Habari za Punde

Rais wa Zanzubar Dk. Shein Azungumza na Balozi wa Uturuki Ikulu Zanzibar.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akimsikiliza  Balozi wa Uturuki katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe.Ali Davutaglu  alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo wakati wa mazungumzo yao .[Picha na Ikulu.] 27/032018

RAIS  wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameihakikishia Uturuki kuwa Zanzibar itaendeleza uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya pande mbili hizo na kusisitiza ushirikiano katika sekta ya utalii kati ya Zanzibar na mji wa kitalii wa Antalya uliopo nchini humo.

Rais Dk. Shein aliyasema hayo leo wakati alipokuwa na mazungumzo na Balozi wa  Uturuki nchini Tanzania Ali Davutaglu  aliyefika Ikulu mjini Zanzibar kwa ajili ya kujitambulisha pamoja na kufanya mazungumzo na Rais wa Zanzibar.

Katika mazungumzo hayo, Rais Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa uchumi wa Zanzibar unategemea kwa kiasi kikubwa sekta ya utalii hivyo ni vyema mashirikiano yakaimarika zaidi kwa watalii wanaofika eneo la kitalii la Antalya nchini Uturuki wakafika na Zanzibar.

Alieleza kuwa mji wa kitalii wa Antalya nchini Uturuki lumebarikiwa kuwa na vivutio vingi sambamba na hali ya hewa nzuri ambapo sifa zote hizo zinafanana na Zanzibar, hivyo ni vyema ukawepo ushirikiano kati ya pande mbili hizo katika kuwaleta watalii wanaofika Antalya kuja kutembelea na Zanzibar.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza kuwa changamoto ya usafiri wa moja kwa moja kati ya Uturuki na Zanzibar iliyokuwepo hapo siku za nyuma hivi sasa haipo kutokana na kuwepo kwa usafiri wa ndege ya Kampuni ya “Turkish Airline” inayofanya safari zake kati ya Istanbul na Zanzibar.

Rais Dk. Shein pia, alitumia fursa hiyo kumueleza Balozi huyo wa Uturuki fursa iliyotolewa na Zanzibar kwa kuikaribisha nchi hiyo kuweka ubalozi wake mdogo hapa Zanzibar kama ilivyo kwa baadhi ya nchi kama vile, China, India, Msumbiji na Misri.

Dk. Shein alimueleza Balozi huyo kuwa iwapo hilo litafanikiwa litasaidia kwa kiasi kikubwa kuendeleza uhusiano na ushirikiano wa kihistoria uliopo katika kuendeleza sekta kadhaa ikiwemo biashara kati ya wananchi wa pande mbili hizo.

Katika maelezo yake, Rais Dk. Shein aliipongeza Uturuki kwa kuendeleza ushirikiano wake na Zanzibar huku akisisitiza haja ya kuendeleza ushirikiano katika sekta ya elimu,afya, uwekezaji na sekta nyenginezo ambapo katika sekta ya elimu alieleza haja ya kuwepo mashirikiano kati ya Chuo Kikuu cha Taifa cha Zanzibar (SUZA) na Chuo Kikuu cha Ankara nchini Uturuki.

Rais Dk. Shein alimueleza Balozi huyo wa Uturuki kuwa uhusiano na ushirikiano kati ya pande mbili hizo uliimarika zaidi pale Rais aliyemaliza muda wake Rais Abdullah Gul alipompa muwaliko kutembelea nchini humo na kufanya ziara mnamo mwaka 2011 hatua ambayo iliendeleza matembeleano kati ya viongozi wa Tanzania na Uturuki.

Sambamba na hayo, Dk. Shein aliipongeza Serikali ya Uturuki chini ya uongozi wa Rais Recep Tayyip Erdogan kwa kuendelea kuiunga mkono Zanzibar katika kuimarisha miradi yake ya maendeleo ikiwemo sekta ya elimu kwa kuendelea kutoa nafasi za masomo kwa wanafunzi wa Zanzibar.

Nae Balozi wa Uturuki nchini Tanzania Ali Davutaglu alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa Uturuki itaendeleza uhusiano na ushirikiano wake kati yake na Zanzibar na kuahidi kuendelea kuunga mkono juhudi zinazochukuliwa na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuimarisha sekta mbali mbali za maendeleo.

Katika mazungumzo hayo, Balozi Davutaglu alimueleza Dk. Shein kuwa Uturuki itaendelea kutoa ushirikiano wake kwa Zanzibar katika kuendeleza miradi ya maendeleo ikiwemo sekta ya elimu na kuahidi kuwa mashirikiano katika sekta ya utalii hasa kati ya mji wa kitalii wa Antalya na Zanzibar kuwa nchi yake italifanyia kazi.

Wakati huo huo, Rais Dk. Shein alifanya mazungumzo na ujumbe wa Kampuni ya Mawasiliano ya HUAWEI kutoka China chini ya uongozi wa Mwenyekiti wa Kampuni hiyo tawi la Tanzania  Gao Mengdong, Ikulu mjini Zanzibar.

Dk. Shein aliipongeza Kampuni ya HUAWEI kwa kuendeleza mawasiliano ya kisasa kwa kuanzisha simu zenye mfumo wa kisasa wa 5G pamoja na kueleza maendeleo ya miradi yao kwa Zanzibar pamoja na mchakato wa mradi wa umeme wa kutumia jua.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.