Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Afya Zanzibar Ikulu Dogo Kibweni.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Afya Zanzibar katika Mkutano wa Utekelezaji wa Mpango Kazi (Bango Kitita) kwa mwezi wa Julia 2018 hadi Marchi 2019, uliofanyika katika ukumbi wa Ikulu Ndogo Kibweni Zanzibar .

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein amesisitiza kuwa chochote kinachoingia nchini kwa ajili ya matumizi ya binaadamu zikiwemo dawa na vyakula ni lazima zifuate sheria na taratibu zilizopo.

Hayo aliyasema leo, katika ukumbi wa Ikulu ndogo Kibweni mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Afya wakati ilipowasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango Kazi wa Wizara hiyo kwa Kipindi cha Julai 2018 hadi Machi 2019.

Dk. Shein alieleza kuwa ni kinyume na sheria na maadili ya dawa kuingiza, kuuza ama kuitangaza bila ya kufuata sheria na taratibu zilizopo na kueleza haja kwa Wizara ya Afya kulivalia njuga suala hilo kutokana na kujitokeza kwa wafanyabiashara wa dawa zikiwemo za kiswahili bila ya kufuata taratibu zilizopo.

Dk. Shein alieleza kuwa hafurahishwi na tabia ya baadhi ya wafanyabiashara wa dawa wakiwemo waganga wa jadi wanaojitangaza na kuwafahamisha watu ju ya ubora wa dawa zao na kueleza kuwa hiyo ni kwenda kinyume na utaratibu na sheria zilizopo.

Alisema kuwa hizo ni mbinu zinazotumika kuwahadaa wagonjwa na haikubaliki si kwa Zanzibar tu hata nchi nyingi duniani kufanya biashara ya dawa namna hiyo kwani kila kitu hasa dawa hufuata taratibu na sheria zilizowekwa kulingana na maadili ya huduma hiyo.

“Haya mambo lazima Wizara ya Afya tuyajuwe, tunapaswa kuwa na utaratibu, hivyo tuziweze vizuri Sheria zetu pamoja na Sera ya Afya kwani hali hii ikiendelea wafanyabaishara ya dawa hasa tiba asili watakuja kutuumizia watu wetu”,alisisitiza Dk. Shein.

Aidha, Rais Dk. Shein alitumia fursa hiyo kuupongeza uongozi wa Wizara ya Afya kwa kutekeleza vyema majukumu yao na kueleza kuwa Wizara hiyo imefanya kazi nzuri.

Aliongeza kuwa ni kawaida kazi ya mwanaadamu huwa haikosi kasoro lakini hata hivyo juhudi za makusudi zimeweza kuchukuliwa na uongozi pamoja na wafanyakazi wa Wizara hiyo katika kuhakikisha mafanikio makubwa yanapatikana.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliitaka Wizara hiyo kutoridhika na mafanikio na juhudi hizo zilizofikiwa na kutaka kasi zaidi iongezwe ili mafanikio zaidi yaweze kupatikana zikiwemo huduma bora za afya kwa wananchi wote.

Dk. Shein alitumia fursa hiyo kumpongeza Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd kwa kumsaidia vyema kazi za Serikali pamoja na kumpongeza Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee nae kuendelea kumsaidia.  

Katika kikao hicho, Makamo wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd nae alihudhuria na kutumia fursa hiyo kuupongeza uongozi wa Wizara hiyo kwa kuendelea kutekeleza vyema majukumu yake huku akimpongeza Rais Dk. Shein kwa mafanikio yaliopatikana chini ya uongozi wake.  

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliipongeza Wizara hiyo kwa kuwasilisha vyema Mpango Kazi wake  .

Nae Waziri wa Afya, Hamad Rashid Mohamed alieleza kuwa Wizara ya Afya imepiga hatua kubwa katika utoaji wa huduma kwa wananchi chini ya uongozi wa Rais Dk. Shein ambapo mafanikio kadhaa yamepatikana.

Alisema kuwa mafanikio kadhaa yamepatikana ikiwa ni pamoja na kuongezeka kwa wataalamu wa afya, ambapo jumla ya wafanyakazi 439 kutoka Unguja 242 na Pemba 197 wa kada mbali mbali wakiwemo madaktari 7 tayari wameajiriwa.

Aliongeza kuwa kuimarika kwa huduma za uchunguzi wa maradhi na huduma za matibabu nako kumeongezeka sambamba na kupatikana kwa lift mpya katika Hospitali ya Mnazi Mmoja ambapo kunaifanya hospitali hiyo kuwa na lift mbili ambazo zote zinafanya kazi sambamba na upatikanaji wa dawa muhimu katika vituo vya afya kwa kuimarika na kufikia zaidi ya asilimia 90 kutoka asilimia 50.

Akiyataja mafanikio mengine ni pamoja na kukamilika kwa ujenzi wa chumba cha upasuaji katika hospitali ya Micheweni na kupandishwa daraja Hospitali za vijiji ya Kivunge na Makunduchi kuwa Hospitali za Wilaya ambapo kupandishwa hadhi hospitali hizo ni sehemu ya utekelezaji wa Ilani ya CCM.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar

Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.