MAKAMU Mwenyekiti
wa CCM Zanzibar Dk. Ali Mohamed Shein ameeleza azma ya Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar kununua boti mpya ili kuwasaidia wananchi wakiwemo wazee wanaoishi katika
visiwa vidogo vidogo vya Unguja na Pemba waweze kuvuka kwa uhakika.
Dk. Shein aliyasema hayo wakati alipokutana na wazee wa Chama
Cha Mapinduzi (CCM) wa Wilaya ya Mkoani huko katika ukumbi wa Skuli ya Mohamed
Juma Pindua, iliyopo Wilaya ya Mkoani, Mkoa wa Kusini Pemba.
Rais Dk. Shein alisema kuwa Serikali ya Mapinduzi ya
Zanzibar tayari imeshaanza mchakato huo ambao utakapokamilika utawasaidiaa kwa
kiasikikubwa wananchi wanaoishi visiwani.
Makamo Mwenyekiti huyo wa CCM Zanzibar alivitaja visiwa sita
ambavyo vimelengwa kupata boti hizo mpya na za kisasa ili ziwe msaada mkubwa
kwao katika kuwasaida kuwavusha kikiwemo Kisiwa Panza, Makongwe, Fundo, Uvinje,
Kokota na Tumbatu.
Aidha, Rais Dk. Shein amesisitiza haja ya kufanya kazi pamoja
na wazee kwani ni watu muhimu sana katika jamii ambao bado mchango wao
unahitajikakatika maendeleo ya kisiasa, kiuchumi na kijamii.
Alisisitiza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar inathamini
na inazijali juhudi za wazee walizozichukua hadi kupelekea kupatikana uhuru wa
Tanganyika na uhuru wa Zanzibar kupitia vyama vya ASP na TANU.
Katika hotuba yake aliyoitoa mbele ya wazee hao wa CCM
pamoja na viongozi wengine wakuu wa chama hicho Rais Dk. Shein alisema kuwa wazee
walichukua juhudi za kujitolea na ndio maana uhuru kwa Tanzania Bara na Zanzibar
ukapatikana hivyo, falsafa hiyo ni lazima ikaendelezwa kwani ina tija katika
kujiletea maendeleo.
Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein alisema kuwa CCM ndio
chama kinachowatetea wanyonge hivyo, ni lazima kitegemee nguvu za wanachama
wake katika kufikia malengo yao waliyoyakusudia ikiwa ni pamoja na kuendelea
kuongoza Dola.
Nae Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Abdalla Juma Mabodi
alisema kuwa Chama Cha Mapinduzi (CCM) bado kinaendelea kuwatunza, kuwaenzi na
kuwathamani wazee na ndio maana wameingizwa katika taratibu zote za chama
hicho.
Aliongoza kuwa hikma za kuwaenzi wazee zimeanza kabda ya
Mapinduzi chini ya Jemedaru Hayati Mzee Abeid Amani Karume na hadi hivi leo
hikma na busara hizo zinaendelea kutumika ikiwa ni pamoja na kuwatuza wazee
wote wa Unguja na Pemba tena bila ya ubaguzi.
Nao Wazee katika taarifa yao walimpongeza Rais Dk. Shein na
kueleza kuwa kitendo cha kwenda kukutana nao ni kielelezo kuwa anawajali na
kuthamini juhudi zao ama mchango wao ndani ya Chama Cha Mapinduzi (CCM).
Aidha, wazee hao wa Mkoani walimpongeza Rais Dk. Shein kwa
jinsi alivyoweza kudumisha amani na utulivu nchini jambo ambalo limemfanya
aweze kutekeleza kwa ufanisi mkubwa maendeleo endelevu nchini.
Wakijataja baadhi ya maendeleo hayo ni pamoja na ujenzi wa
barabara zenye viwango, upandishaji wa bei za karafuu, fedha za kila mwezi kwa
wazee wa umri wa miaka 70 ambao miongoni mwao wanafaidika, ongezeko la fedha
kwa wastaafu na uwekaji wa umeme na maji salama katika visiwa vya Unguja na
Pemba na mengineyo.
Wazee hao pia, walitumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dk.
Shein kwa kuendelea kuyaenzi Mapinduzi matukufu ya Zanzibar kwa vitendo kwa
kuendeleza kwa kasi matunda yake kama vile kuendeleza huduma za afya na elimu
bure kwa wananachi.
Sambamba na hayo, nao wazee wa Makongwe walitoa pongezi zao
za pekee kwa Rais Dk. Shein kwa kuwapelekea umeme katika kisiwa hicho ambapo
hivi sasa wananchi wa kisiwa hicho wamekuwa wakifaidika na huduma hiyo muhimu
katika maisha ya mwananadamu ikiwa ni pamoja na kufanya biashara zao kwa
ufanisi mkubwa.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment