Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi na Mkuu wa Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) Mhe.Dk.Ali Mohamed Shein akihutubia wakati wa hafla ya Mahafali ya 15 ya Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA) yaliofanyika katika Ukumbi wa Dk. Ali Mohamed Shein Tunguu Wilaya ya Kati Mkoa wa Kusini Unguja.
RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la
Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein amesema ni muhimu kwa programu ya Ufundishaji
wa Kiswahili kama lugha ya pili (TEKSOL), ikaanzishwa katika ngazi ya
stashahada na shahada, ili vijana wengi zaidi waweze kujifunza namna ya
ufundishaji wa lugha hiyo.
Dk. Shein amesema hayo katika sherehe za mahafali ya 15 kwa Wahitimu wa
mwaka wa masomo 2018/2019 ya Chuo Kikuu cha Taifa Zanzibar (SUZA), zilizofanyika katika
Ukumbi wa Dk.Ali Mohamed Shein Campus ya Tunguu, Mkoa wa Kusini Unguja.
Dk. Shein ambae pia ni Mkuu wa Chuo hicho alisema uanzishaji wa
Programu ya Ufundishaji wa Kiswahili kama lugha ya pili, utasaidia kuongeza
fursa za ajira kwa vijana wa Zanzibar kwenda kufundisha Kiswahili ndani na nje
ya nchi; wakati huu ambapo nchi mbali mbali duniani zimeanza kufundisha lugha
hiyo katika vyuo Vikuu.
“Kwa hivyo, sisi ambao lugha ya Kiswahili ndio lugha yetu mama, lazima
tuwe mbele na tuamini kuwa tuna uwezo mkubwa zaidi wa kufundisha Kiswahili
fasaha, kwani ndicho kilichotulea na kutukuza na vile vile, tunaujua utamaduni
wake”, alisema.
Aliwataka Wahitimu wa masomo hayo kufanya kila juhudi kutafuta fursa za kwenda kufundisha Kiswahili katika
nchi mbali mbali duniani, ikiwemo za Jumuiya ya Maendeleo ya Nchi za Kusini mwa
Afrika (SADC).
Aidha, aliwataka wahitimu kuchukua
hatua ya kuwasiliana na taasisi zinazohusika pamoja na kufuatilia katika
mitandao, ili kuhakikisha wananufaika na
fursa hizo.
Alieleza kuwa katika hafla ya ufunguzi wa Kongamano la Kimataifa la
Kiswahili lililofanyika hivi karibuni, alifurahia hatua ya kukabidhiwa idadi
kubwa ya tasnifu za wataalamu waliohitimu katika fani za lugha ya Kiswahili
katika ngazi ya Shahada ya Uzamivu na Shahada ya Uzamili kutoka vyuo vikuu
mbalimbali nchini, ikiwemo SUZA.
Alisema kuwepo kwa hazina kubwa ya
wataalamu wenye shahada za juu katika Kiswahili, ikiwemo Tasnifu 17 za Uzamivu
(PhD) na 95 za Uzamili (Masters), kunapaswa
kwenda sambamba na maandalizi ya kuanzisha Skuli ya Tafsiri na Ukalimani,
akibainisha hatua hiyo italiwezesha
Taifa kuandaa wataalamu waliobobea wa fani za tafsiri na ukalimani katika masuala ya mawasiliano ikiwemo
mikutano ya Kimataifa.
Aidha, alitaka juhudi zifanyike kuimarisha
Skuli ya Kiswahili na Lugha za Kigeni ili
ifikie kuwa Kitivo Kikuu na kuifanya Zanzibar kuwa Kituo Bora,
“Center of Exellence”.
“Ni muhimu tuongeze vifaa na
vivutio vyengine ili kuwafanya wageni wanaotaka kujifunza lugha ya Kiswahili
washawishike kujiunga na taasisi hiyo,
tuandae mipango imara, tuwe na mikakati madhubuti pamoja na kutafuta
nyenzo, kwani wazee walisema mti hawendi ila kwa nyenzo” alisema.
Katika hatua za kukiimarisha chuo
hicho, Dk. Shein alisema uanzishaji wa programu mbali mbali umezingatia
mahitaji ya mipango ya maendeleo na soko la ajira, hatua inayokwenda sambamba
na uanzishaji wa Skuli mpya ya Utibabu wa Meno, na kubainisha kuwa ni jambo linalofurahisha.
Alisema kwa mnasaba na jambo hilo,
Serikali imeamua kuanzisha Taasisi ya Masomo ya Ubaharia pamoja na
kukiunganisha Chuo hicho na Skuli ya Kilimo, kwa kuzingatia upungufu mkubwa wa madaktari wa
meno pamoja na kuzindeleza taaluma za uuguzi na ukunga.
Aidha, alisema kuanza kwa mafunzo
ya Shahada ya Udaktari wa Meno na Shahada ya Uuguzi na Ukunga katika mwaka huu
wa masomo ni hatua nyengine muhimu ya maendeleo katika kuimarisha huduma za
afya nchini.
Alieleza kupatikana kwa wataalamu
wa fani hiyo kutasaidia sana katika kukabiliana na matatizo ya maradhi ya meno
yanayowasumbua wananchi.
Vile vile,alisema wataalamu wa
fani ya uuguzi na ukunga watatoa mchango mkubwa katika kuinua huduma hizo na
kufanikisha utekelezaji wa malengo ya
serikali katika kukabiliana na vifo vya mama wajawazito na watoto wakati wa
kujifungua.
Dk. Shein aliitaka SUZA kuandaa utaratibu wa kutathmini mitaala yake na
kuangalia ubora wa wahitimu wake, katika kuyamudu majukumu yao kulingana na
masomo waliyojifunza wakati wakiwa chuoni.
