RAIS wa Zanzibar na
Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein ametoa msamaha kwa
wanafunzi kumi na tisa (19) ambao bado walikuwa wakiendelea kutumikia vyuo vya
Mafunzo vya Unguja na Pemba ikiwa ni miongoni mwa shamra shamra za Sherehe za miaka
56 ya Mapinduzi ya Zanzibar.
Kwa
mujibu wa taarifa iliyotolewa na Katibu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu
Kiongozi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee ilieleza kuwa kwa uwezo aliopewa chini ya
kifungu cha 59 cha Katiba ya Zanzibar 1984, Rais Dk. Shein ameamuru kuwa
kifungo kilichobaki cha wanafunzi walionufaika na msamaha huo, ambao bado
wanaendelea kutumikia katika vyuo vya Mafunzo vya Unguja na Pemba kuwa kipindi
hicho chote kinafutwa na kwamba wanafunzi hao waachiwe huru kuanzia leo tarehe
11 Januari 2020.
Taarifa
hiyo, imeeleza kuwa, kwa kuwa Zanzibar itakuwa inasherehekea miaka 56 ya
Mapinduzi ya Zanzibar hapo kesho tarehe 12 Januari 2020, na kwa kuwa Rais
ameridhika kuwa kuna sababu za kutosha za kutumia uwezo wake huo katika sherehe
hii, wanafunzi hao waachiwe huru.
Walionufaika
na msamaha huo kwa Unguja ni Salum Kombo Juma, Rashid Abdalla Salum, Shaame
Mussa Suleiman, Rajab Juma Suleiman, Mwinyi Abdalla Rajab, Faki Ramadhan Juma,
Abdalla Said Khamis, Omar Khalfan Said, Abdulbaki Abdulaziz Muhammad, Mwinyi
Maulid Haji, Said Ali Seif na Abdalla Ame Khamis.
Aidha,
wengine walionufaika na msamaha huo kwa upande wa Pemba ni Fauzi Abdalla Said,
Is-haka Saleh Ali, Hashim Moh’d Khamis, Ussi Juma Khamis, Juma Salum Moh’d,
Moh’d Khamis Ali na Maulid Abdalla Seif.
Msamaha
huo ambao hutolewa kila mwaka katika kipindi cha sherehe za Mapinduzi matukufu,
huwahusisha wanafunzi ambao ni wazee sana, wenye maradhi sugu au wenye makosa
madogo ambao wamebakisha muda mfupi wa kutumikia chuoni sambamba na kuonesha nidhamu nzuri chuoni na kujutia
makosa yao.
Wanafunzi
wa Chuo cha Mafunzo, wenye makosa kama vile kuua kwa makusudi, wizi wa kutumia
nguvu, wizi wa mali ya Umma, makosa ya kudhalilisha wanawake na watoto, makosa
ya dawa za kulevya na wenye makosa mengi ya zamani kwa kawaida huwa hawapewi
msamaha.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024
2231822
E-mail:
rajabmkasaba@yahoo.co.uk
No comments:
Post a Comment