Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, Azungumza na Viongozi wa Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wenye Viwanda wa Ras Al Khaimah.J sZ

 
Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk.Ali Mohamed Shein kulia Mhe.Mohammed Ali Musabah,Mwenyekiti wa Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wenyeviwanda wa Ras Al Khaimah na Waziri wa Ardhi Maji Nyumba na Nishati Zanzibar Mhe.Salama Aboud Talib, wakimasiliza Meneja wa Mamlaka ya Maendeleo ya Utalii wa Serikali ya Ras Al Khaimah Bi.Navritu Rai na Viongozi  wa Kampuni za Uwekezaji, Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wenye Viwanda pamoja na Mamlaka za Vitega Uchumi wa Ras Al Khaimah, hafla hiyo imefanyika katika Ukumbi wa Hotel ya Waldorf Astoria Ras Al Khaimah)

VIONGOZI wa Kampuni za Uwekezaji, Jumuiya ya Wafanyabiashara na Wenye Viwanda pamoja na Mamlaka za Vitega Uchumi za Ras Al Khaimah wameeleza azma yao ya kushirikiana na kuiunga Zanzibar ili izidi kupiga hatua katika kujiletea maendeleo endelevu.

Maelezo hayo waliyatoa wakati walipofanya uwasilishaji wa shughuli zao za kimaendeleo za nchi hiyo kwa Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein pamoja na Ujumbe wake huko katika ukumbi wa Hoteli ya Waldorf Astoria, mjini Ras Al Khaimah.

Miongoni mwa viongozi hao ni pamoja na viongozi wa Jumuiya Wafanyabiashara na wenye Viwanda wa Ras Al Khaimah  ambapo Msaidizi Mkurugenzi Mkuu wa Jumuiya hiyo Bi Eiman Darwish Alhayyas alieleza ukubwa wa Jumuiya hiyo yenye wanachama wapatao 139 pamoja na kazi inazozifanya.

Bi Eiman Darwish aliongoza kuwa Jumuiya yao hiyo ina uzoefu wa  miaka 52 katika kuwasaidia wafanyabiashara pamoja na Mashirika na Makampuni ya biashara ambayo tayari yameweza kupata mafanikio makubwa na kuweza kuimarisha na kukuza uchumi wa nchini hiyo.

Alisema kuwa shughuli za Jumuiya yao zimeipelekea Ras Al Khaimah kuwa ni nchi inayoongoza kwenye uzalishaji wa viwanda katika nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), hivyo walieleza haja kwa Zanzibar kupata kuitumia fursa hiyo.

Uongozi huo waliikaribisha Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kushirikiana katika maeneo mbali mbali yakiwemo maeneo mengine mapya ya biashara yanayohusiana na usalama wa chakula, viwanda, utalii pamoja na kilimo.

Ahmed Numan ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa Masoko na Mawasiliano katika Mamlaka ya Vitega Uchumi ya Ras Al Khaimah ( RAKEZ) ambapo katika maelezo yake alieleza kuwa Ras Al Khaimah ni nchi inayotambulika ulimwenguni katika masuala ya uwekezaji.

Alieleza kuwa katika nchi za Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE), Mamlaka hiyo ya (RAKEZ) ni moja kati ya Mamlaka ya Vitega Uchumi inayokuwa kwa haraka sana na matunda yake yanaonekana ambapo tayari inamiliki Kampuni 40500 za uwekezaji.

Aidha, Mkurugenzi huyo alieleza kuwa (RAKEZ) inachangia asilimia 25 za Pato la Taifa la nchi hiyo ambazo zinatokana na uzalishaji wa viwanda.

Akiwasilisha mada yake juu ya Mamlaka ya Maendeleo ya Utalii ya Ras Al Khaimah Bi Navritu Rai yeye kwa upande wake alieleza maendeleo ya Utalii ya Ras Al Khaimah sambamba na hatua zinazochukuliwa ili kuuendeleza zaidi utalii.

Alieleza kuwa idadi ya watu wa nchi hiyo ni 345000 ambapo wanajivunia rasilimali walizonazo ambazo ndizo zinazoendeshea utalii ambazo ni milima, fukwe, jangwa, chemchem za asili na mikoko ambavyo hivyo ndivyo vivutio vyao vikubwa vya utalii.

Alieleza kuwa lengo lao ifikapo mwaka 2025 waweze kuingiza  watalii milioni 2.9 ambapo kwa hivi sasa tayari wanapokea watalii milioni 1.2 wakiwa na lengo la kufikisha watalii 1.5 mwishoni mwa mwaka 2021.

