Na. Paschal Dotto-Maelezo.
Serikali Kupitia Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano,
imesema kuwa itaendelea kuwajengea uwezo na uzoefu mafundi sanifu na mafundi
Michundo, ili waendelee kutekeleza kazi zao kwa ufanisi na kuongeza wataalam
katika kada hiyo kwani fani hizo zina watu wachache.
Akizungumza Jijini Dar es Salaam katika Mkutano wa
Wasanifu Majengo na mafundi Michundo, Katibu Mkuu Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na
Mawasiliano,Dkt. Elius Mwakalinga alisema kuwa Serikali kupitia Wizara ya
Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano imejikita katika kuhakikisha kuwa ujenzi wa
miundombinu unafanikiwa kwa kiasi kikubwa.
“Serikali imedhamiria kujenga miundombinu ili
kuwezesha ukuaji wa Sekta ya Viwanda nchini, hivyo Mafundi sanifu wanategemewa
sana katika kuwezesha miundombinu hii, ili Tanzania iweze kufikia ndoto ya kuwa
kwenye uchumi wa kati kupitia viwanda, na katika kutekeleza hilo mwaka wa Fedha
2019/2020, Wizara ya Ujenzi imejikita katika ajenda tatu ikiwemo kuwajengea
uwezo wasanifu na wahandisi wote nchini”, Alisema Dkt. Mwakalinga.
Dkt. Mwakalinga alisema kuwa Serikali inahakikisha
watalaam chini ya Taaluma ya Uhandisi, Usanifu Majengo, Ukadiriaji Majenzi na
kada zingine katika sekta ya ujenzi wanaongezeka kiidadi na kujengewa ujuzi
mahsusi ili kuwa na uwezo na kumudu mahitaji ya nchi ya wataalam hao.
Aidha, Dkt. Mwakalinga aliwathibitishia kuwa serikali
inaendelea kushirikiana na bodi mbalimbali za taaluma za kihandisi kwa kutoa
miradi inayotekelezwa nchini ili kuwawezesha watalaam hao kupata uzoefu na
kufanya kazi kwa ufanisi mkubwa na kazi hiyo itaanza rasmi mwaka wa fedha
2019/2020, Julai Mosi.
“Napenda niwadhihirishie kuwa, Serikali ya Awamu ya
Tano, chini ya uongozi wa Rais Magufuli, inayo dhamira ya dhati ya kuendeleza
fani ya usanifu kwa kutumia miradi yake inayotekelezwa, kama vile ujenzi wa
Reli ya kisasa, SGR, Ujenzi wa Interchange Ubungo, Ujenzi wa Bwawa kubwa la
kuzalisha umeme mto Rufiji, na ujenzi wa Daraja la Selander, kwa hiyo miradi
hii itaweza kutoa uzoefu mkubwa kwa wataalum wetu”, alisema Dkt. Mwakalinga.
Katika kuongeza uzoefu wa watalaam hao, Dkt Mwakalinga
amesema ni lazima kuwepo na maarifa na vitendea kazi ambavyo kwa sasa ni uwepo
wa miradi ya kimaendeleo ambayo inatekelezwa na Serikali na sasa mafundi sanifu
wanahitajika ili kuiwezesha miradi hii kutekelezwa pasipo gharama kubwa.
Akaongeza kuwa Serikali inapoendelea na zoezi la
kuwapa uwezo watalaam hao inawaomba wawe waadilifu, wenye kujituma na wenye
weledi mkubwa maana kazi yao hiyo ni kubwa sana kuliko kazi zingine za
kihandisi.
“Kama nilivyosema hapo awali tutaendelea kuwajengea
uwezo watalaam wetu kwa kutumia miradi tuliyonayo, lakini kujenga uwezo kuna
uhusiano mkubwa na masuala ya kujituma, kuijitoa kwa moyo kwa taifa, kufanya
kazi kwa bidii na weledi mkubwa, hii ndiyo itakuwa tiketi ya kupata kazi na
tutachagua watalaam kulingana na vigezo hivyo,”Alisisitiza Mwakalinga.
Akizungumzia kuhusu changamoto za uhaba wa wataalam
hao, Dkt. Mwaklinga aliainisha kuwa, kwa takwimu za Shirika la kazi duniani,
ILO, zinabaini kuwa Mhandisi mmoja anapaswa kufanya kazi na Mafundi Sanifu
watano, na Mafundi Stadi 25, na kuongeza kuwa hiyo inaonyesha umuhimu wa
wasanifu na mafundi stadi katika sekta ya ujenzi.
Kwa Upande wake Mwenyekiti wa Bodi ya Usajili
Wahandisi (ERB), Prof. Ninatubu Lema, alisema kuwa Wasanafi wanahitajika
kijituma ili kuanzisha viwanda vidogovidogo vya kutengeneza vitu mbalimbali
ambavyo vinaweza kuuzwa nchini.
“Mnatakiwa Mafundi Sanifu kuwa wabunifu katika kujenga
na kutengeneza uwezo kwa kufanya
wajasiriamali wa kujenga viwanda vidogovidogo, ili mtu mmoja aajiri watu
watano, watu sita au watu 10 na kutengeneza vitu vidogovidogo vya kuuzwa hapa
nchini, … tuko tayari kuratibu na kwenda kwenye nchi za wenzetu kama India,
China kutazama hivyo viwanda vidogovidogo.”, Alisema, Prof.Lema.
No comments:
Post a Comment