Habari za Punde

Wizara ya Kazi Uwezeshaji Wazee Wanawake na Watoto Zanzibar Yawasilisha Utekelezaji wa Mpango Kazi kwa Mwezi wac Julai hadi Disemba 2019 /2020. Wizara Mpango Uo


Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein, akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Kazi Uwezeshaji Wazee Wanawake na Watoto Zanzibar, wakati wa kuwasilisha Taarifa ya Utekelezaji Mpango Kazi kwa mwezi wa Julai hadi Disemba 2019 / 2020, uliofanyika katika ukumbi wa Ikulu Jijini Zanzibar.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk. Ali Mohamed Shein, amesema kuwa kuwepo kwa mazingira ya muhali katika jamii kumeweza kuchangia kwa kiasi kikubwa kudhorotesha mienendo ya kesi za udhalilishaji wa wanawake na watoto.  

Hayo aliyasema leo, Ikulu Jijini Zanzibar alipokutana na uongozi wa Wizara ya Kazi, Uwezeshaji, Wanawake na Watoto wakati ilipowasilisha taarifa ya utekelezaji wa Mpango Kazi  kwa kipindi cha Julai hadi Disemba katika mwaka wa fedha 2019/2020.

Rais Dk. Shein alieleza haja ya kuachana na muhali katika kuzitafutia ufumbuzi kesi za udhalilishaji wa wanawake na watoto na kusisitiza umuhimu wa kusimamia sheria na kutaka sheria kuchukua mkondo wake ili kuondoa malakamiko katika jamii.

Alieleza kuwa juhudi za makusudi zimechukuliwa na Serikali ikiwa ni pamoja na kuunda Kamati Maalum ya kupambana na vitendo vya ushalilishaji wa wanawake na watoto hivyo kuna kila sababu ya kuchukuliwa hatua za kisheria kwa wanaofanya vitendo vya udhalilishaji huo.

Rais Dk. Shein alisisitiza haja ya kuendelezwa mikakati iliyowekwa na Serikali kupitia Wizara hiyo ili kuhakikisha yale yote yaliopangwa yanafanyiwa kazi na hatimae kupata matokeo yaliyokusudiwa.

Alifahamisha kuwa kuna kila sababu ya kupambana na vitendo vya udhalilishaji wa wanawake na watoto kwa kufuata sheria zilizowekwa na kuitaka Wizara hiyo isichoke na isivunjike moyo katika kukabiliana na vitendo hivyo kwani ni miongoni mwa kazi iliyokabidhiwa kusimamia hayo.

Alisema kuwa mambo hayo yanahitaji nguvu za pamoja kwani hayo ni mapambano makubwa yanayofanywa na watu ambao wamekosa haya kutokana na kufanya vitendo hivyo vya kinyama.

Sambamba na hayo, Rais Dk. Shein aliitaka Wizara hiyo kufanya kazi kwa pamoja, kuendelea kushirikiana, kuongeza uzalendo kwenye kazi zao pamoja na kuwa waadilifu, waaminifu na watiifu sambamba na kuwa wabunifu katika kazi.

Aidha, Rais Dk. Shein alieleza umuhimu wa kuundwa kwa Sheria ya Wazee ambayo Serikali imeamua kuiunda kwa makusudi ambapo mbali ya mambo mengine pia, Sheria ndani yake yamo masuala ya Pencheni ya Jamii yatakuwemo hatua ambayo itaondosha wasi wasi mkubwa wa wazee juu ya kuendelea kwa Pencheni yao hiyo.

Nae Makamu wa Pili wa Rais Balozi Seif Ali Idd aliipongeza Wizara hiyo na kueleza haja ya kutafutwa njia za kuondosha udhalilishaji huku akipongeza hatua zinazochukuliwa na Wizara hiyo katika kufuatilia mikopo wanayoitoa kwa wananchi.

Nae Katibu Mkuu Kiongozi na Katibu wa Baraza la Mapinduzi Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliipongeza kazi nzuri ya utayarishaji na uwasilishaji iliyofanywa na Wizara hiyo na kuutaka uongozi wa Wizara hiyo kuendelea kushirikiana.  

Mapema Waziri wa Kazi, Uwezeshaji Wazee, Wanawake na Watoto Maudline Cyrus Castico akisoma utangulizi wa taarifa hiyo kwa niaba ya Wizara anayoiongoza ilimpongeza Rais Dk. Shein kwa kutekeleza vyema Ilani ya Uchaguzi ya CCM.

Aidha, Waziri Castico alieleza kuwa  Dira ya Wizara hiyo ni kuwa na jamii ya Wazanzibari yenye ajira za staha, ubunifu na uwezo wa kukabiliana na umasikini, inayotoa haki na fursa sawa kwa watu wa makundi yote.

Waziri Castico alileza kuwa Dira hiyo  inatekelezwa kwa kuimarisha upatikanaji wa kazi na ajira zenye staha, kukuza usawa wa kijinsia na kuwawezesha wanawake,  vijana, wazee na watoto kwa kusimamia utekelezaji wa sheria na kanuni za kazi.

Aliongeza kuwa Wizara hiyo imeanzishwa kwa lengo la kusimamia utekelezaji wa sheria na miongozo ya kazi, kuratibu upatikanaji wa ajira za staha hasa kwa vijana, kuimarisha program za kuwawezesha wananchi kiuchumi na kuimarisha haki, ustawi na maendeleo ya wanawake, watoto, wazee na wanaoishi katika mazingira magumu.

Aidha, Waziri huyo alieleza majukumu yaliyotekelezwa na Wizara yake kwa kipindi cha miezi sita ikiwa ni pamoja na kuunga umeme wa jua katika nyumba 150 katika kijiji cha Makoongwe Pemba na Mbuyu Tende Unguja kupitia mradi wa “Barefoot Zanzibar”

Pia, kwa maelezo ya Waziri Castico Wizara imeweza kutunisha Mfuko wa Uwezeshaji Wanawake Kiuchumi kwa ongezeko la TZS  Milioni 161 ambapo ni sawa na asilimia 230 ya lengo walilojipangia kwa miaezi 6.

Nao viongozi wa Wizara hiyo walieleza mafanikio yaliopatikana katika Wizara hiyo na kueleza mikakati yao waliyoiweka katika kuhakikisha wanafikia malengo ya kuwatumikia wazee,  wanawake pamoja na watoto huku wakisisitiza kuimarisha mashirikiano waliyonayo.

Aidha, walipongeza utaratibu wa mikutano hiyo ambayo walisema imeweza kusaidia utendaji wa kazi zao na kutumia fursa hiyo kumpongeza Rais Dk. Shein kwa jinsi anavyowaongoza.
Rajab Mkasaba, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777427449. Fax: 024 2231822 
 E-mail: rajabmkasaba@yahoo.co.uk

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.