Habari za Punde

Kuwasaidia Vijana na Kuwatunza Kwani Wana Umuhimu Mkubwa Katika Jamii.


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Vijana Utamaduni Sanaa na Michezo Zanzibar, wakati wa mkutano wa Utekelezaji wa Bajeti na Mpango Kazi wa Wizara hiyo kwa mwezi wa Julai hadi Juni 2019, uliofanyika katika ukumbi wa Ikulu Zanzibar.23-8-2019.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ameupongeza uongozi wa Wizara ya Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo kwa kuwapa mwanga wa kimaisha vijana na kusisitiza haja ya kuwaenzi na kuwaendeleza.

Hayo aliyasema leo, Ikulu mjini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo wakati ilipowasilisha Mpango Kazi wa Julai  2018 hadi Juni 2019 sambamba na Mpango Kazi wa Utekelezaji kwa mwaka 2019/2020.

Alieleza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar imefanya kazi kubwa katika kuhakikisha vijana ambao ndio kundi kubwa inawawekea mazingira mazuri ya kujiajiri sambamba na kuwapa mafunzo ya ujasiriamali.

Hivyo, Rais Dk. Shein alisisitiza haja kwa Wizara hiyo kuendelea kuwasaidia vijana na kuwatunza kwani wana umuhimu mkubwa katika jamii na ndio maana Serikali anayoiongoza inaendelea kuwawekea mikakati maalum ya kuwaendeleza kimaisha.

Rais Dk. Shein alitoa pongezi kwa Wizara hiyo kwa kuwasilisha vyema Mpango Kazi wao na kueleza kuwa vikao na utaratibu huo umekuwa ukitatua mambo mbali mbali ambayo hatiamae kuleta tija.

Dk. Shein alieleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar ya kujenga uwanja mpya kwa ajili ya shughuli maalum za Serikali zikiwemo sherehe za Mapinduzi.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza haja kwa Wizara hiyo kuwa karibu sana na wasanii wa hapa nchini kwani wengi wao wanavipaji vizuri na iwapo watawekewa mikakati maalumu ya kuwaimarisha watazidi kufanya vizuri kitaifa na kimataifa.

Rais Dk. Shein alieleza kuwa tayari Kiswahili kimeingizwa katika Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) hivyo, kuna haja ya kukiendeleza na kukiimarisha hasa kwa Zanzibar kwani ndio chimbuko la lugha hiyo na kusisitiza haja ya kukaa pamoja kati la Baraza la Kiswahili la Zanzibar na uongozi wa vyombo vya habari vikiwemo vya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliipongeza kazi nzuri ya uwasilishaji iliyofanywa na Wizara hiyo huku akisisitiza haja kwa uongozi na wafanyakazi kuendeleza mashirikiano.

Mapema Waziri wa  Vijana, Utamaduni, Sanaa na Michezo Balozi Ali Karume akiwasilisha muhtasari wa utekelezaji mpango Kazi wa Wizara hiyo alipongeza jitihada zilizochukuliwa za kuendeleza lugha ya Kiswahili ambapo kwa sasa imetangazwa kuwa lugha ya nne rasmi itakayotumika katika mikutano ya (SADC).

Balozi Karume alieleza kuwa Wizara hiyo kupitia Baraza la Kiswahili Zanzibar inachukua juhudi zikiwemo uanzishaji wa Kazi Data ya wataalamu wa Kiswahili Zanzibar,Uchapishaji wa Makala za Kiswahili, vitabu vya taaluma ya Kiswahili, lahaja pamoja na kuandaa makongamano ya Kiswahili.

Waziri huyo alieleza mafanikio ya wizara hiyo ikiwa pamoja na kuyaunganisha Mabaraza ya Vijana kwenye fursa za uchumi, kuongezeka idadi ya wanachama wa Baraza la Vijana na kufikia 3,276 pamoja na kuwapatia vijana mafunzo ya kilimo, ufugaji, elimu ya ujasiriamali na uzalendo kupenda nchi yao.

Aidha, alieleza kuwa Wizara imefanikiwa kuvipatia vifaa vya muziki kikundi cha taarabu cha Taifa ambapo hapo awali vifaa vingi vilivyokuwa vikitumiwa na kikundi hicho vilikuwa ni vya kukodi na kuazimwa kutoka vilabu mbali mbali vya taarabu.

Katika kuhakikisha utamaduni, mila, silka za wazanzibari zinaenziwa, zinaendelezwa kwa manufaa ya Taifa, Wizara kwa kushirikiana na kikundi cha Taifa cha Maigizo na  Kikundi cha Culture imeandaa maigizo maalumu yatakayoelezea utamaduni halisi wa Mzanzibari.

Aliongeza kuwa jumla ya kazi za Sanaa 31 zikiwemo nyimbo, maigizo, tenzi, mashairi,kasida pamoja na vipindi vya kuelimisha jamii zikiwemo matangazo na hadithi fupi vimerekodiwa kupitia studio ya Filamu na Muziki Rahaleo.

Pia, alieleza kuwa Wizara imefanikiwa kukamilisha Sera ya Michezo na kuvisaidia vyama vya michezo kuandaa na kushiriki katika mashindano mbalimbali ya kitaifa na kimataifa pamoja na kuandaa tamasha la mazoezi ya viungo kitaifa.

Uongozi huo pia ulieleza mafanikio ya kukamilisha matengenezo makubwa ya kiwanja cha MaoZedong na matengenezo madogo kwa kiwanja cha Gombani na Amaan Stadium ambapo kwa upande wa viwanja vya Wilaya ya Kusini Pemba vya “Kangani” na Kaskazini “Kishindeni” vimo katika hatua za uwekaji lami katika sehemu ya kukimbilia.

Aidha, uongozi huo ulieleza jitihada wanazoendelea kuzichukua katika kudhibiti filamu zisizo na maadili huku wakieleza juhudi wanazozichukua katika kuhakikisha Kiswahili kinatumikakwa fasaha na usahihi katika vyombo vya habari pamoja na jamii nzima kwa jumla.

Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.