TAARIFA
KWA VYOMBO VYA HABARI KUHUSU KILELE CHA MAADHIMISHO YA SIKU YA MAADILI NA HAKI
ZA BINAADAMU ZANZIBAR YATAKAYOFANYIKA TAREHE 10/12/2018.
Kila ifikapo tarehe 9 Disemba ya kila mwaka dunia
huadhimisha siku ya kupinga rushwa ambayo imeridhiwa na kupitishwa na Umoja wa
Mataifa kupitia mkataba wa Kupinga Rushwa ulioidhinishwa mwaka 2003. Vile vile,
katika jitihada za kuondoa aina zote za ubaguzi, kueneza uhuru na kupambana na vitendo
vya uvunjifu wa haki za binaadamu tarehe 10 Disemba, 1948 Baraza Kuu la Umoja
wa Mataifa lilipitisha Azimio la Kimataifa la Haki za Binaadamu na kuchaguliwa
rasmi kuwa kila ifikapo tarehe 10 Disemba ya kila mwaka ni siku ya Haki za
Binaadamu duniani.
Kwa kuwa kila ifikapo tarehe 9 Disemba ya kila mwaka
Jamuhuri ya Muungano waTanzania huadhimisha siku ya Uhuru wa Tanganyika. Kwa upande wa Tanzania Serikali ya
Jamuhuri ya Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imeamua kuwa tarehe
10 Disemba kila mwaka iwe ndio siku ya
kuadhimisha kilele cha siku ya Maadili na Haki za Binaadamu.
Taasisi zinazohusika moja kwa moja na usimamizi wa
jukumu la Maadili na Haki za Binaadamu ni tano (5) nazo ni : Tume ya Maadili ya
Viongozi wa Umma, Mamlaka ya Kuzuia Rushwa na Uhujumu Uchumi, Ofisi ya Mdhibiti
na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali, Idara ya Utawala Bora na Tume ya Haki za
Binadamu na Utawala Bora. Kupitia siku hii ya maadhimisho ya siku ya Maadili na
Haki za Binaadamu, taasisi hizi hufanya shughuli mbali mbali ikiwemo kuratibu
matukio yenye mnasaba na uimarishaji wa Maadili na Utawala Bora nchini.
Katika kuadhimisha siku hii adhimu, Taasisi
zinasimamia Maadili na Haki za Binaadamu zimefanya shughuli mbali mbali ikiwemo
utoaji elimu kama ifuatavyo:-
1. Kuandaa
na kurusha vipindi kupitia vyombo mbali mbali vya habari;
2. Kuandaa
mikutano na Sekta mbali mbali;
3. Kuandaa
mikutano katika shehia mbali mbali za Unguja na Pemba;
4. Kuandaa
mkutano na sasi za kiraia;
5. Kufanyika
kwa uzinduzi wa klabu za mapambano dhidi ya rushwa;
6. Kufanyika
kwa bonanza la mpira wa miguu; na
7. Kuandaa
makongamano mbali mbali.
Maadhimisho haya
ya siku ya Maadili na Haki za Binaadamu kila mwaka huja na ujumbe mahasusi ambapo
ujumbe wa mwaka huu unasema “tuimarishe
uadilifu, uwajibikaji, haki za binaadamu na mapambano dhidi ya rushwa kwa
maendeleo ya taifa”. Sherehe za mwaka huu zinatarajiwa kufanyika kesho
Jumaatatu tarehe 10 Disemba, 2018 katika uwanja wa Gombani Mpya Chake Chake
Pemba. Wageni mbali mbali wa kitaifa,
viongozi wa umma na wajumbe wa kimataifa wanatarajiwa kuwepo katika maadhimisho
hayo ambayo Mgeni Rasmin atakuwa Makamo wa Pili wa Rais, Mheshimiwa Balozi Seif
Ali Iddi.
Wananchi wote wa kisiwa cha Pemba wanaombwa
kushiriki katika maadhimisho hayo kwani mapambano dhidi ya rushwa, maadili ya
uongozi, haki za binaadamu ndio chachu ya maendeleo ya wananchi na nchi yetu.
Hivyo, bila ya kuwepo kwa nguvu za pamoja na mashirikiano baina ya mamlaka
husika na wananchi mapambano haya hayawezi kufanikiwa. Mambo mbali mbali yatakuwepo
katika kilele cha maadhimisho hayo yakiwemo utoaji wa taarifa za kimaendeleo
katika sekta husika, kupata msaada wa haki na elimu ya wajibu wa raia na elimu
ya utawala bora.
Ahsanteni nyote mnakaribishwa.
Imetolewa na
…………………………………..
Assaa A. Rashid
Mwenyekiti wa Kamati ya Maadhimisho ya
Siku ya Maadili na Haki za Binaadamu Zanzibar ambae pia ni Mwenyekiti wa Tume
ya Maadili ya Viongozi wa Umma Zanzibar.
No comments:
Post a Comment