Alisema chuo kinapaswa kuendelea kubuni programu za masomo ambazo
zitapunguza wahitimu kutegemea zaidi ajira kutoka Serikalini na badala yake
kuweza kujiajiri wao wenyewe.
Alisema Serikali itaendelea kufanya kila linalowezekana kuwasaidia
vijana wanaohitimu, ili waweze kuitumia elimu waliyoipata kujiajiri pamoja na
kuwapatia mikopo ili kuendeleza maisha yao. Aidha, alisema Serikali inaendelea
na juhudi kukamilisha taratibu zitakazowezesha kuwa na fedha za kutosha ili
kuwawezesha wananchi kiuchumi.
Rais Dk. Shein aliwakumbusha wahitimu hao kuwa elimu ni bahari isiyo na mwisho, hivyo
akawataka wasitosheke na hatua
waliyofikia kwa kutambua kuwa jamii ina matarajio makubwa kwao.“Ni vyema
mkaitumia elimu yenu vyema kwa faida yenu na jamii, huku mkizingatia uadilifu,
uzalendo, maadili mema na malezi mema tuloachiwa na wazee wetu”, alisema.
Aliwataka wahadhiri na wafanyakazi wa SUZA kuendelea kutimiza wajibu wao kwa kufanya kazi kwa bidii ili kuhakikisha wanafunzi wanahitimu wakiwa wamebobea na
wenye nidhamu, sambamba na kuuhimiza Uongozi kusimamia Sheria ya Utumishi wa
Umma namba 2 ya mwaka 2011.
Aidha, aliwataka wahadhiri kuzingatia uwiano wa kiwango bora cha elimu na
namna ya kutathmin uwezo wa watahiniwa, pamoja na utoaji wa alama za ufaulu kwa
weledi ili kuepusha migongano, jambo ambalo litateremsha kiwango cha elimu
inayotolewa.
Katika hatua nyengine, Dk. Shein
aliwataka wahitimu wa ngazi ya Uzamivu (Phd), kufanya juhudi katika kufanya
utafiti na kuandika makala za kitaaluma
pamoja na kuandika vitabu, ili
hatimae wafikie daraja la uprofesa.
Alisema Serikali imekuwa ikitenga
bajeti kubwa ya fedha kugharamia huduma
za elimu ikiwemo mishahara ya wahadhiri na wafanyakazi wa chuo pamoja na
uimarishaji wa miundo mbinu ya elimu ikiwemo vitabu na ujenzi wa majengo ya
kisasa na ubadilishaji wa sera, ili kuhakikisha
wanafunzi wanapata nyenzo bora za kujifunzia.
“Sasa hivi kujifunza kumerahisishwa na matumizi ya Teknolojia ya Habari
na Mawasiliano (TEHAMA) hivyo, itumieni vizuri teknolojia hiyo, ili
ikuzidishieni maarifa na ujuzi na wala msiitumie kwa mambo yasiyofaa”, alisema.
Alisema mabadiliko ni jambo la lazima katika maisha ya binadamu na
mazingira yake na kubainisha jukumu la Serikali katika kuwaletea maendeleo watu
wake, akibainisha SUZA ndio hazina na uti wa mgongo katika kufikia maendeleo ya
Zanzibar.
Dk. Shein alitoa shukurani kwa viongozi, wahadhiri
na wafanyakazi wote waliofanya kazi
nae tangu alipokabidhiwa dhamana ya Mkuu
wa Chuo hicho mwaka 2010, wakiwemo wale ambao wamefariki, kustaafu na wengine
kukabidhiwa majukumu mengine.
Nae, Waziri wa
Elimu na Mafunzo ya Amali Riziki Pembe Juma alitoa pongezi kwa Serikali kwa
mafanikio makubwa yaliofikiwa katika kukiendeleza Chuo hicho na hivyo kuwa
chachu katika maendeleo ya kijamii na kuchumi.
Aidha, Makamo
Mkuu wa SUZA, Zakia Abubakar alisema kuendelea kufanya vizuri kwa wahitimu wa
kike ni jambo la kupongezwa linaloonyesha matumizi mazuri ya uwezo wao katika
masomo.
Alisema katika
mahafali ya mwaka huu, wahitimu wa kike wameendelea kufanya vyema kwa kupata
asilimia 54 dhidi ya asilimia 46 za wanaume, huku mwanafunzi bora wa jumla
akiwa mwanamke.
Alisema chuo
hicho kinakabiliwa na changamoto mbali mbali, ikiwemo ya ukosefu wa dahalia,
hususan katika Campus ya Tunguu inayohusisha ukosefu wa maeneo mbali mbali ya
utoaji wa huduma kitaaluma kwa wanafunzi.
Alisema jumla ya
wahitimu 1,719 kutoka fani mbambali wamefaulu na kutunukiwa vyeti, stashahada
pamoja shahada, hatua inayokifanya chuo hicho kufikisha jumla ya wahitimu
12,000 katika kipindi cha miaka 15 sasa.
Katika mahafali
hayo ambayo yalihudhuriwa na Viongozi mbali mbali wa Kitaifa, akiwemo Makamo wa
Rais wa Jamuhuri ya Mauungano wa Tanzania Dk. Mohamed Gharib Bilali na Makamo
wa Pili wa Rais wa Zanzibar Balozi Seif Ali Idd, Rais Dk. Shein alikabidhi
zawadi kwa wanafunzi bora katika ngazi za cheti, Stashahada na Shahada.
Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982.
Fax: 024 2231822
E-mail: abdya062@gmail.com
No comments:
Post a Comment