Habari za Punde

MAJALIWA: SERIKALI IMEFUNGA VYUO VYA KATI, VIKUU KUJIKINGA NA CORONA

Waziri Mkuu Kassim Majaliwa akizungumza na waandishi wa habari, Dar es Salaam jana kuhusu hatua za awali zilizochukuliwa na Serikali kutokana na kuwepo kwa maambukizi ya virusi vya ugonjwa wa Corona nchini. 
Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu.

SERIKALIimeagiza vyuo vyote vya elimu ya kati na vya elimu ya juu vifungwe kwa muda wa siku 30 kuanzia leo Machi 18, 2020 ili kuondoa msongamano katika maeneo hayo na kuweza kujikinga na virusi vya corona. 

Amesema hadi leo, nchini kuna jumla ya watu watatu waliobainika kuwa na virusi vya corona ikiwa ni ongezeko la wagonjwa wawili, mmoja ni raia wa Ujerumani (24) aliyegundulika Zanzibar na mwingine ni raia wa Marekani (61) aliyegundulika Dar es Salaam. Wote wapo katika uangalizi.

Waziri Mkuu ametoa kauli hiyo leo (Jumatano, Machi 18, 2020) wakati akizungumza na waandishi wa habari kwenye makazi ya Waziri Mkuu, Oysterbay, jijini Dar es Salam. 

Waziri Mkuu amesema kwa sasa wanafunzi wengi wa vyuo wamefunga, hivyo amewataka wasirudi vyuoni hadi watakapotaarifiwa na walioko vyuoni wametakiwa warejee majumbani kwao ili kuondoa msongamano kwenye maeneo hayo.

“Vyuo vya ualimu wanafunzi wake walitakiwa kufanya mitihani mwezi Mei, Waziri wa Elimu, Sayansi na Teknolojia atafanya taratibu za kurekebisha  ratiba ya mitihani kulingana na matokeo ya hali ya maambukizi.”

Waziri Mkuu amewasisitiza wananchi waendelee na shughuli zao kwa umakini na wasiwe na taharuki kwani Serikali inaendelea kulifanyia tathmini suala hilo na kwamba itakuwa inatoa taarifa kadiri inavyohitajika.

Hata hivyo, Waziri Mkuu amesema huduma katika  maduka, masoko na za usafiri ziendelee kutolewa kama kawaida ila kwa umakini mkubwa na kwenye vyombo vya usafiri wa umma wahusika wahakikishe hawajazi sana abiria.

Jana, Machi 17, 20202 Serikali ilitanga kuzifunga shule zote za awali, msingi na sekondari  kwa muda wa siku 30 na kwamba wanafuzi wa kidato cha sita waliopaswa kuanza mitihani Mei 4, 2020 nao watapaswa kusibiri Wizara ifanye utaratibu mwingine kulingana na matokeo ya hali ya maambukizi.

Waziri Mkuu alisema mikusanyiko yote mikubwa ya ndani na nje isiyo ya lazima imesitishwa kuanzia sasa ikiwemo shughuli za michezo, matamasha ya muziki, mikutano mbalimbali ikiwemo ya shughuli za kisiasa, mahafali na shughuli nyingine za kijamii. 

Alizitaka wizara na taasisi zizitishe semina, warsha, makongamano na mikutano yote hapa nchini ambayo inahusisha washiriki toka nchi zenye maambukizi makubwa. “Watanzania wenye safari zisizo za lazima kwenye nchi zenye maambukizi makubwa, wanashauriwa wasitishe safari hizo,” alisisitiza.

Akielezea hatua nyingine zinazochukuliwa na Serikali ili kudhibiti ugonjwa huo, Waziri Mkuu alisema: “Serikali imesitisha michezo yote inayokusanya makundi ya watu ikiwemo Ligi Kuu ya Tanzania Bara (VPL), Ligi Daraja la Kwanza (FDL), Ligi Daraja la Pili (SDL) na aina nyngine. Wizara ya Habari, Utamaduni, Sanaa na Michezo iziandikie taasisi zake.”

Pia aliwataka Wakuu wa Mikoa na Wilaya wahakikishe maeneo yote yaliyobainishwa na kutengwa (vituo vya huduma na ufuatiliaji) kwa ajili ya kuwahudumia wagonjwa endapo watajitokeza katika maeneo yao yanakuwa na mahitaji yote muhimu na yanahudumiwa ipasavyo.

Alisema Watanzania hawana budi kuzingatia ushauri unaotolewa na Serikali na kupuuza taarifa za uzushi zinazosambazwa kwenye mitandao ya kijamii. “Watanzania tuache mzaha wa kutumia mitandao ya kijamii kufanya upotoshaji wa tahadhari katika jambo hili,” alionya.

Kuhusu viongozi wa dini, Waziri Mkuu aliwaomba waendelee kushirikiana na Serikali katika kuwaelimisha waumini wao wote kuzingatia tahadhari za ugonjwa huu. Pia amevitaka vyombo vyote vya habari vishirikiane na Serikali katika utoaji wa elimu kwa umma kuhusu kujikinga na Corona bila kufanya upotoshaji wala kuipa jamii hofu.

Aliwataka wananchi watoe taarifa kuhusu uwepo wa mgonjwa au kupata ufafanuzi kuhusu ugonjwa huu kupitia namba za bure za 0800110124, 0800110125 na 0800110037.

IMETOLEWA NA:
OFISI YA WAZIRI MKUU,
JUMATANO, MACHI 18, 2020.

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.