Habari za Punde

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Mhe.Dk. Ali Mohamed Shein Azungumza na Uongozi wa Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora Zanzibar.

Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi Dk.Ali Mohamed Shein (kulia) akizungumza na Uongozi wa Wizara ya Nchi Ofisi ya Rais Utumishi wa Umma na Utawala Bora  katika kikao cha utekelezaji wa Mpango kazi kwa kipindi cha  Julai-Disemba 2019 katika ukumbi wa Ikulu Mjini Zanzibar,(kushoto) Katibu Mkuu wa Wizara hiyo Nd,Yakout Hassan Yakout.

RAIS wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dk. Ali Mohamed Shein  amesema viongozi wote wa Serikali wana wajibu wa kusajili taarifa za mali na madeni kwa uwazi, ikiwa ni hatua muhimu katika kukamilisha dhana ya utawala bora.

Dk. Shein amesema hayo Ikulu jijini Zanzibar, wakati akipokea taarifa ya utekelezaji wa mpango kazi kwa Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala Bora kwa kipindi cha kuanzia Julai hadi Disemba 2019/2020.

Alisema ni wajibu wa viongozi wote nchini kubainisha kwa usahihi na kwa uwazi mali na madeni waliyonayo, na kueleza kuwa hakuna sababu ya viongozi kuficha mali zao.

Alipongeza uongozi wa  Tume ya Maadili na Viongozi wa umma kwa kutambua dhima kubwa iliyokabidhiwa na Taifa pamoja na kutekeleza vyema majukumu yao, ambayo yanawahusisha viongozi wote wa umma.

Aidha, aliipongeza Tume ya Maadili ya Viongozi wa Umma kwa kufanya kazi zake kuambatana na misingi ya haki na demokrasia na kutoa fursa ya kujieleza kwa viongozi wanaotuhumiwa.

Alisema ana matumaini makubwa  ofisi hiyo itaweza kupata mafanikio makubwa katika siku za usoni kutokana na kasi kubwa ya utendaji kazi inayochukuliwa na watendaji wake.

Katika hatua nyengine,   Dk. Shein  aliutaka uongozi wa Chuo cha Utawala wa Umma (IPA) kuendelea kutekeleza malengo ya utoaji wa mafunzo kwa watumishi wa umma na wananchi mbali mbali ili kuwajengea uwezo, sambamba na kuliwezesha Taifa kuwa na  wigo mpana wa wataalamu.

Alipongeza juhudi zinazofanywa na uongozi wa chuo hicho  katika utoaji wa taaluma kupitia viwango tofauti vya elimu.

Nae, Katibu Mkuu wa Baraza la Mapinduzi na Katibu Mkuu Kiongozi, Dk. Abdulhamid Yahya Mzee aliipongeza Uongozi wa Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala bora kwa juhudi kubwa wanazoendelea kuchukuwa katika kusimamia na kupanga vyema maslahi na stahiki mbali mbali za watumishi wa umma, hatua iliyowezesha kuleta utulivu mkubwa kwao.

Alishauri Ofisi hiyo kuharakisha utoaji wa matokeo kwa wananchi na wanavyuo wanaofanya usaili wa nafasi mabali mbali za kazi, akibainisha kuwepo kwa utaratibu unaochukuwa muda  mrefu hivi sasa hadi  kukamilisha mchakati wa ajira kwa watumishi wapya.

Alisema baadhi ya nyakati hali hiyo imekuwa ikiipotezea Serikali watumishi wenye sifa na viwango bora vya elimu baada ya wananchi hao kuchukuliwa na taasisi nyengine binafsi au kujiunga na taasisi zilizoko   Tanzania Bara kutokana na ucheleweshaji huo.

Aidha, Dk. Abdulhamid aliushauri uongozi wa Ofisi hiyo kuzingatia kwa kina changamoto ya  kuwepo kwa makundi ya watumishi kutoka baadhi ay Idara/taasisi za Serikali wanaokwenda mafunzoni na baadae kubadili kada, jambo alilosema limekuwa likiziathiri  idara/taasisi wanazotoka.   

Mapema, kwa niaba akiwasilisha taarifa ya utekelezaji ya Mpango kazi ya Ofisi ya Rais, Utumishi wa Umma na Utawala bora kwa kipindi cha Julai hadi Disemba, 2019/2020, Waziri Ofisi ya Rais na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Issa Haji Ussi ‘Gavu’ alisema Wizara hiyo imepata mafanikio makubwa katika utekelezaji wa mpango huo kupitia programu mbali mbali.

Alisema mafanikio hayo yamefikiwa kutokana na upatikanaji wa fedha wa shilingi 6,587,048,945/ ikiwa sawa ni asilimia 93 ya fedha zilizokadiriwa kutumika katika kipindi hicho.

Alisema miongoni mwa mafanikio hayo ni pamoja na kuandaa miongozo ya usimamizi wa TEHAMA katika taasisi ya udhibiti wa viwango na kutoa ushauri wa kitaalamu katika aunzishaji wa mfumo wa Elektronik katika shughuli za uendeshaji na utoaji wa mizigo bandarini.

Alisema Wizara ilifanya mapitio ya sheria ya Utumishi wa umma ya mwaka 2011 na kuandaa mapendekezo ya marekebisho ya sheria hiyo pamoja na kanuni zake.

Aidha, alisema ilifanikiwa kuingiza taarifa za awali za viongozi katika mfumo wa kielektronik wa kusajili taarifa za mali na madeni ya viongozi.

Sambamba na hayo Waziri Gavu  alisema Wizara hiyo ilitowa elimu ya uelewa kwa maafisa utumishi na mamlaka, mashirika na taasisi zinazojitegemea kuhusu muongozo wa fomu ya upimaji utendaji kazi pamoja na fomu ya upandishwa vyeo kwa watumishi wa umma.

Vile vile, alisema Wizara ilifanikiwa kukamilisha ripoti ya hali ya rushwa na uhujumu uchumi ya mwaka 2019.

Alieleza kuwa katika kipindi hicho Wizara ilikusanya jumla ya shilingi 53,363,982/ kutokana na ada ya ukaguzi wa Hesabu za mashirika na taasisi mbali mbali, ikiwa sawa na asilimia 59 ya makadirio.

Aidha, Mwenyekiti wa Tume ya Maadili ya Viongozi wa umma Asaa Ahmad Rashid alisema kumekuwepo uwasilishaji mzuri wa taarifa za mali na madeni ya viongozi wa umma na kubainisha kuwa hadi Disemba, 2019 jumla ya viongozi 2,300 walikuwa wamewasilisha taarifa zao katika Ofisi hiyo.

Hata hivyo, alisema kuna baadhi ya viongozi huchelewa kuwasilisha taarifa zao kwa wakati, sambamba na viongozi wengi hususan wale ambao hawako katika ngazi za uteuzi, ikiwemo wahasibu  na wakaguzi wa ndani ambao  hushindwa kabisa kuwasilisha taarifa zao.

Abdi Shamna, Ikulu Zanzibar
Postal Address: 2422 Tel.:0777476982. Fax: 024 2231822 
 E-mail: abdya062@gmail.com

No comments:

Post a Comment

ZanziNews Copyright © 2014

Theme images by Bim. Powered by Blogger.