Na.Haji. Nassor, Pemba.
MWISHONI mwa mfungo wa mwezi mtukufu
wa ramadhani, waislamu duniani kote, huungana pamoja kuadhimisha sikukuu ya
Eidel-fitry.
Waislamu,
baada ya kutimiza mfungo huo, kisheria hulazimika kusherehekea sikukuu hiyo,
kwa kula, kunywa na kuvaa vizuri tena imesisitizwa viwe vile vya halali.
Yapo mambo kadhaa
ndani ya siku hiyo, yamekatazwa kisheria kuyafanya, ikiwa ni pamoja na kufunga,
kunywa ulevi, zinaa, kufanya kazi ingawa kwa kipindi maalum.
Ingawa kila
tendo linalopelekea dhambi, limeshapigwa vita na kupingwa vikali na maandiko
matakatifu, lakini siku hiyo ya sikukuu yamesisitizwa zaidi, kuyaacha.
Yapo pia
yaliogogotezewa kufanywa ndani ya sikukuu, kwamba yanaongeza sunna zaidi, ikiwa
ni pamoja na kutembelea wagonjwa, kuwasaidia wasiojiweza, kuwatembelea ndugu na
jamaa hasa waliokaribu.
Ingawa kwa
mtindo usiokubalika, wapo wanaosherehekea sikukuu hiyo kwa kupanda magari
yalioruhusiwa kubeba abiria 20, ingawa huanzia 30 hadi 45 wengine wajirusha kwa
mwendo kasi .
Inawezekana
wanafanya hivyo, kama sehemu ya sherehe, ingawa wanajua kuwa, kwenye uislamu
hakuna sherehe ilioruhusiwa kwa kuvunja sheria hata kama ni za nchi, maana
haziathiri uislamu.
Suala la kuheshimu
sheria za nchi, linamgusa kila mmoja, na wala ujio wa sikukuu hii ilioko mbele
yetu, haijaruhusu na wala haina mamlaka ya kuwataka vijana na wazee wa kiislamu,
kuvunja sheria za usalama barabarani.
Walishasema
wataalamu wa sheria na wanazuoni, kuwa kila kitu kinachofanywa, ni vyema ikaangaliwa
sheria kwanza, kwa hapa Tanzania na Zanzibar kuelekea sherehe hizi za sikukuu,
hilo linapaswa kuliangaliwa.
Lazima
ujiulize suali, tena ni vyema na kujitafutia na jibu wewe mwenyewe, kama
umeshafunga mwezi mzima wa ramadhani ukiamini kuwa kufanya hivyo ni wasjibu,
sasa je kuvunja sheria za usalama barabarani unadhani ni sunna.
Mwendo kasi,
kupakia watu zaidi ya uwezo wa gari, ulevi na kisha kuendesha gari, gari za
mizigo kufanywa ndio za kubebea abiria, unadhani haya ni sahihi.
Kwa mfano,
sheria ya uchaguzi ya Zanzibar no 11 ya mwaka 1984, kwenye kifungu chake cha
56, kimehalalisha suala la vyama kufanya kampeni, ingawa sio kwenye nyumba za
ibada.
Kumbe nalo
hilo lipo kisheria, kama kilivyo kifungu cha 7, kinavyoeleza haki ya kupiga
kura kwa mzanzibari alietimiza masharti kwa mujibu wa sheria.
Kama kila
jambo linafuata sheria, iweje kipindi cha sikukuu wazazi na walezi kuwaruhusu hasa
watoto na vijana wao, kujazana pomoni kwenye magari kama vile sheria ya usalama
barabarani imeenda likizo.
Kwa hili la
kuvunja kwa sheria ya usafiri barabarani, kwa waislamu kwa kisingizio cha
kusherehekea sikukuu, na kisha kujazana kama makumbi kwenye gari, mbona
hufanywa kama vile sheria au katiba imeridhia.
Ingawa juzi
Kamanda wa Polisi mkoa wa kusini Sheihan Mohamed Sheihan, wakati akizungumza na
ukurasa huu, alishatamka kuwa mara hii wapiganaji wake watakua makini na hilo.
Iweje kwenye
nchi moja sheria nyengine ziwe makini kusimamiwa na hata wananchi wenyewe,
mfano kumpiga bakora aliegundulika kula mchana wa ramadhani, lakini hili la
kuvunja sheria barabarani liwe baridi.
“Katika hili jeshi la Polisi, halitaangalia mtu
usoni, gari inayobeba abiria 20 ikizidisha, taratibu za kisheria zitafuata mkondo wake, maana wengi wanadhani, kipindi
cha sikukuu kama vile sheria hazipo’’,alisema.
Kama kila
kitu kinapaswa kifanywe kwa mujibu wa sheria, ni lazima sheria ya usalama
barabarani ya Zanzibar no 7 ya mwaka 2003, ifuatwe kikamilifu, maana hili ni
kwa maslahi ya watu wote.
Lakini jeshi
hilo katika sherehe hizo za sikukuu, limeaapa kupambana na wale wanaoendesha
vyombo vya magaurudumu mawili, kwa mwendo kasi “tako moja’.
“Hawa ndio
wamekuwa wachafuzi wakubwa wa sheria za barabarani na kupelekea wanaosherehekea
kujaa na hofu ya usalama, sasa lazima tutawaangali mara mbili”,alisema Kamanda.
Kama katiba
ni sheria mama, basi ile ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Ibara yake
ya 13, na ya Zanzibar kifungu cha 12 vimetamka, lazima kuwe na usawa mbele ya
sheria, iweje kipindi cha sikukuu usalama barabarani uwe rehani.
Na ndio
maana Jeshi la Polisi mkoani wa kusini Pemba, likaenda mbali na kuvitaka vyombo
vyengine vinavyosimamia, kuwa gari iliosajiliwa kwa ajili ya kubeba mizigo, yatatiwa
mkononi ikiwa yatagundulika kubebea watu kwenye siku zote za sherehe.
“Tumegundua
hata magari ya aina hiyo hubeba watu kupindukia, hivyo inapotokea ajali, hata
idadi ya wanaoumia au kufariki huwa kubwa’’,alisema kamanda wa Polisi.
Mwananchi Aisha
Hassnuu Omar (30) mkaazi wa Wawi Pemba, anakumbuka vyema mwaka juzi, kulipotokezea
ajali eneo la Chanjamjawiri, baada ya gari iliobeba vijana waliokuwa wakitokea
kwenye sherehe za sikukuu na kupinduka.
“Mimi naona
jeshi la Polisi kipindi cha sikukuu kama wanaopata mapumziko ya kazi zao,
kwanini wanaona gari ya abiria imejaa kupindukia lakini
hawaisimamishi’’,alihoji.Bimkubwa
Haji Ali (29) wa Chake chake, anasema sheria za usalama barabarani, hutakiwa
kusimamiwa wakati wote, ingawa Polisi kipindi cha sikukuu huachia wenye magari
wafanye watakavyo.
Dereva wa
gari ya abiria Said Haji Kombo (30) anaebeba abiri Chake chake - Wete,
anashangaa kuona siku za kawaida abiria mmoja akizidi, dereva na kondakta wake
hufikishwa mahakamani, ingawa wakipeleka watu kwenye sherehe za sikukuu hawaulizwi.
“Sisi
madereva hata abiria wakijazana kiasi gani hatuathiriki, maana pesa
inaongezeka, lakini kazi ya kupekua na kuhesabu abiria, polisi waifanye vipindi
vyote’’,alishauri.
Kondakta wa
gari ya Mkoani- Chake Ali Muhusin, yeye anadhani kipindi cha sikukuu, kama vile
askari wa usalama barabarani wamepewa tamko la kuzisamehe gari za abiria na wajaze
wapendavyo.
Sheria no7 ya
Zanzibar ya mwaka 2003 ya usafiri barabarani, imetamka makosa kadhaa ambayo mtu
akiyafanya atakua ni mkosaji, kwa mfano kuzidisha abiria.
Sheria
inaelekeza dereva akizidisha abiria aliosajiliwa kwenye gari yake, adhabu yake
ni kutoza faini ya dola 10 za marekani, sawa na wastani wa shilingi 1,400,
sambamba na dola 5 kwa kila abiria aliezidi.
Ingawa
sheria ikafafanua kuwa, kama hilo ni kosa la pili, sasa faini itakuwa dola 15,
kwa kila abiria aliezidi, ambapo ufafanuzi kwa abiria aliezidi ni yule aliekaa
chini.
Sasa kwenye
kipindi cha kuelekea sikukuu, wapo madereva huruhusu gari zao, kupakia watu hadi
juu ya bodi, ingawa sheria ya usafiri barabarani ipo saa 24.
No comments:
Post a Comment