Habari za Punde

Benki ya Maendeleo ya Afrika Kuipandisha Daraja Tanzania.



Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB), Alex Mubiru akielezea jambo wakati wa mazungumzo yake na Waziri wa Fedha na Mipango, Mhe. Dkt. Phillip Mpango (Mb), Jijini Dodoma.

Na. Saidina Msangi na Josephine Majura, WFM, Dodoma
Benki ya Maendeleo ya Afrika (AfDB) inatarajia kuipandisha daraja Tanzania kutoka katika hadhi ya kunufaika na Mfuko wa Maendeleo wa Benki (ADF)hadi kuwa na hadhi itakayoiwezesha Tanzania kuweza kupata rasilimali fedha zaidi kupitia dirisha la African Development Bank (ADB) la Benki ya Maendeleo ya Afrika.

Endapo Tanzania itafanikiwa kupandishwa hadhi, nchi itaweza kunufaika na ongezeko la fedha kutoka Benki ya Maendeleo ya Afrika kutoka Dola za Marekani milioni 350 kwa mwaka hadi Dola za Marekani milioni 812 kwa mwaka. 

Hayo yamesemwa Jijini Dodoma na Mwakilishi Mkazi wa Benki hiyo Dr. Alex Mubiru alipokutana na kufanya mazungumzo na Waziri wa Fedha na Mipango, Dkt. Philip Isdor Mpango, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha na Mipango-Treasury Square. 

Katika mazungumzo hayo, Dr. Alex ameeleza kuwa hatua hiyo ya kupandishwa hadhi ama kupandishwa daraja inatokana na uchumi wa nchi kufanya vizuri hususani katika maeneo ya kasi ya ukuaji wa uchumi na kuwa na deni himilivu.

“Hatua hiyo itaiwezesha Tanzania kupata fedha zaidi kutoka katika Benki hiyo na kuwezesha utekelezaji wa miradi ya maendeleo na vipaumble kwa Serikali” Alisisitiza Bw. Mubiru. 

Mwakilishi Mkazi wa Benki ya Maendeleo Afrika (AfDB), Bw. Alex Mubiru, amesema kuwa benki hiyo inajivunia kufanya kazi na Tanzania ambayo ni miongoni mwa nchi Waasisi wa Benki hiyo.

Katika mazungumzo yao, Dkt. Mpango ameeleza kuwa Serikali inajivunia kufanya kazi pamoja na Benki ya AfDB kwa kuwa benki hiyo imekuwa na masharti rafiki katika upatikanaji wa mikopo.

Dkt. Mpango amesema kuwa Benki hiyo ina mtazamo chanya katika maendeleo ya watu na kuwa dira katika mipango ya maendeleo na kuahidi kushirikiana nao vyema katika kukuza uchumi wa nchi.

Aidha, Waziri Mpango ameipongeza benki hiyo kwa kukubali kutekeleza miradi ya Ujenzi wa Barabara ya Mzunguko Dodoma (km110.2) kwa kiwango cha lami pamoja na ujenzi wa Uwanja wa Ndege wa Dodoma (Msalato) na kubainisha kuwa uamuzi huo ni mzuri kwani licha ya Dodoma kuwa ni Makao Makuu ya nchi lakini pia miundombinu hii itaunganisha na kuchochea ukuaji wa uchumi na biashara katika mikoa mingi nchini pamoja na nchi jirani.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.