Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Aongoza Wananchi Katika Maziko ya Aliyekuwa Waziri wa SMZ Marehe Ali Juma Shamuhuna Kijiji Kwao Donge Imiyani Mkoa wa Kaskazini Unguja leo

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe. Dk. Ali Mohamed Shein, akiwa katika Sala ya kuuombea Mwili wa Marehemu Ali Juma Shamuhuna Sala iliofanyika katika msikiti wa Kijiji Kwao Donge leo kulia Mtoto wa Marehemu Shamuhuna na Makamu wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Iddi wakishiriki katika Sala hiyo.


RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Alhaj Dk. Ali Mohamed Shein ameongoza mamia ya wananchi katika mazishi ya Marehemu Ali Juma Shamuhuna yaliyofanyika kijijini kwao Donge Eneani, Mkoa wa Kaskazini Unguja.

Rais Dk. Shein aliungana na viongozi mbali mbali wa Serikali, dini na vyama vya siasa pamoja na ndugu, jamaa, marafiki na wananchi kadhaa akiwemo Makamo wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zubeir Ali Maulid na viongozi wengineo.

Mapema Rais Dk. Shein aliungana na wananchi katika sala ya kumuombea dua Marehemu hapo hapo kijini kwao Donge Eneani ambapo baada ya sala hiyo taratibu za mazishi zilifanyika.

Akisoma Wasfu wa Marehemu Ali Juma Shamuhuna, Waziri wa Nchi Ofisi ya Makamo wa Pili wa Rais Mohamed Aboud alisema kuwa Marehemu Shamuhuna ambaye alikuwa Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali Mstaafu alizaliwa katika kijiji cha  Donge mnamo tarehe 01 Januari mwaka 1944.

Katika uhai wake Marehemu Shamuhuna alipata elimu ya Msingi katika skuli ya Kiembe Samaki na Skuli ya Msingi ya Makunduchi mwaka 1952 hadi 1959 ambapo pia, alisoma skuli ya Sekondari ya Lumumba Kidato cha Kwanza hadi cha Nne mnamo mwaka 1959 hadi 1963.

Kwa upande wa Elimu ya Juu, Marehemu Shamuhuna alisoma Diploma ya Juu ya “Diary Technology”, “B.SC Animal Production” mwaka 1977 hadi 1980, “M.B.SC Animal Genetics and Breeding” mwaka 1981 hadi 1982 pamoja na “B.A Economic Inter Trade” mwaka 1992 hadi mwaka 1996.


Marehemu Shamuhuna kwa upande wa ajira aliwahi kuwa Meneja Mkuu katika Shamba la Mifugo Kizimbani mnamo mwaka 1966 hadi 1969, alikuwa Meneja Mkuu wa Shamba la Wanyama Kizimbani, Tunguu, Pangeni na Hanyegwa Mchana mnamo mwaka 1969 hadi 1976.

Pia, Marhemu Shamuhuna aliwahi kuwa Meneja Mkuu wa Ushirika wa Uzalishaji wa Wanyama mnamo mwaka 1981 hadi 1985, Mkuu wa Mradi wa “World Food Programme” ulioendeshwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la (UNDP) mwaka 1985 hadi 1988 na hatimae kufikia Katibu Mkuu Wizara ya Kilimo mwaka 1988 hadi 1990.

Kwa upande wa nafasi za Kisiasa, Marehemu Shamuhuna alikuwa Mwanachama mwaminifu wa Chama Cha Mapinduzi (CCM), na alikamata nyadhifa mbalimbali ikiwemo Mhasibu katika Tawi la Kwahani mwaka 1981 hadi 1985, Mjumbe wa Kamati ya Siasa ya Mkoa mwaka 1985 hadi 2012.

Pia, Marehemu Shamuhuna aliwahi kuwa Mjumbe wa Kuteuliwa kwa uteuzi wa Rais katika Baraza la Wawakilishi (BLW) mwaka 1995 hadi 2000 ambapo pia, aliwahi kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kupitia (BLW) mnamo mwaka 1995 hadi 2000.

Aidha, Marehemu Shamuhuna aliwahi kuwa Kamishna wa Tume ya Muwafaka 2001 hadi mwaka 2002 ambapo pia, aliwa hukuwa Mwakilishi wa Jimbo la Donge mwaka 2000 hadi 2015 baada ya hapo alistaafu shughuli za kisiasa.

Sambamba na hayo, Marehemu Shamuhuna amewahi kushika nyadhifa mbalimbali za Uwaziri katika Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ikiwa ni pamoja na kuwa Naibu Waziri Kiongozi na Waziri wa Habari, Utamaduni na Michezo, Waziri wa Elimu na Mafunzo ya Amali, Waziri wa Ardhi, Waziri wa Nchi Ofisiya Rais Mipango.

Marehemu  Shamuhuna amefariki dunia jana jioni (19.05.2019), huko Fuoni Wilaya ya Magharibi B, Mkoa wa Mjini Magharibi Unguja, ambako alikuwa akiugua.

Marehemu amewacha watoto tisa na kizuka mmoja, Mwenyezi Mungu ailaze mahala pema peponi, roho ya Marehemu Ali Juma Shamuhuna, Amin.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.