Habari za Punde

DC CHONGOLO ASITISHA VIBALI VYA UCHIMBAJI MCHANGA MABONDENI KATIKA WILAYA YA KINONDONI

Watu waliokuwa wakifanya shughuli ya kuchimba mchanga katika bonde la Mto Salasala wakipanda miti aina ya miazi, Magugu kwa lengo la kuzuia mmomonyoko wa udongo.
 Nyumba zilizoko pembezoni mwa mto Salasala zilizoathiriwa na bonde hilo.
Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Mhe. Daniel Chongolo akikagua mtambo uliokuwa ukikarabati Mto Salasala jana alipofanya ziara ya kukagua mito ambayo imeathiriwa na watu waliokuwa wakichimba mchanga.

Mkuu wa Wilaya ya Kinondoni Mhe. Daniel Chongolo amesitisha vibali vya uchimbaji mchanga vilivyotolewa na Bodi ya Maji Bonde la Ruvu kutokana na kuleta madhara ya uharibifu wa mito na kusababisha athari kwenye makazi ya watu katika Halmashauri hiyo.

Vibali vilivyositishwa katika ni vile vilivyotolewa kufanya shughuli hizo katika Bonde la mto Salasala, Mto mbezi, Ndumbwi, Nyakasangwe, na kusema kuwa mito hiyo inapita katikati ya makazi ya watu na kwamba baada ya kufanyika marekebisho utawekwa utaratibu upya wa kufanya shughuli hizo.

Akizungumza  mara baada ya kufanya ziara katika Bonde la mto Salasala (Mto Tegeta)  Mhe. Chongolo amesema kuwa amefikia uamuzi huo baada ya wakandarasi  waliopewa vibali hivyo kuharibu mto huo na hivyo kuamuru kupandwa kwa Miti hiyo ambayo itasaidia kuzuia mmomonyoko wa udongo.

Amesema kuwa kinachofanyika hivi sasa ni kurekebisha mito hiyo kwa kupanda miti, magugu pamoja na mianzi inayoshika ardhi ili kuzuia mmomonyoko wa undongo  na hivyo kuweka mkakati wa kuratibu shughuli za utoaji mchanga kufanyika katika maeneo hayo.

Mhe. Chongolo amesena kuwa katika Halmashauri hiyo ameruhusu kibali hicho kutolewa katika bonde la Mpigi kwa maelekezo ya kuhakikisha kuwa shughuli hizo zifanyike kwa ajili ya kusafisha mto ili kuondosha adhari kwani mchanga ukijaa sana husababisha maji kusambaa nje.

“Wakati tunafanya haya ni lazima tusitishe shughuli zote zinazofanyika hapa, tulifanya tathimini ya kuangalia athari kwa kuunda timu ambayo ilikamilisha majukumu yake na kuleta ripoti hiyo Disemba mwaka jana, mwezi wa kwanza mwaka huu tulianza mjadala na wale ambao walipewa kandarasi ya kutoa mchanga kwenye mito hii” amesema Mhe. Chongolo

Nakuongeza kuwa “ baada ya majadiliano hayo,  tulikubaliana  nao kupanda Miazi, Miti na Magugu,  na watu ambao mnawaona hapa asilimia 90 niliagiza kila mwenye kibali cha bonde anayekuja aje na watu 10 kwa ajili ya kushirikiana kupanda miti, na hii miti inayopandwa hapa sijanunua wameleta wao” ameongeza Mhe. Chongolo.

Mhe. Chongolo amesisitiza kuwa “ kwanza mchanga usiondolewe kibiashara ,tutoe mchanga sehemu ambayo tunaona kuwa kunaongezeko ambalo linaweza kusababisha athari, ili turuhusu maji yapite bila kuleta madhara kwa wananchi waliopo pembezoni mwa mto na huyo anayetoa ahakikishe anafanya marekebisho ikiwemo kupanda miti, magugu na mianzi.

Katika hatua nyingine Mhe. Chongolo amesema kuwa " Tunachangamoto ya watu kufanya shughuli za kibinadamu kwenye maeneo ya maji,  Serikali imeshaelekeza watu ambao wapo kwenye maeneo haya wanatakiwa kuwa umbali wa mita 60 kwa 60 , lakini hatufuati hiyo Sheria ya mazingira.

Wananchi mliopo katika maeneo haya, niwasihi sana acheni kufanya shughuli hapa, leo tunapanda miti ili kunusuru bonde hili lisiendelee kukua,   mchanga utatolewa kwa kibali kwa ajili ya kusafisha mto ila sio kuchimba mchanga kwa shughuli ya kibiashara ama nyingine, " amesema Mhe. Chongolo.

Imetolewa na Kitengo Cha Habari na Uhusiano
Halmashauri ya Manispaa ya Kinondoni.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.