika la Biashara la Taifa la Zanzibar (ZSTC) Ali Hilali Vuai aliainisha makosa yaliyoanzishwa na Sheria hiyo na kanunui zake kuwa ni kuhujumu mkarafuu kwa aina yoyote, kuchafua karafuu kwa makusudi na kuanika karafuu isivyotakiwa.

Akiwasilisha tathmini ya Zao la Karafuu Zanzibar mtaalamu wa Kilimo kutoka Wizara ya Misitu na Maliasili Badru Kombo Mwamvura alisema Sekta ya Kilimo cha Karafuu inakabiliwa na changamoto nyingi hivyo Sheria hiyo inahitaji ifanyiwe kazi ipasavyo ili kukabiliana na changamoto hizo.

Alizitaja baadhi ya changamoto hizo kuwa ni uharibifu wa Mikarafuu kwa makusudi, ukatajaji wa mikarafuu, wizi wa karafuu, ujenzi na uchimbaji mchanga ndani ya mashamba ya mikarafuu.

Kwa upande wao baadhi ya washiriki kutoka vyombo vya kusimamia Sheria walisema ili Sheria hiyo iweze kutimiza lengo la kuundwa kwake lazima kuwepo kwa ushirikiano mkubwa baina ya Polisi, Mahakama na  Waendesha mashtaka.

Mwanasheria Mfawidhi kutoka Afisi ya Mwendesha Mashtaka (DPP) Zanzibar, Suleiman Haji Hassan alisema kesi nyingi zinazotokana na karafuu zimekuwa hazifiki katika mamlaka husika kutokana kutowajibika ipasavyo kwa baadhi ya taasisi za Kisheria.


“Nina kumbukumbu ya kesi moja tu iliyotufikia, hii inaonesha ni jinsi gani hakuna ufuatiliaji wa kesi hizi, na hata pale zinapofuatiliwa basi huwa zinaishia kuamuliwa kienyeji ”.Alibainisha.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.