Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira Mhe. Mussa Sima akitoa majibu ya Serikali wakati wa kipindi cha maswali na majibu hii leo Bungeni mjini Dodoma. Pamoja na mambo mengine Mhe. Sima amesisitiza juu ya uzingatiaji wa Sheria ya Mazingira kwa wenye viwanda na kwamba Serikali itaendelea kutoa elimu kwa wenye viwanda na kuwatoza faini wale wote wanaokiuka Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004.
Na. Lulu Mussa Dodoma.
Serikali imetoa wito
kwa wamiliki wa viwanda kuzingatia utekelezaji wa Sheria ya Mazingira na
Mikakati mbalimbali iliyopo kwa ajili ya kuwezesha usimamizi endelevu wa hifadhi
ya mazingira kwa faida yetu na ya vizazi vijavyo.
Hayo yamesemwa leo
bungeni Dodoma na Naibu Waziri Ofisi ya Makamu wa Rais Muungano na Mazingira
Mhe. Mussa Sima wakati wa kipindi cha maswali na majibu na kusisitiza kuwa Tanzania
inachangia kiasi kidogo sana katika tatizo la uzalishaji wa gesijoto ambazo ndio
chanzo cha mabadiliko ya tabia nchi.
Hata hivyo, pamoja na kuchangia kidogo kiasi hicho, Tanzania imeendelea kuathirika
kutokana na athari zitokanazo na mabadiliko ya tabianchi kama vile kupungua kwa
barafu ya mlima Kilimanjaro, kuongezeka kwa usawa wa bahari; ukame, mafuriko ya
mara kwa mara na mlipuko wa magonjwa.
Imebaini kuwa tatizo
la mabadiliko ya tabia nchi kwa kiwango kikubwa linasababishwa na uzalishaji wa
gesijoto unaotokana na matumizi ya nishati (47%), uzalishaji viwandani (30%) na
usafirishaji (11%) kwa shughuli za maendeleo katika nchi zilizoendelea
kiviwanda hususan za Ulaya, Amerika, Asia na Australia. Bara la Afrika kwa
ujumla limechangia gesijoto kiasi kisichozidi asilimia tatu (3). Tanzania huzalisha kiasi cha tani 0.09 za hewa ukaa (Per Capital emission) kwa mwaka.
Mheshimiwa Sima
amesema kuwa, tatizo kubwa linatokana na uchafuzi wa mazingira unaofanywa na baadhi
ya viwanda nchini ni kutiririsha maji taka yenye sumu na kemikali ambazo huathiri sana viumbe hai pamoja
na mazingira kwa ujumla.
“Tanzania inayo Sheria ya Usimamizi wa Mazingira
ya Mwaka 2004, Sheria hii imeweka misingi ya Usimamizi, Tathmini na Kuchukua tahadhari
kuhusu madhara kwa mazingira yakiwemo ya viwandani. Kwa kuzingatia Sheria hii,
Serikali imekuwa ikielimisha na kuwatoza faini wamiliki wa Viwanda wanaokiuka Sheria
hii na wanaoendelea kukaidi maelekezo na masharti waliyopewa hufungiwa kufanya
shughuli na kupewa masharti kabla ya kuruhusiwa kuendelea na shughuli zao tena.”
Alisisitiza Mhe. Sima.
Wakati huo huo Mhe.
Sima amewataka wamiliki wa viwanda kote nchini kuhakikisha Tathmini ya Athari kwa
Mazingira (Environmental Impact Assessment) na Ukaguzi wa Mazingira
(Environmental Audit) vinafanyika na kuzingatiwa. Aidha, wamiliki wa viwanda wanapaswa
kutumia nishati rafiki kwa mazingira na kutumia teknolojia banifu
katika uzalishaji wa bidhaa zao ili kusaidia kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.
No comments:
Post a Comment