Habari za Punde

NFRA YASISITIZA HAITONUNUA MAHINDI YASIYOKUWA NA UBORA





Kaimu Ofisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), Vumilia  Zikankuba

Na Mathias Canal, NFRA-Dodoma
IKIWA msimu wa kununua mazao umeanza, Kaimu Ofisa Mtendaji Mkuu wa Wakala wa Taifa wa Hifadhi ya Chakula (NFRA), Vumilia  Zikankuba amewataka wakulima kuhakikisha wanazingatia ubora wa mahindi.

Aidha, amesema nchi inachakula cha kutosha na kusisitiza kuwa katika msimu wa kwanza wa ununuzi wa mahindi bei ya NFRA ni wastani wa Sh 380 hadi Sh 400 kwa kilo.

Akizungumza na waandishi wa habari ofisini kwake Mjini Dodoma, Zikankuba alisema NFRA haitaweza kununua mahindi mabovu na kusisitiza wakulima kuwa na mahindi yenye ubora ambayo yatawasaidia kupata masoko ya nje pia.

" Haiwezekani NFRA itumia fedha za Serikali kununua mahindi yasiyokidhi viwango vya ubora na machafu kutoka kwa wakulima. Hivyo wakulima wanapaswa kuzalisha mahindi kwa kuzingatia viwango vya ubora vinavyokidhi vigezo vya soko..

Aliongeza: “Lazima chakula tunachonunua kizingatie ubora. Tunataka tubadilishe taswira ya NFRA kwa sababu awali kulikuwa na tatizo la chakula kuharibika kwa kipindi kifupi.”

Zikankuba alisema ili kuhakikisha mahindi ya wakulima yanaweza kukidhi viwango vinavyotakiwa NFRA tayari imekwishatoa elimu kwa wakulima kupitia vikundi na kwenye vyombo vya habari.

Alibainisha kuwa baada ya elimu hiyo wakala umefanikiwa ambapo wakulima kutoka maeneo ya Makambako, Sumbawanga na Mpanda wameanza kuzalisha na kuuza mahindi yenye ubora kwa NFRA.

“Changamoto iliyopo ni kwa baadhi ya wakulima wachache ambao bado wamekuwa wagumu kubadilika na wale ambao wanaamini wakitumia nafasi zao wanaweza kuuza mahindi yasiyo na ubora,"

Alisema kwa mkulima kuwa na mahindi yenye ubora unatoakiwa utasaidia katika kupata soko la NFRA, pia katika taasisi zingine zinazonunua nafaka hiyo za ndani na nje ya nchi.

"Dhima ya serikali ni kwenda uchumi wa kati kupitia uchumi wa viwanda, kwa mahindi pekee hayatumiki kwa chakula pekee, bali kutengeneza bidhaa mbalimbali. Hivyo hatuwezi kufikia Tanzania ya viwanda endapo wakulima watazalisha malighafi zisizokuwa na ubora,” alieleza.

Viwango vinavyopaswa kuzingatiwa na wakulima wa mahindi ni kwamba unyevunyevu usizidi asilimia 13.5, takataka asilimia 0.5 na punje zilizovunjika zisizidi kwa asilimia 2.

Viwango vingine ni punje zilizoliwa na wadudu na zilizosinyaa zisizidi asilimia moja, punje mbovu asilimia mbili na punje za rangi tofauti zisizidi asilimia 0.5.

Zikankuba alitoa msisitizo kwa wakulima kutunza chakula badala ya kukiuza chote.

“Msimamo wa Rais (John Maguful) wa kutotoa chakula cha msaada upo sahihi kwa sababu kuna maeneo walikwishazoea kupelekewa chakula cha msaada. Msimamo huo umelenga kuwahamasisha wananchi kutunza chakula, haya malalamiko ya hatuna chakula yanachangiwa na uzembe wa wananchi wa kuuza chakula chote,” Vumilia, alibainisha.

Alisema jukumu la wakala ni kutunza chakula kwa ajili ya dharura kama kumetokea majanga kama mafuriko, njaa, tetemeko  na majanga mengine ambayo wanachi watahitaji msaada wa chakula.

Kuhusu bei ya mahindi ambayo NFRA imeanza kununua mahindi kwa wakulima Zikankuba alisema ni wastani wa Sh 380 kwa kilo hadi Sh 400 kwa kilo kulingana na eneo na eneo, na ni bei inayoendana na mwenendo wa bei ya soko.

 “ Mfano bei ya soko ya mahindi mkoani Ruvuma ni Sh 250 kwa kilo, lakini sisi kama NFRA tunanunua kwa bei ya juu ya kuanzia Sh 350 hadi 380 kwa kilo," alisema.

 Aliongeza: “Mkoani Dodoma NFRA inanunua Sh  420 kwa kilo, Makambako Sh 400, Shinyanga Sh 500, Katavi na Ruvuma Sh 350 hadi 380. Bei hiyo bado ni ya juu ukilinganisha na bei ya soko iliyopo,” alifafanua.

Aidha, Zikankuba alisema ziada ya mazao yote yaliyozalishwa na wakulima msimu huu imefikia tani milioni 2 huku ziada ya mahindi pekee ni tani 970,000.

Zikankuba alisema NFRA imetengewa Sh bilioni 15 kwa ajili ya kununua tani 28,000 kwa awamu ya kwanza ikiwa ni asilimia 2 ya ziada ya mahindi iliyopo.

Zikankuba alisisitiza kuwa NFRA inazingatia ubora wakati wa kununua kwa kuwa ni haki na muhitaji kupatiwa chakula bora na Salama kwa afya  wakati wa dharula hivyo mahindi ambayo hayana ubora yakituzwa kwa muda mrefu ghalani yanakuwa na nafasi kubwa kupata vimelea vya fangasi ambao husababisha uwepo wa sumu kuvu katika nafaka hiyo. 

Alisema kuwa Sumu kuvu ni hatari sana kwa afya ya mlaji. Tatizo hili kwa kiasi kikubwa sana, linaweza kuepukika kwa mkulima kufuata mbinu bora za kilimo, mbinu bora za utayarishaji nafaka na mbinu bora za kuhifadhi nafaka baada ya kuvuna. Lengo la NFRA ni kutoa chakula chenye ubora na salama wakati wa dharula.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.