Alisema kuwa njia kubwa wanazozitumia katika kukuza utalii wao ni kubuni vivutio vipya kwa mfano shamba la lulu ambalo wafanyaji shughuli za kutafuta lulu huzisarifu katika mapambo ya vitu mbali mbali ambavyo ni vivutio vikuu vya watalii sambamba na upandaji wa mikoko ambayo ndege hufanya makaazi yao ambayo pia, ni vivutio vya watalii.

Aliongeza kuwa Ras Al Khaimah ina bustani ya miti ya asili ambayo imekuwa ni kivutio kimoja wapo kikubwa cha watalii.

Pia, kuwepo kwa michezo mbali mbali nayo imekuwa kivutio cha watalii hasa michezo ya kuruka majabalini huku akieleza azma ya miradi mingine wanayokusudia kuanzishwa ni kuanzisha utalii kwa michezo ya watoto.

Aidha, walieleza azma yao ya kuanzisha Chuo maalum kwa ajili ya kuwafundisha watu njia tofauti za kujiokoa na majanga mbali mbali.

Pamoja na hayo, viongozi hao walieleza kuwa mbali ya kuanzisha vivutio mbali mbali vinavyotokana na rasilimali walizonazo za utalii pia, wanachukua juhudi za makusudi katika kuutangaza utalii wao kwa kufanya maonyesho pamoja na wao kushiriki katika maonyesho katika nchi mbali mbali ulimwenguni.

Pia, walieleza namna wanavyoendeleza miji mipya ya kisasa inayotokana na  kufukia bahari kikiwemo kisiwa cha kitalii cha Marjan ambacho ni nembo muhimu katika maendeleo ya Ras Al Khaimah ambacho kinapokea watalii 17200 kwa mwaka na bado wapo wageni ambao hukosa nafasi kwa uhaba wa nafsi za makaazi.

Mkuu wa Utawala wa Kisiwa cha Marijani Abdulla Al Abdool alieleza kuwa maendeleo katika kisiwa hicho yataendelea kukua kwani tayari kuna wawekezaji kadhaa wa ndani na nje ya Ras Al Khaimah ambao wameonesha nia ya kutaka kuekeza miradi mbali mbali.

Kwa upande wa Mamlaka ya Bandari ya Ras Al Khaimah ni Shirika ambalo lina uzoefu mkubwa wa uendeshaji wa hsughuli za baharini ikiwemo bandari ambapo huduma zao za mambo ya bahari ni ya daraja la kwanza.

Bandari za Ras Al Khaimah zimekuwa kiunganishi muhimu kwa nchi za Unoja wa Falme za Kiarabu (UAE) ambapo pia, ni miongoi mwa vituo vinavyosambaza saruji na vifaa vyengine ujenzi katika nchi za Ghuba ambayo ina Vyelezo 14 vya kufanyia matengenezo ya meli zinazoharibika.

Mkuu wa Mamlaka hiyo Adrian Pearson alieleza kuwa shughuli zote za bandari katika nchi hiyo zinaendeshwa na wawekezaji wa kigeni kwa asilimia mia moja.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein nae kwa upande wake alitumia fursa hiyo kutoa pongezi kwa uongozi wa Kampuni, Jumuiya ya Wafanyabiashara  na Mamlaka za Ras Al Khaimah na kuisifu azma ya kuwepo kwa mashirikiano kati ya pande mbili hizo.

Nao viongozi wa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar walieleza kufarajika kwao na maelezo ya uwasilishaji wa shughuli za maendeleo yaliofikiwa na Ras Al Khaimah na kuuliza masuala kwa ajili ya kupata ufafanuzi zaidi juu ya mambo mbali mbali kwa lengo la lujifufunza sambamba na kwenda kuyafanyia kazi zaidi nyumbani  hatua kwa hatua.

Viongozi hao walipongeza mafanikio yaliofikiwa na Ras Khaimah pamoja na mbinu wanazotumia katika kuendeleza siri ya mafanikio yao kwenye maendeleo wanayoyapata hasa katika sekta ya uwekezaji na utalii ambazo zimekuwa zikiimarika kila uchao.

Sambamba na hayo, viongozi hao walieleza kuwa miongoni mwa maendeleo yaliyokwisha fikiwa na Ras Al Khaimah tayari Serikali ya Mapinduzi Zanzibar kwa upande wake imeshaanza kuchukua hatua za utekelezaji wa mipango yake mbali mbali pamoja na mikakati maalum kwa kushirikiana na wawekezaji wa ndani na nje ya nchi ili kuyafikia maendeleo kama hayo.
 Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.