Habari za Punde

DC Wilaya ya Mkoani awataka viongozi kufanya kazi kwa uadilifu


Habiba Zarali, Pemba
MKUU wa Wilaya ya Mkoani kisiwani Pemba, Issa Juma Ali, amewataka viongozi wa Wilaya hiyo kufanya kazi zao kwa uadilifu , kufuata sheria na mipaka inayowaongoza, ili waweze kutimiza majukumu yao kikamilifu bila ya hitilafu yoyote kujitokeza.
Kauli hiyo aliitowa huko Ofisini kwake ,alipokuwa akizungumza na viongozi mbalimbali wakiwemo masheha  na madiwani wa wilaya hiyo kwa lengo la kuwatambulisha wajibu wao katika kuwatumikia wananchi.
Alisema  upatikanaji  wa  ufanisi katika kazi  hutokana na mashirikiano  yaliyopo kati ya  viongozi ambao ndio watoa huduma  na wananchi wanaopokea huduma hizo.
Alifahamisha kila mmoja ni vyema akafanya kazi zake bila ya kumuingilia mwenzake ili kuhakikisha maendeleo yanapatikana bila ya chuki na uhasama ndani yake.
“Katika kazi kila mmoja ana majukumu yake ya kufanya hivyo basi ni vyema mukawa na umoja na mashirikiano ili kazi zenu ziweze kufanikiwa na kuleta tija”, alisema.
Aidha mkuu huyo wa wilaya,  aliwataka watendaji  hao kuendelea kusimamia shughuli zote  za maendeleo  na kutoa taarifa  kwa vyombo vinavyohusika kwa kila linalotendeka.
Kwa upande wak,e Sheha wa Shehia ya Ng’ombeni , Subira Iddi Mohamed, alisema pamoja na mashirikiano  hayo ipo haja ya kuongeza  nguvu katika sekta  ya elimu ili wanafunzi waweze kuleta matokeo mazuri zaidi.
Alisema wapo baadhi ya  wanafunzi wilayani humo  hushindwa kushuhulikia masomo yao  na kujishughlisha na  mambo yasiyo wahusu  ikiwa ni pamoja  na kuangalia  Tv  hadi  saa  sita za usiku jambo ambalo linachangia kuleta matokeo mabaya.
Alieleza kutokana na umuhimu wa elimu ni vyema yawepo mashirikiano ya pamoja kati ya wananchi na viongozi wao kwani muda utakapowapita watoto hao bila ya kusoma hawatoweza kuipata tena elimu waliyoikosa .
“Bila ya kuwaekea mikakati madhubuti ya kujishughulisha na kusoma wanafunzi wataharibika na tutabakia na janga la vijana wasio na muelekeo katika wilaya yetu na kuiwekea serikali mzigo usiobebeka ”, alisema .
Nae  Diwani wa kuteuliwa  wilaya ya Mkoani,  Abdallah Ali Muhamed, alimpongeza mkuu huyo wa wilaya na kusema kuwa watahakikisha wanaendeleza  ushirikiano  kati yao kwa lengo la kuendeleza umoja utakaoleta maendeleo ndani  ya wilaya hiyo.
Hivyo viongozi hao waliahidi kutowa ushirikiano kati yao na mkuu huyo ili kuhakikisha wilaya hiyo inasonga mbele kimaendeleo.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.