Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akizungumza na Naibu Waziri wa Mambo ya Nje na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) Nd,Guo Yezhou (kushoto) wakati alipofika Ikulu Mjini Zanzibar leo akiwa na Ujumbe wake,[Picha na Ikulu] 25/10/2019.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.
Ali Mohamed Shein amesema kuwa Zanzibar itaendelea kuthamini uhusiano na
ushirikiano uliopo kati yake na Jamhuri ya Watu wa China sambamba na Chama
chake cha Kikomunisti cha (CPC).
Rais Dk. Shein ametoa kauli
hiyo leo Ikulu mjini Zanzibar wakati
alipofanya mazungumzo na Naibu Waziri wa
Mambo ya Nje na Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama Cha Kikomunisti cha China (CPC),
Guo Yezhou.
Katika mazungumzo
hayo, Rais Dk. Shein alisema kuwa huwezi kuyataja maendeleo ya Zanzibar bila ya
kuihusisha Jamhuri ya Watu wa China kupitia Chama Cha Kikomunisti cha China
(CPC), hiyo ni kutokana na uhusiano na ushirikiano mwema na wa kihistoria.
Rais Dk. Shein alisema
kuwa Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China imeifanyia mambo mengi Jamhuri ya
Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar kwa uungaji mkono wake katika kuimarisha
sekta za maendeleo.
Akitoa ushuhuda jinsi
ya Jamhuri ya Watu wa China ilivyoisaidia Zanzibar katika kuimarisha sekta za
maendeleo ikiwemo afya, elimu, viwanda, kilimo, sekta ya habari, miundombinu,
michezo na mengineyo Rais Dk. Shein alisema kuwa nchi hiyo ni marafiki wa kweli
kwani imeanza ushirikiano mara tu baada ya Mapinduzi matukufu ya Januari 12,
1964.
Aliongeza kuwa mbali
ya Serikali ya China kusaidia sekta hizo ikiwa ni pamoja na ujenzi wa kiwanda
cha Sukari Mahonda, Kiwanda cha Sigareti Maruhubi, Viwanda vyenginevyo pia,
nchi hiyo imeleta Mapinduzi makubwa katika sekta ya elimu kwa kutoa nafasi
nyingi za masomo nchini mwake.
Alieleza kuwa kubwa
kuliko yote hayo ni ukarabati mkubwa wa Hospitali ya Abdalla Mazee Mkoani
Pemba, Ukarabati wa uwanja wa Mao Zedong pamoja na ujenzi wa uwanja wa ndege
Terminal III.
Aidha, Rais Dk. Shein
alimueleza kiongozi huyo haja ya kukuza ushirikiano uliopo kati ya Chama Cha Mapinduzi (CCM) na Chama Cha
Kikomunisti cha China (CPC) pamoja na Serikali mbili za Jamhuri ya Muungano wa
Tanzania na Serikali ya Jamhuri ya Watu wa China kama ulivyofanywa na waasisi
wake Hayati Mwalimu Julius Nyerere na Mwenyekiti Mao Zedong.
Alieleza kuwa
ushirikiano huo ulianza tokea mwanzo wa vyama vya ASP, TANU na hatimae kuja kwa
CCM na kueleza urafiki mzuri uliooneshwa na viongozi wa pande mbili hizo kwa
kutembeleana ambao umekuwa ukiendelezwa hadi hivi leo.
Sambamba na hayo, Rais
Dk. Shein alitumia fursa hiyo kutoa shukurani zake kwa Serikali ya Jamhuri ya
Watu wa China kupitia Chama cha Kikomunisti cha China (CPC) kusaidia ujenzi wa Chuo cha Uongozi cha
Mwalimu Julius Nyerere kinachojengwa Wilaya ya Kibaha Mkoni Pwani.
Dk. Shein alitoa
pongezi na salamu kwa Rais wa Jamhuri ya Watu wa China na Mwenyekiti wa (CPC)
Xi Jinping kwa kuendelea kuiunga mkono Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo
Zanzibar.
Rais Dk. Shein alisema
kwamba hatua ya ujenzi wa chuo hicho kupitia Chama cha Kikoministi cha China (CPC)
ambacho ndicho kinachojenga zinaendeleza uhusiano na ushirikiano wa kihistoria
uliopo baina ya Jamhuri ya Watu wa China na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Nae Naibu Waziri wa
Mambo ya Nje ambaye pia ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama Cha Kikomunisti cha
China (CPC) Guo Yezhou alitoa pongezi kwa mapokezi mazuri aliyoyapata yeye na
ujumbe wake tokea walipowasili nchini Tanzania.
Alisema kuwa miongoni
mwa lengo la ujio wake ni kuendeleza uhusiano na ushirikiano uliopo kati ya
Jamhuri ya Watu wa China na Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ikiwemo Zanzibar
huku na yeye akitumia fursa hiyo kutoa salamu za Rais Xi Jinping kwa Rais Dk.
Shein.
Naibu Waziri huyo wa
Mambo ya Nje ambaye pia, ni Mjumbe wa Kamati Kuu ya Chama cha (CPC), alimueleza
Rais Dk. Shein kuwa chuo hicho ni kwa ajili ya kutoa mafunzo ya uongozi kwa
nchi sita zenye vyama vya ukombozi vilivyoshirikiana na (CPC) ambavyo ni (CCM),
(ANC), (ZANU-PF), (FRELIMO), (MPLA) na (SWAPO) cha Namibia.
Kiongozi huyo
alimueleza Rais Dk. Shein kuwa kutokana na China kuthamini juhudi za Tanzania
ilizozichukua katika kuiunga mkono nchi hiyo ndipo Rais Xi Jinping alitoa tunzo
kwa Waziri Mkuu Mstaafu Dk. Salim Ahmed Salim hivi karibuni ikiwa ni kutambua
mchango wake mkubwa katika kuiwezesha China kuwa mwanachama wa Umoja wa Mataifa
(UN).
Pia, Kiongozi huyo
alimuhakikishia Rais Dk. Shein kuwa China itaendelea kuiunga mkono Zanzibar
katika kuimarisha miradi mbali mbali ya maendeleo na kupongeza miradi ambayo
tayari imeshakamilika huku akisisitiza kuwa bado nchi hiyo itaendeleza hatua
zake za kuisaidia Zanzibar ikiwemo kuleta wataalamu wakiwemo madaktari kutoka
Jimbo la Jingsu.
Alisisitiza kuwa Chama
cha (CCP) kitaendeleza uhusiano na ushirikiano wake na Chama Cha Mapinduzi
kwani vyama hivyo vina historia kubwa ambayo kuna kila sababu ya kuiimarisha
ambapo katika ujumbe wake alifuatana na Balozi mdogo wa China Xie Xiaowu ambapo
pia, Naibu Katibu Mkuu wa CCM Zanzibar Abdalla Juma Mabodi alishiriki.
Rajab Mkasaba, Ikulu
Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax:
024 2231822
E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment