Habari za Punde

Nasiha za Bi Hekima:Jinsi wanawake tunavyodhalilishwa kwa ujanajike wetu mpaka na tunaowazaa!

Na Bi Hekima

Leo nina ujumbe mzito wa kutuma.

Nimeamua kufunguka na kutominya maneno maana naona sasa mambo na maneno yanavuka mipaka ya kiasi, uungwana na heshima kwani kuna waja wamelewa kibri, majigambo na majivuno, ubabe na ujinsi kiasi cha kumgeuza Mwenyezi Mungu mshiriki wao katika tabia, kauli na mila ambazo hakika haziakisi sifa wala utukufu wa Mwenyezi Mungu.

Kuna matukio matatu ambayo nitayajengea kupambanua hoja yangu. Jana nlikua maeneno ya Amani dukani. Wakati nataka kurudisha gari nyuma ntoke nilipopaki ilisadifu kuwa askari kazuia gari ili wanafunzi wavuke.

Wakati narudi nyuma niingie barabara kuu kuna vitoto vya kiume wa darasa la 2 mpaka la nne baadhi wakiwa wamepanda baiskeli wanapita pia njia hiyo. Sijaamini maskio yangu niliposkia kauli yao ya kunitaka ntoke njiani wakisema "huyu mwanamke si afanye atoke! Huyu mwanamke atatuweka hapa!" Mtoto ninayemjukuu ananiita we mwanamke?!  Hawa watoto ndo wanaonekana wanaenda skuli, chuoni na darsa kujifunza kuwa mwanamke hata wa size ya dada, mama, shangazi au bibi yako ni "mwanamke tu!" Tena hukwita kama taka taka fulani hivi.

Lakini inapaswa nisishangae maana huu wa kuwadhalilisha, kuwapuuza na kuwadharau wanawake ni utamaduni ulioenea hata kwa wanaojivunia kuwa "wacha mungu".

Wapo waja wanaamini kuwa waliotukuzwa na wanaofaa ni wanaume tu. Si kwa sababu yoyote ila jinsi yao tu. Hivyo kuna mja mmoja kuna siku tunaenda kusali ikasadifu wanaume wanasali juu wanawake chini akatukejeli kwa kusema "huko ndio kwenu. Nyinyi daima watu wa chini tu!" Narudia alikuwa naye anaenda kusali lakini roho yake ina mawazo na mtizamo kuwa yeye "bora" kwa vile tu ni mwanamme.

Majuzi nlikua nimemtemblea mtu nka paki gari sehemu nliokuta wengine wameweka. Ingawa nafasi ilikua imebanwa kwa vile gari yangu ndogo ikaingia. Nimeacha njia ya kuweza kupita mtu. Nikiacha mzigo tu mitaa ya ng'ambo hivyo nlikua sina ukaazi hapo baada ya dakika nkatoka.

Kwa mshangao nkakuta kuna mtu kaweka pikipiki yake mbele ya gari yangu. Nimesubiri mda kuona kama miongoni mwa waliokaa vibarazani watasema chochote au kuja kuondoa. Kila mmoja kabaki alipokuwa wana 'check' situation.

Baada mda akapita kijana mmoja nkamuomba nsaidie kuiweka pembeni kidogo niweze kutoka. Mara akatoka kijana na jiwe, mtoto ambaye namzaa kwa umri mkubwa tu, akitufurumushia matusi ya "mwanaharamu wewe, ….nina …mamako ishike uone!!"....Hakika sijamfahamu nini maana yake.

Hata hivyo akaja akaiondoa pikipiki yake akilalama kuwa nilipoweka gari ni "njia kubwa". Mimi sijaona njia. Nimeona uchochoro wa wapita kwa miguu. Hilo mmoja pili hakujakuwa na namna ya kusema kuwa hapa kuna njia huwa tunatumia siku nyingine gari jitahidi kuiweka vile! Inakuwaje mtoto mdogo kwa vile tu "mwanamme" anadhani ni haki yake kuongea na wewe anavyotaka au hata kukuvunjia heshima? "Ndio pepo iko chini ya miguu ya mama hiyo?" Ndivyo kumtukuza mwanamke hivi?

Tena narudia kuwa sishangazwi kwani wakuwafunza nao hawana busara, hawana malezi, hawana upeo na wala hawana 'humility'. Ukisikiliza yanayoitwa mawaidha ambayo yanarushwa masaa 24 katika radio na kanda na hata katika cable basi asili mia 95 ya mawaidha hayo ni kuhusu wanawake. Kati ya hayo 5% ni kuhusu utii wa wanawake kwa 'wanaume hasa waume zao. Mawaidha yaliyobaki ni kuwakejeli, kuwa kebehi, kuwa laani, kuwa umbua, kuwa kosoa alimradi kuwatoa kila walakini kuwanyima utukufu na utu wao.

Sijaona popote mwanamme anahakikisha chochote au akitajwa kuwa BORA kwa vile tu yeye  ni mwanamme. Wala sijaona popote ambapo alichoharamishiwa mwanadamu kimeharimishwa kwa misingi ya ubaguzi. Wala sijasoma popote ambapo Mwenyezi Mungu anahimiza binadamu wadhalilishane, au wahujumiane au waumbuane au wakebehiane.  Sasa ubavu huu wa kibri kiliokithiri wanaume wanaojiita waislamu wanaupata wapi?  Watakaa katika majukwaa wakibwabwaja maneno bila ya kujali aina ya hadhira iliyopo  ila ya kuwa na kiasi au uchaguzi nini wanasema na nani wanamwambia na kwa malengo yepi.

Ninalolitambua mimi ni kuwa waja wa namna hii na 'siasa zao za jinsi au za dini' hazina malengo mema ya kukuza upendo au heshima kati ya watu.

Nina hakika katika moyo wangu kuwa Mwenyezi Mungu anayehubiriwa siye Mwenyezi Mungu aliyemjaalia kila mwanadamu utukufu. Nina hakika kuwa kamwe kwa kuumba viumbe tofauti katika dunia dhamira ya Jalali kamwe haikuhusu kunyima wengine utu na kuwafanya wengine Bora wakuu wa kiburi na majivuno.

Nina hakika kuwa hakuna utukufu katika tabia iliyomfakarisha sheitan na Muumba wake hivyo imani ya namna hiyo haiwezi kuwa na tija. Na nina hakika silazimiki kuvumilia, kukubaliana wala kuweka uzito katika matamshi, utamaduni na utashi unaojenga na kupalilia tabia za kishetani.

KUBWA zaidi kama mwanamke Si RADHI kwa matamshi, maneno ama kauli zenye lengo la kuudhalilsiha utu na utukufu wangu. SI RADHI na watu wanaoneza utamaduni unaohimiza watu kudharauliana, kubezana au kuumbuana.


Ijumaa hii namuomba mwenyezi Mungu awazindue waja waliojisahau na kumfuata 'shaitan' kwa mawazo na majivuno awazindue na watubie, la kama walizaliwa na mwanamke kama mimi, wakalelewa na kukuzwa na mwanamke kama mimi na wakapata faraja na maliwazo kwa mwanamke kama mimi wakaosa kumshkuru, kumheshimu na kumuenzi basi hujuma zao ziwarudi, ziwasute na ziwafadhaishe kwa udhalimu wanaotufanyia na kwa upotofu wanaosababisha hata kwa kizazi kinachoinukia. Ya Rabbal Alamin.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.